2013-02-05 08:11:14

Hali ya amani na usalama inaanza kurejea kidogo nchini Mali, lakini bado kuna dharura zinazopaswa kufanyiwa kazi!


Baraza la Maaskofu Katoliki Mali linasema kwamba, hali ya usalama nchini humo inaendelea kuwa shwari kidogo, lakini kwa sasa tatizo ni huduma kwa watu wasiokuwa na makazi, waliolazimika kuyakimbia makazi yao ili kusalimisha maisha yao kutoka Kaskazini mwa nchi ambako Vikosi vya ulinzi na usalama vya Ufaransa vinapambana na majeshi ya waasi nchini Mali.

Rais Francois Hollande hivi karibuni ametembelea mji wa Timbuktu na kupokelewa na maelfu ya wananchi wa Mali waliokuwa wanamshangilia kutokana na uamuzi wa nchi yake kusaidia harakati za kupambana na vikosi vya waasi vilivyokuwa vinatishia amani na usalama Kaskazini mwa Afrika, kutokana na kujihusisha pia na vitendo vya kigaidi.

Licha ya mafanikio yaliyokwisha kupatikana, lakini bado Mali inakabiliwa na hali ngumu ya maisha, kwani bado wananchi wengi wanahofia usalama wa maisha yao na kwamba, gharama ya maisha imepanda sana, ikilinganishwa na hali ya maisha ya wananchi wa Mali. Bado watu wanahitaji huduma ya afya, malazi, chakula na maji safi na salama.

Kutokana na changamoto hii, Askofu Georges Fonghoro wa Jimbo la Mopti, amewaomba Wasamaria wema, kuchangia kwa hali na mali ili kuokoa maisha ya wananchi wanaoendelea kuteseka kutokana na mgogoro wa kivita nchini humo. Wananchi wengi hawana makazi na wanaoteseka zaidi ni wanawake na watoto. Bado wananchi wanaona wasi wasi wa kurudi katika maeneo yao ili kuendelea na maisha kama kawaida!







All the contents on this site are copyrighted ©.