2013-02-04 08:18:18

Juhudi za Kanisa katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa Ukimwi katika Kipindi cha Miaka 30 iliyopita!


Miaka 30 imekwishagota, tangu wataalam walipogundua Virusi vya Ugonjwa wa Ukimwi duniani, janga ambalo limepelekea watu wengi hususan vijana ambao ni nguvu kazi ya mataifa mengi kujikuta wakipoteza maisha wangali vijana wabichi. Katika harakati hizi, Kanisa Katoliki limekuwa mstari wa mbele si tu kwa kutoa faraja kwa waathirika wa Ukimwi bali pia kutoa dawa za kurefusha maisha pamoja na ushauri nasaha unaogusa maisha ya mtu mzima: kiroho na kimwili.

Hivi karibuni, Shirika la Wayesuit linalojishughulisha na Mapambano dhidi ya Ugonjwa wa UKIMWI, AJAN kwa kushirikiana na Shirika la Mabinti wa Mtakatifu Paulo, wamechapisha Kitabu kuhusu UKIMWI; kwa kujikita katika tafakari za kiimani juu ya janga la Ukimwi Barani Afrika. Kitabu hiki ni jitihada za makusudi katika mchakato wa mapambano dhidi ya ugonjwa wa Ukimwi Barani Afrika.

Kitabu hiki kinawahusisha wasomi, wadau na wanaharakati katika mapambano dhidi ya baa la ugonjwa wa Ukimwi. Kinauangalia ugonjwa huu katika medani mbali mbali za maisha, daima utu na heshima ya binadamu ikipewa kipaumbele cha kwanza. Utangulizi umeandikwa na Kardinali John Onaiyekan, Askofu mkuu wa jimbo kuu la Abuja, Nigeria, anayepongeza juhudi na kazi kubwa iliyofanywa na waandishi wa kitabu hiki katika kuufahamu ukweli wa ugonjwa wa Ukimwi Barani Afrika na mchango unaotolewa na Kanisa Katoliki katika mapambano haya.

Kardinali Onaiyekan anasema, hiki ni kitabu ambacho kinagusa mahusiano msingi ya kijamii na kiuchumi; utamaduni, haki msingi za binadamu; maadili na utu wema. Kanisa linashiriki kikamilifu katika mapambano haya kwa kutoa nadharia pamoja na utekelezaji wake katika uhalisia wa maisha ya watu, kwani itakumbukwa kwamba, Kanisa Katoliki ni kati ya wadau wakubwa wanaowahudumiwa waathirika wa ugonjwa wa Ukimwi sehemu mbali mbali Barani Afrika. Changamoto kubwa iliyoko mbele ya Jumuiya ya Kimataifa anasema Kardinali Onaiyekani ni elimu makini itakayosaidia mchakato wa mapambano dhidi ya maambukizi mapya ya virusi vya Ukimwi.

Elimu hii inapaswa kujikita kwa namna ya pekee katika haki msingi za binadamu, maadili na utu wema bila kusahau kubainisha mikakati ya shughuli za kichungaji kwa ajili ya kuwasaidia waathirika wa ugonjwa wa Ukimwi. Ni matumaini ya Kanisa kwamba, baada ya kifo kuna maisha ya uzima wa milele, Kardinali John Onaiyekani, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Abuja anasema kwamba, mapambano dhidi ya ugonjwa wa Ukimwi, baado yanaendelea na kamwe watu wasibweteke, kwani wanaweza kukiona kile kilichomnyoa kanga manyoya!








All the contents on this site are copyrighted ©.