2013-02-06 07:42:39

Mikakati ya Caritas Rwanda katika huduma za upendo na mshikamano kwa Mwaka 2013


Shirika la Misaada la Kanisa Katoliki nchini Rwanda, Caritas, limehitimisha mkutano wake wa mwaka kwa kutoa mapendekezo yanayopaswa kufanyiwa kazi na vitengo vyake vikuu vinne yaani: Utawala, Afya, Maendeleo na Huduma za Kijamii. Utekelezaji huu unalihusisha pia Baraza la Maaskofu Katoliki Rwanda kwa kuliomba lijihusishe zaidi na zaidi katika huduma kwa wafungwa magerezani.

Tume ya haki, amani, familia, vijana na elimu imeombwa pia kuwa karibu zaidi na Caritas, ili kwa pamoja waweze kutoa huduma bora na makini zaidi kwa Familia ya Mungu nchini Rwanda. Katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, Caritas Rwanda inatarajia kuchapisha ujumbe maalum kwa ajili ya waamini, kama sehemu ya mchakato wa kuendeleza huduma kwa wafungwa magerezani; wakimbizi na wahamiaji ambao bado wako kwenye kambi za wakimbizi nchini humo.

Caritas katika Majimbo mbali mbali nchini Rwanda inahamasishwa kujenga vituo maalum vitakavyosaidia kutoa elimu ya ufundi na majiundo makini kwa watoto na vijana. Ili kuhamasisha uelewa makini wa huduma zinazotolewa na Caritas, kuna haja ya kuanzisha Siku ya Caritas Kiparokia. Taasisi inayoratibu huduma za afya zinazotolewa na Kanisa Katoliki nchini Rwanda, imewapongeza wajumbe wa Caritas Rwanda kwa mchango na huduma wanayotoa kwa wananchi wa Rwanda. Caritas Rwanda imealikwa pia kushiriki katika mkutano mkuu wa Taasisi hii utakaofanyika tarehe 14 Machi 2013.








All the contents on this site are copyrighted ©.