2013-02-11 08:51:13

Jifunzeni kwa imani na matumaini Fumbo la Msalaba wa Kristo: kielelezo cha huruma, upendo na msamaha wa kweli!


Askofu mkuu Josephat Lebulu wa Jimbo kuu la Arusha, Tanzania, katika mahojiano na Radio Vatican anasema, maadhimisho ya Siku ya Wagonjwa Duniani yanayofikia kilele chake kila mwaka tarehe 11 Februari ni mwaliko wa kuonesha mshikamano wa upendo na wagonjwa pamoja na wahudumu wa sekta ya afya, ili waweze kusimama kidete kulinda na kutetea maisha, utu na heshima ya kila mgonjwa wanayemhudumia. RealAudioMP3

Katika taabu na mahangaiko ya afya ya roho na mwili, kuna haja kwa waamini kulikumbuka Fumbo la Msalaba, kielelezo makini cha: upendo, huruma na msamaha kwa binadamu. Ni mwaliko kwa waamini kushiriki katika mateso ya Kristo kama sehemu ya mwendelezo wa mchakato wa kazi ya ukombozi iliyoanzishwa na Kristo mwenyewe. Wawe tayari kupokea Misalaba ya maisha yao kwa imani, matumaini na mapendo makuu.

Anamshukuru Mungu kwa wema na ukarimu wake. Kama Padre na Askofu ameonja pia mateso, magumu na mahangaiko ya ndani katika maisha na utume wake. Jambo la msingi ni kumkabidhi mateso na mahangaiko yote haya Kristo ili kupata nguvu na ari mpya zaidi. Waamini wajifunze maana ya mateso yanayookoa na kuyapokea yote kwa moyo wa uvumilivu na subira; changamoto kubwa zaidi ni kuungana kabisa na Yesu Kristo kwa kuyamimina yote mbele yake!







All the contents on this site are copyrighted ©.