Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya Tano ya Kipindi cha Mwaka C wa Kanisa
Tunakuleteeni kipindi Tafakari Neno la Mungu, tayari tukiwa Dominika ya tano ya mwaka
C. Mama Kanisa ametuwekea Neno akitukumbusha wito wetu na wajibu wetu wa kutanganza
Neno la wokovu kwa mataifa, ili wapate kuokolewa.
Hata hivyo
twadaiwa sisi wenyewe kutakaswa na kukiri ukuu wa Bwana kwa ajili ya wajibu huo. Nabii
Isaya katika somo la kwanza yuko katika ndoto na anamwona Bwana ambaye ameketi katika
kiti cha enzi kilicho juu sana.
Bwana huyu aliye katika kiti cha enzi amezungukwa
na Maserafi ambao wanamwimbia wimbo maarufu wakisema “mtakatifu, mtakatifu, mtakatifu”.
Katika hili Nabii Isaya anaona utukufu wa Mungu ukingaa mbele yake na kwa unyenyekevu
anakiri udhaifu na dhambi zake mbele ya Mungu. Kwa hakika ndivyo inavyopaswa kuwa
mbele ya fumbo kuu. Mwaliko kwako mpendwa unayenisikiliza ni kuingia katika maono
ya nabii Isaya na kuaanza kutafakari ukuu wa Mungu, kuguswa na hatimaye kuanza safari
ya kutumwa kwa ajili ya mataifa, umisionari wetu.
Nabii Isaya anapoona utakatifu
wa Bwana anaogopa, hata hivyo haogopi na kukimbia bali anabaki ili aweze kuonja uzuri
wa ukuu huo. Namna ya kuonja ukuu wa Bwana ni kukiri kwa unyenyekevu mkubwa kutositahili
kwake kuona mambo makuu hayo, anasema “ole wangu mimi mwenye midomo michafu na ambaye
hukaa katika watu wachafu” Anakiri pia udhaifu kwa ajili ya wengine.
Kama
Mwana wa Mungu alivyojinyenyekeza mno na Baba yake akamkirimia jina lipitalo kila
jina, vivyohivyo katika mastahili ya Mwana wa Mungu Nabii Isaya katika upole wake
anakirimiwa zawadi ya ondoleo la dhambi. Zawadi hii inatolewa pale mmoja wa maserafi
anapomgusa kinywa chake kwa kaa la moto na kumwambia umeondolewa dhambi zako. Kisha
zawadi ya ondoleo la dhambi anatumwa kwa ajili ya kutangaza Neno la Mungu kwa jumuiya
yake.
Mpendwa hivi leo kaa la moto hutujia kwa njia ya sakramenti ya ubatizo,
Ekaristi Takatifu, Kipaimara, kitubio nk. na mara mwaliko wa kutumwa hufuata, maana
tukishapokea neema za Bwana tuna nguvu kwa ajili ya kuhubiri Habari njema. Wapendwa
kwa ubatizo tumetakaswa kwa ajili ya wajibu wa kuokoka sisi wenyewe lakini pia kwa
ajili ya wengine, basi ni kazi kwako kuyaweka mausia ya Bwana yakujiayo kwa njia ya
Neno lake kila siku katika mwendo wa kimisionari.
Katika somo la II Mtakatifu
Paulo akiwaandikia Wakorintho anataka kuwahakikishia ile imani waliyonayo ina msingi
katika Ufufuko wa Bwana ambayo imewafikia kwa njia ya Mitume. Anasema Bwana alikufa
kwa ajili ya dhambi na akafufuka na kuwatokea Mitume, kwanza Mtakatifu Petro na kisha
wengine. Mwishoni alinitokea mimi ambaye sikustahili kutokewa na Bwana kwa sababu
naliliudhi Kanisa, lakini kwa Neema ya Mungu nimekuwa hivi nilivyo”. Mtume Paulo anasema
kwa neema ya Mungu niliyoipokea nimefanya kazi nzito hata kuwapita wengine, lakini
sijivuni bali ni neema ya Mungu pamoja nami. Wakorintho wanaitwa sasa kuishika imani,
kwa maana katika kuishika ndiko kuna wokovu wa milele.
Katika Injili, Luka
tunapata kusikia juu ya wito wa Mitume. Bwana yuko kando ya ziwa Genezareti, pale
kuna vyombo viwili na Bwana anaingia chombo kimojawapo na kumtaka Mt. Petro akipeleke
mbali kidogo na pwani. Jambo la kwanza hapa tunaloliona ni uteuzi wa Mt Petro kuwa
kiongozi mkuu. Bwana akiwa katika chombo kile anawafundisha watu na akishakumaliza
mafundisho yake anamwambia Petro tweka mpaka kilindini! Mt. Petro anasita kwa sababu
hawakupata samaki usiku kucha, lakini anaamini na kukiri akisema kwa neno lako nitazishusha
nyavu. Matokeo ya kuaamini kwake wanapata samaki wengi. Wafanye nini sasa kwa wingi
huu? Wakawaita washirika wao. Hapa twajifunza kuwa jambo jema ambalo ni wokovu ni
kwa ajili ya wote.
Mpendwa msikilizaji, mambo yote haya, kwa Mt Petro ni mambo
ya ajabu na hivi anaanguka kifudifudi mbele ya Bwana, alama ya ungamo la dhambi kama
alivyofanya Nabii Isaya katika somo la I na kisha anakubali na kusadiki ukuu wa Yesu
Kristu ya kuwa ni Mwana wa Mungu. Kinachofuata daima kama Nabii Isaya alivyofanyiwa
ni kutumwa, sasa utavua watu badala ya samaki! Mara moja pasipo kuchelewa wanaacha
nyavu zao na kumfuata Bwana.
Katika injili hii ya leo twaweza kujifunza kama
nilivyokwisha sema, yafuatayo yaani wajibu wa kuwasaidia watu wote ili waokoke uko
katika ubatizo wetu na sakramenti nyingine zinazotupatia baraka kwa ajili ya utume.
Bwana hafundishi akiwa pwani bali yuko ziwani na hivi mwinjili ataka kutuambia kuwa
sasa baada ya kusikia Neno la Mungu Jumapili lazima kwenda kwenye maisha ya kawaida
na kutangaza ujumbe huo, ndiyo kusema katika Jumuiya Ndogondogo za Kikristo.
Katika
chombo kuna watu wa aina zote wadhambi na wema kumbe wokovu si kwa wema tu bali wadhambi,
cha msingi ni kuungama kama Mt. Petro alivyofanya mbela ya Bwana. Mt. Petro ndiye
anayepeleka chombo ziwani, hapa polepole Bwana anatangaza ukuu wa Mt. Petro katika
Kanisa akikabidhiwa kuongoza na kuchunga taifa la Mungu, akiwa mfano hai wa kukiri
imani mbele ya Bwana. Tena Mtakatifu Petro hapeleki chombo kadri anavyotaka bali atakavyo
Bwana, kumbe Kanisa analoliongoza Baba Mtakatifu ni Kanisa la Bwana, na hivi atafanya
anachotaka Bwana, yaani kusikiliza na kufuata mapenzi ya Mungu.
Kumbe wito
kwako unayenisikiliza ni kuitikia wito wa Mungu kwa imani na kukubali kuongozwa na
Bwana siku zote na si vionjo vyako wala vya mwingine! Jumuiya Ndogondogo ni chombo
cha Bwana na si chaguo ambalo ni kwa ajili ya mtu fulani, kumbe tutekeleze wito huo
ulio wa tija kwa wokovu wetu.
Ni vema, ndugu yangu mpendwa ukumbuke tunapovua
samaki baada ya muda samaki hawa hufa, kumbe ndiyo maana leo Bwana anatualika kuvua
watu ambao wakishondolewa katika giza la dhambi huishi milele. Kazi kubwa ni kuondokana
na visasi kati yetu sisi wenyewe na kuwasaidia wengine waondokane na vita, wivu, uongo,
uvunjifu wa amani kwa sababu ya imani na sadiki tofauti, uhalibifu wa maisha adilifu
katika familia na waweze kuishi kwa amani.
Nikutakie furaha na amani katika
kipindi hiki na hasa tunapojiandaa hapo tarehe 13Februari kuanza kipindi cha Kwaresima.
Iwe ni fursa ya kusali, kutafakari Neno la Mungu, kushiriki kikamilifu katika Sakramenti
za Kanisa pamoja na kumwilisha Imani katika matendo ya huruma kwa maskini na wote
wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Tumsifu Yesu Kristo.
Tafakari hii imeletwa
kwako na Padre Richard Tiganya, C.PP.S.