Mlima Kilimanjaro kutumika kutangaza vita dhidi ya Malaria
Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda amesema Mlima Kilimanjaro unaweza kutumika vizuri
zaidi kwenye vita ya kupambana na ugonjwa wa malaria kwa wanamichezo na watu mashuhuri
kuupanda mlima huo na kuchangisha fedha za kusaidia kampeni ya kupambana na ugonjwa
huo.
Alitoa kauli hiyo Jumamosi, Februari 9, 2013 wakati akihojiwa na waandishi
wa habari mara baada ya kushiriki mjadala kuhusu juhudi za Serikali katika kupambana
na ugonjwa wa malaria uliofanyika kwenye kituo cha mikutano cha Sandton, kilichopo
jijini Johannesburg, Afrika Kusini. Alisema katika majadiliano yake na baadhi ya wajumbe
walioshiriki mjadala huo, wengi waliunga mkono wazo alilolitoa la kutumia Mlima Kilimanjaro
katika kampeni za kupambana na ugonjwa huo.
“Nimeongea na baadhi ya wajumbe
katika hafla hii hapa Johannesburg, wengi wameliafiki wazo la kutumia Mlima Kilimanjaro
kutangaza mapambano haya... kila mwanamichezo atakayepanda mlima huu atatangazwa kwamba
ameshinda vita dhidi ya malaria na fedha atakayochangisha itatumika katika kampeni
ya kupambana na malaria barani Afrika,” alisema.
Alipoulizwa ni kitu gani cha
tofauti alichojifunza katika mjadala huo, Waziri Mkuu alisema jambo kubwa aliloliona
ni jinsi ya kutumia mbinu mbadala za kupeleka ujumbe kuhusu mapambano dhidi ya malaria.
“Kila mtu ana dhamana ya kuchangia vita dhidi ya malaria. Hawa wenzetu wameitisha
viongozi wa makampuni makubwa kutoka Afrika Kusini na nje ya nchi hiyo, wako wadau
mbalimbali jioni ya leo walioshiriki mjadala huu,” alisema.
Akitoa mfano wa
Tanzania, Waziri Mkuu alisema tangu mwaka 2000 idadi ya wagonjwa wa malaria imekuwa
ikishuka lakini vilevile idadi ya wafadhili wanaochangia jitihada za kupambana na
ugonjwa huo nayo pia imekuwa ikishuka. Ndiyo maana nimesema kuna haja ya kutumia wadau
wengine kama vile Bunge, NGOs na Serikali za Mitaa ili kuona wanaweza kusaidia vipi
katika vita hiyo,” alisema.
“Wenzetu hawa, (akimaanisha - Muungano wa Mashirika
ya Kimataifa yanayopambana dhidi ya Ugonjwa wa Malaria – United Against Malaria (UAM)
wametumia mashindano ya AFCON kupeleka ujumbe wa kupambana na ugonjwa huu unaoua watu
wengi Afrika sababu ni moja tu: watu wengi wanapenda mpira wa soka iwe uwanjani au
kuangalia kwenye luninga kwa hiyo wanajua fika kuwa ujumbe ukitolewa pale utawafikia
watu wengi sana na kwa haraka zaidi. Sisi Tanzania tulishaanza na sasa tunaangalia
uwezekano wa kutumia basketball, netball na michezo mingine kufikisha ujumbe huu,”
alisema.
Mwenyekiti wa Umoja wa Wabunge wanaopambana na Malaria (TAPAMA- Tanzania
Parliamentarians Against Malaria), Bi. Riziki Lulida ambaye alikuwa miongoni mwa wajumbe
waliofuatana na Waziri Mkuu Afrika Kusini, alisema Tanzania bila Malaria inawezekana
na wao kama Wabunge wanaweza kwenda vijijini kutoa elimu kwa wananchi jinsi ya kujikinga
na ugonjwa huo.
Naye Dk. Hamisi Kigwangalla ambaye ni Makamu Mwenyekiti wa
TAPAMA alisema atatumia fursa ya kushiriki mjadala huo kama njia ya kujifunza mbinu
mbadala za kuishirikisha jamii kwenye vita dhidi ya ugonjwa wa malaria. “Leo tumeona
wenzetu wakiwatumia watu maarufu kama Yvonne ChakaChaka, Mark Fish – mchezaji wa zamani
wa BafanaBafana na pia Drogba yuko kwenye matangazo yao kuhamasisha wananchi watumie
vyandarua kujikinga na malaria… sisi pia tunaweza kutumia wasanii na wanamichezo wetu
kuelimisha umma kuhusu mapambano dhidi ya malaria,” alisema.
Naye Mbunge wa
Chonga, Pemba, Dk. Haroub Mohammed Shamisi ambaye pia ni mjumbe wa TAPAMA alisema
ushirikishwaji mkubwa wa jamii kwenye vita dhidi ya malaria umesaidia sana kushusha
viwango vya maambukizi ya malaria kule Zanzibar.
“Zanzibar imepiga kasi sana
katika vita hii na sababu kubwa iliyochangia ni ushirikishwaji wa karibu wa wananchi
kwenye kampeni dhidi ya malaria. Baadhi ya wabunge tuliamua kuungana ili tupeleke
ujumbe huu kwa wananchi kwa urahisi ili tuweze kufanikiwa kwa haraka zaidi,” alisema.