2013-02-02 16:05:27

Kanisa Katoliki litaendelea kuwekeza katika Katekesi na Elimu ya dini shuleni ili kujenga taifa la watu wenye nidhamu, maadili na utu wema!


Askofu Evaristo Chengula wa Jimbo Katoliki Mbeya, Tanzania, ametoa ufafanuzi wa tamko la Jukwaa la Wakristo kuhusu suala la kuchoka kutukanwa na kuonewa siyo dhana ya kulipiza kisasi bali ni kuwa watu wa sala na kitubio na ikiwezekana kukaa na kuzungumza na wanaojenga chuki na kufanya uharibifu wa mali ya watu na serikali.

Askofu Chengula ametoa ufafanuzi huo katika semina ya Makatekista na Walimu wa dini iliyofanyika katika ukumbi wa vijana jijini hapa ambao walitaka kujuwa ukimya huo utadumu hadi lini hali wanachokozwa, wanatishiwa maisha na vitu kuharibiwa.

Amesema amesema licha ya kanisa kutukanwa,kuchokozwa na kuharibiwa na hata kufikia ya kuanza kupigwa risasi halitajibu zaidi ya kuendelea kusali rozali takatifu,kufanya kitubio na kuendelea kufunga ili kushinda majaribu hayo yasiyompendeza mwenyezi mungu."Kanisa Katoliki limetukanwa sana, limefanyiwa uchokozi na uharibifu mkubwa na sasa wameanza kutupiga na bunduki, huku vikitolewa vitisho vya kuuawa Mapadre na Maaskofu wazi wazi, lakini tunaposema limechoka kutukanwa msibebe bunduki bali muwe watu wa sala na kuwaombea wanaofanya hayo ili watubu na kumrudia Mwenyezi Mungu,"alisema.

Aliongeza"muwe watu wa sala, mapatano na wakakamavu, tusali Rozali katika nyumba zetu, tufanye kitubio na tuwe watu wa kufunga na tumshinde shetani hiyo ndiyo silaha pekee na ikibidi kutokana na kuchoka huku tuwe tayari kuzungumza na hao wanaotuchokoza, tujimwagie majivu na kusali." Aidha Askofu Chengula ametoa ushauri kwa Serikali na Mamlaka husika kutoruhusu kujengwa nyumba za starehe karibu na vyuo ama shule kwani ndiyo chanzo kikubwa cha ongezeko la vitendo vya kikatili vya utoaji wa mimba na kuuwa watoto wanaokotwa katika madampo ya taka katika vyuo na mashule.

Amesema haiwezekani kuchanganya elimu na starehe kwani kitendo cvha kujenga nyumba za starehe jirani na vyuo kunamjengea mazingira magumu ya ushawishi mwanafunzi na ndiyo matokeo ya kushindwa kuendelea kimasomo ama mwendelezo wa kuokotwa watoto katika madampo. "Pale Iringa katika chuo kikuu cha Rouco wamefaulu kwani kuna muda walitaka kujenga majengo ya aina hiyo lakini Mungu alisikia vilio vya watu wake na sasa pako salama na Mbeya ili vitendo vipunguwe na kumalizika na watoto waweze kusoma kwa usalama hayo maeneo yaondolewe," amesema.

Hata hivyo amewaagiza Mapadre, Watawa wa Kike na Kiume, Makatekista na Walimu wa dini kuongeza jitihada za dhati kuwatembelea mara kwa mara wanafunzi na wanachuo kuwapatia ushauri licha ya kuendeela kutoa mafundisho ya dini ili waweze kufuata maadili mema.

Katika semina hiyo mambo mbalimbali yamezungumzwa kuhusu muhtasari wa mafundisho ya dini kuanzia shule za awali hadi vyuo vikuu ambapo Katibu Mtendaji wa Idara ya Katekesi kutoka Baraza la Maaskofu Tanzania Padri Raphael Madinda alitoa mada kuhusu umuhimu na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi kuridhia kuingizwa katika mtaala wa elimu nchini. Padri Madinda alisema mmong’onyoko wa maadili na kuibuka kwa vurugu, migomo na migogoro mbalimbali hata kusababisha maandamano mashuleni chanzo kikubwa ni ukosefu wa mafundisho ya dini ambayo yanamjenga mwanafunzi kumuogopa Mungu na kuishi kwa kufuata: sheria za nchi, maadili na utu wema.

Ametoa wito kwa waamini wa Kanisa Katoliki kujitokeza kwa wingi kutoa mafundisho ya dini kwa wanafunzi kuanzia ngazi ya awali, msingi, sekondari,v yuo na vyuo vikuu ili jamii iweze kurejea katika maisha ya upendo, amani, tulivu, upatanisho, haki na kuvumiliana; mambo ambayo yanaendelea kuporomoka kwa kasi ya ajabu nchini Tanzania.

Katika Semina hiyo Padri Innocent Sanga amesema changamoto kubwa wanayokabiliana ni ukata katika kuwawezesha walimu na makatekista kufundisha katika shule mbalimbali kwani Jiografia ya maeneo ya Mkoa wa Mbeya ina milima na mabonde na shule kujengwa umbali mrefu unaohitaji vyombo vya usafiri sanjari na fedha za kujikimu jambo ambalo wanaendelea kulitafutia ufumbuzi wakati wakiendelea kujitoa.

"Kwa kweli walimu na makatekista wanatoa huduma za kufundisha mashuleni katika mazingira magumu,kuna maeneo yana umbali mrefu lakini wanajituma kutembea,tunawapongeza sana lakini pia tunawashukuru mapadri na masista kwa kuendelea kuonyesha mfano kwa kuendelea kufundisha,"amesema.

Hata hivyo Askofu Chengula wakati akigawa vitabu vya muhtasari wa Mafundisho ya dini mashuleni amewapongeza Mapadri kwa kuendelea kutoa mafundisho ya dini kwani hilo ndilo jukumu kubwa la Kanisa kufundisha Katekesimu, Neno la Mungu, Maisha ya Kisakramenti sanjari na huduma nyingine za kiroho na kimwili.









All the contents on this site are copyrighted ©.