Mchango wa sekta binafsi katika mapambano dhidi ya Malaria Barani Afrika
Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda amesema makampuni yapatayo 22 yamejiunga na
Mpango wa Kupambana na Malaria kupitia sekta binafsi na sekta ya michezo (Malaria
Safe Companies) ikiwa ni kuunga mkono juhudi za Serikali za kushirikiana na sekta
binafsi kumaliza kabisa ugonjwa huo. Alitoa kauli hiyo Jumamosi, Februari 9, 2013
wakati akishiriki mjadala kuhusu juhudi za Serikali katika kupambana na ugonjwa wa
malaria uliofanyika kwenye kituo cha mikutano cha Sandton, kilichopo Jijini Johannesburg,
Afrika Kusini.
Amesema si jambo rahisi kuiachia Serikali peke yake iendeshe
mapambano dhidi ya ugonjwa huo, ndiyo maana Serikali ya Tanzania iliamua kutumia mfumo
wa kushirikisha sekta binafsi ili kuongeza chachu katika kampeni hiyo. “Ugonjwa wa
Malaria hauna mipaka. Huwezi kusema mbu ataishia Tanzania, Zimbabwe, Malawi au Afrika
Kusini tu. Tunapaswa kuungana pamoja, na mimi natamani kuona nchi zetu zikiungana
kupambana na ugonjwa huu,” alisema.
Alisema mpango huo ulianza mitatu iliyopita
lakini ulizinduliwa rasmi mwishoni mwa mwaka jana. Aliyataja baadhi ya makampuni hayo
ni Bakhresa, Kampuni za Bia za SBL na TBL, SONGAS, NSSF, PPF na Shirikisho la Mpira
wa Miguu (TFF). Tanzania ni nchi ya pili kati ya 12 barani Afrika zilizojiunga na
Mpango huo. Alilitaka Shirikisho la Soka Barani Afrika (CAF) kutumia fursa ya mashindano
hayo yanayofikia kilele chake leo, lichukulie mapambano haya kama changamoto ya kuziunganisha
nchi wanachama wa SADC katika mapambano dhidi ya malaria kwani katika ngazi ya Umoja
wa Afrika (AU) suala hilo limekwishapiga hatua.
Mjadala huo uliwashirikisha
Waziri wa Afya wa Afrika Kusini, Dk. Aaron Motsoaledi na Naibu Waziri wa Afya wa Msumbiji,
Dr. Nazira Vali Abdulla ambao walihojiwa na mtangazaji wa habari za michezo wa kituo
cha televisheni cha SuperSport, Bi. Carol Tshabalala ikiwa imebakia siku moja tu kufanyika
kwa fainali za Kombe la Mataifa Afrika (AFCON 2013).
Mjadala huo uliandaliwa
ili kuzihimiza serikali za nchi za Afrika kuongeza juhudi katika kupambana na malaria
ambao unaongoza kwa vifo vitokanavyo na ugonjwa huo. Mahojiano hayo yatarushwa leo
usiku kwenye fainali za michuano hiyo itakayozikutanisha timu za Nigeria na BurkinaFaso.
Kwa
mujibu wa Shirika la Afya Duniani, takwimu za mwaka 2011 zinaonyesha kuwa kati ya
vifo 655,000 vinavyotokana na malaria kila mwaka, asilimia 91 ya vifo hivyo inatokea
barani Afrika. Na asilimia 86 ya vifo hivyo, huwakumba watoto walio chini ya umri
wa miaka mitano.
Ili kupambana na ugonjwa huo, bara la Afrika linagharimika
kutumia kiasi cha dola za marekani bilioni 12 kila mwaka zikiwa ni kwa ajili ya matibabu
na muda ambao unapotea kwa wafanyakazi kukosa kufanya kazi au wananchi kushindwa kufanya
shughuli za uzalishaji.
Naye mwanamuziki maarufu nchini Afrika Kusini, ambaye
pia ni Balozi wa Kupambana na Malaria barani Afrika, Bi. Yvonne ChakaChaka ambaye
alishiriki chakula cha jioni mara baada ya mjadala huo, alisema wadau wengi zaidi
wanahitajika kushiriki kampeni hii ifike mahali idadi ya vifo vya watoto wachanga
ipungue.
”Nilipoanza kufanya uhamasishaji wa kupambana na malaria ni Ethiopia
pekee ambao walikubali kushirikiana nami. Wakati huo kila sekunde 30 mtoto mmoja alikuwa
anakufa kutokana na ugonjwa huo, lakini sasa hivi imefikia kila baada ya dakika moja,”
alisema.
”Zinatakiwa jitihada zaidi za wadau wote ili ifike mahali tuseme
mtoto mmoja anapoteza maisha kwa ugonjwa huu kila baada ya saa moja, siku moja au
kila baada ya wiki moja na pengine tufike mahali iwe hakuna kabisa vifo vya aina hiyo
,” alisema.
Alisema anaujua ubaya wa malaria kwa sababu mmoja wa wanamuziki
wake alipoteza maisha kutokana na ugonjwa huo. “Ni lazima tuunganishe nguvu katika
vita dhidi ya malaria la sivyo vizazi vijavyo vitatuhukumu. Tunaweza kumaliza ugonjwa
huu, kila mmoja akitimiza wajibu wake,” alisisitiza.