Imani na matumaini ni nguzo muhimu katika kuitikia wito wa Kristo!
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, wakati wa Sala ya Malaika wa Bwana, Jumapili
iliyopita alitafakari kuhusu Liturujia ya Neno la Mungu, Jumapili ya tano ya Kipindi
cha Mwaka wa Kanisa, kwa kuangalia wito wa mitume wa kwanza wa Kristo, baada ya kuwafundisha
watu waliokuwa wamemiminika kumsikiliza anamwambia Petro kushusha nyavu zake tena
baada ya kuvua usiku kucha bila mafanikio. Simoni anatii na kushusha nyavu zake na
hivyo kufanikiwa kupata wingi wa samaki.
Mwinjili Luka anaonesha imani na matumaini
ya Mitume wa kwanza wa Yesu, kwa kuacha yote na kumfuasa, kwa kumtambua kuwa ni Bwana
na Mwalimu. Baba Mtakatifu anasema, wito wa Mungu kwa waja wake hauangalii sana ubora
wa mtu bali imani yake, kama anavyodhihirisha Simoni kwa kusema, "Bwana kwa neno lako
nitazishusha nyavu zangu".
Baba Mtakatifu anasema, Wainjili wanaelezea matukio
makuu mawili ambayo yanawahusisha mitume katika shughuli yao ya uvuvi: kabla ya mateso
ya Kristo na baada ya ufufuko wake, kielelezo makini cha utume wa Kanisa kwa sasa
na baada ya ufufuko wa wafu. Kwa sasa linakusanya wema na wabaya, lakini baada ya
ufufuko Kanisa litakuwa ni kwa ajili ya watu wema tu! Ndivyo anabyobainisha Mtakatifu
Augostino, Askofu na Mwalim wa Kanisa.
Mtakatifu Petro ni kielelezo cha wafuasi
wa Kristo ambao kamwe hawapaswi kukata tamaa kumtangaza Kristo kwa watu wote hadi
miisho ya dunia. Liturujia ya Neno la Mungu kwa Jumapili hii ni mwaliko wa kutafakari
wito wa kipadre na kitawa, kazi ya Mungu! Binadamu si chanzo cha wito wake mwenyewe,
bali anajibu changamoto hii kutoka kwa Mwenyezi Mungu na kamwe mapungufu ya binadamu
yasiwe ni kikwazo pale Mwenyezi Mungu anapomwita mtu. Jambo la msingi ni kuwa na imani
na nguvu kutoka kwa Mwenyezi Mungu mwingi wa huruma anayebadili na kufanya mtu kuwa
mpya zaidi.
Baba Mtakatifu anawaalika waamini kujiaminisha katika Neno la Mungu
ili kama watu binafsi na Jumuiya za Kikristo wawe na ujasiri na imani ya kutangaza
na kushuhudia Injili hadi miisho ya dunia. Vikwazo na magumu kamwe yasiwakatishe tamaa,
bali wasonge mbele kwa imani na matumaini kwa kutekeleza wajibu wao na Kristo atakamilisha
yale yanayosalia. Anawataka waamini kujiaminisha kwa Bikira Maria, Malkia wa mitume,
aliyefahamu unyonge wake, lakini akatoa jibu la uhakika linaloonesha kujitoa kwake
bila ya kujibakiza. Bikira Maria awasaidie waamini kuendelea kujitoa kikamilifu ili
kumfuasa Kristo Bwana na Mwalim.