2013-02-02 19:26:35

Yaliyojiri kwenye maadhimisho ya Siku ya XVII ya Watawa Duniani kwa Mwaka 2013


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, katika maadhimisho ya Siku kuu ya Kutolewa Bwana Hekaluni, hapo Jumamosi, tarehe 2 Februari, 2013 ameadhimisha Ibada ya Misa Taikatifu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Ibada ambayo imepamba kwa uwepo wa umati mkubwa wa Mashirika ya Kitawa na Kazi za kitume.
Kwa mara ya kwanza, Siku ya Watawa Duniani, iliadhimishwa kunako mwaka 1997, kama sehemu ya mchakato unaopania kuhamasisha miito ya kitawa ndani ya Kanisa, kama cheche ya utakatifu wa maisha, changamoto na mwaliko kwa kila mwamini.
Siku hii inapania pamoja na mambo mengine, kumshukuru Mungu kwa ushuhuda wa maisha na huduma inayotolewa na Watawa sehemu mbali mbali za dunia, kwa kuishi Mashauri ya Kiinjili, yaani: Utii, Ufukara na Usafi wa Moyo.
Mara ya mwisho kwa Baba Mtakatifu kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu na Watawa wa Mashirika mbali mbali, ilikuwa ni mwaka 2006. Mara nyingine zote, Baba Mtakatifu amekuwa akiadhimisha Siku kuu hii kwa njia ya Masifu ya Jioni. Ibada ya Misa Takatifu kwa Mwaka 2013 imeanza kwa maandamano ya Watawa 50 kutoka Mashirika mbali mbali ya Kitawa na Kazi za Kitume, kielelezo cha karama mbali mbali zinazojionesha ndani ya Kanisa kama zawadi ya Roho Mtakatifu.
Katika Maandamano haya, Wakuu mbali mbali wa Mashirika wameshiriki pia, huku wakiwa wamebeba mikononi mwao mishumaa inayowaka, kielelezo cha Kristo Mwanga wa Mataifa na changamoto kwa Watawa wenyewe kuwa kweli ni mwanga kati ya watu wanaowahudumia. Kwa njia ya ushuhuda wao makini, watawa pia wanaweza kuendeleza mwanga wa Kristo unaookoa walimwengu.








All the contents on this site are copyrighted ©.