2013-01-31 08:46:24

Umaskini Duniani na changamoto zake!


Kuna zaidi ya watu billioni moja duniani wanaokabiliana na umaskini mkubwa. Dhana ya umaskini imekuwa ni sehemu ya maisha ya mwanadamu, lakini wakati mwingine umaskini huu unasababishwa na binadamu mwenyewe kwa kuendekeza sera na uchumi unaotoa mwanya kwa matajiri kuendelea kutajirika zaidi na maskini, akina yakhe pangu pakavu tia mchuzi kuendelea kuogelea katika lindi la umaskini na utupu! Huu ndio ukweli utakaoendelea kumwandama mwanadamu katika hija ya maisha yake hapa duniani. RealAudioMP3

Ni maneno ya Kardinali Robert Sarah, Rais wa Baraza la Kipapa linaloratibu Misaada ya Kanisa Katoliki Cor Unum katika mahojiano na Radio Vatican kuhusiana na baa la umaskini duniani, kampeni ambayo inaendeshwa kwa namna ya pekee na Shirikisho la Radio na Televisheni Barani Ulaya.

Lakini umaskini pia unaweza kuangaliwa kwa jicho chanya, kwani ni kielelezo cha mtu kuishi kwa kiasi, wakiwa na tabasamu na furaha ya kweli, badala ya kuwa na mali nyingi lakini daima watu wanalala macho wazi kama bundi kwa hofu na magonjwa yanayotokana na kuwa na mali nyingi kupita kiasi. Watu maskini wana imani kubwa katika maisha; binadamu anapaswa kupata mahitaji yake msingi yanayozingatia utu na heshima yake kama binadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.

Kardinali Sarah anabainisha kwamba, hata katika Agano la Kale, utajiri ulionesha baraka na neema kutoka kwa Mungu. Kristo katika utume wake anabainisha kwamba, amekuja kuwatangazia maskini Habari Njema ya Wokovu na kwamba, Heri Maskini maana Ufalme wa Mungu ni wao. Kristo Mwana wa Mungu, amejifanya kuwa maskini, kiasi hata cha kuchukua ubinadamu na kufanana na mwanadamu katika mambo yote isipokuwa hakutenda dhambi.

Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican wanaliasa Kanisa kuonesha ile sura ya umaskini. Huu ni mwelekeo chanya kuhusu dhana ya umaskini ndani ya Kanisa, ambao kwa maneno mengine unafahamika kama Nadhiri ya Ufukara, yaani kuwa na matumizi sahihi ya mali na utajiri wa ulimwengu huu, kama wanavyofanya Watawa katika Mashirika yao! Ni matajiri wa vitu, lakini wakarimu kwa njia ya mali waliyonayo kwa ajili ya maisha na utume wa Kanisa. Lakini Jumuiya ya Kimataifa haina budi kujifunga kibwebwe anasema Kardinali Robert Sarah ili kupambana na umaskini unaodhalilisha ut una heshima ya mwanadamu.

Huu ndiyo utume na dhamana ambayo Mama Kanisa ameendelea kuitekeleza katika hija ya maisha yake hapa duniani kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa ut una heshima ya mwanadamu, aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Kanisa limeendelea kuwekeza katika huduma ya afya kwa kuendeleza ile kazi ya Kristo Msamaria mwema, aliyemganga mwanadamu kwa kumondolea magonjwa yake pamoja na dhambi zilizokuwa zinamsumbua moyoni mwake. Kanisa limeanzisha shule katika ngazi mbali mbali ili kumkomboa mwanadamu kutoka katika lindi la ujinga na kumwezesha ili kupambana fika na hatimaye, kuweza kuboresha mazingira yake, ili dunia iweze kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi.

Kanisa linaendelea kuunga mkono juhudi za wakulima, ili waweze kujinasua na baa la njaa na umaskini wa kipato, kwa njia ya kilimo bora na kilimo kinachozingatia utunzaji bora wa mazingira pamoja na matumizi sahihi ya pembejeo na teknolojia rafiki kwa mazingira, kama sehemu ya mwendelezo wa mchakato wa utunzaji wa kazi ya uumbaji. Kanisa kwa huduma mbali mbali limeendelea kutoa fursa za kazi na ajira ili kuboresha maisha ya watu kwa kutambua kwamba, kazi ni utimilifu wa utu na heshima ya mwanadamu. Mama Kanisa anasema Kardinali Robert Sarah anapenda kumhudumia mtu mzima: kiroho na kimwili.

Kanisa linaendelea kuonesha mshikamano wa upendo kwa watu wanaoteseka kutokana na maafa asilia, vita, kinzani na migogoro ya kisiasa na kijamii kama inavyojionesha huko Mashariki ya Kati na sehemu mbali mbali za dunia. Kanisa limekuwa ni alama ya matumaini na kimbilio la wengi katika mapambano dhidi ya umaskini, ujinga na maradhi, hasa sehemu za vijijini. Kanisa linapenda kumfariji mtu katika mahangaiko yake kimwili na kiroho, ili aweze kutambua kwamba, anapendwa na anathamani kubwa mbele ya Mwenyezi Mungu.

Kumbe, kuna haja kwa kila mtu katika hali yake kuhakikisha kwamba, anatunza na kudumisha misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano. Binadamu ajifunze kutunza mazingira; kuzingatia kanuni maadili kuhusu uchumi na fedha kwani myumbo wa uchumi kimataifa unaoendelea kuwatumbukiza watu wengi katika umaskini wa kipato ni matokeo ya kutozingatia kanuni maadili katika mfumo wa fedha. Mungu na mwanadamu wapewe kipaumbele cha kwanza katika mipango na sera za maendeleo endelevu.








All the contents on this site are copyrighted ©.