Ukata na athari za mafuriko zinavyo vuruga huduma za Kijamii nchini Malawi
Mheshimiwa Padre Piergiorgio Gamba ambaye kwa miaka mingi amekuwa mstari wa mbele
katika mapambano na huduma kwa wagonjwa wa Ukimwi nchini Malawi anasema kwamba, fedha
za kununulia dawa za kurefusha maisha kwa wagonjwa wa Ukimwi nchini Malawi zimepunguzwa
kwa kiasi kikubwa kiasi kwamba, wagonjwa wengi wameanza kukata tama na kwamba, juhudi
zilizokuwa zinafanywa na Mashirika haya pengine sasa zikagonga mwamba na idadi ya
waathirika wa ugonjwa wa Ukimwi wakaongezeka.
Hali hii inatishia amani kwani
wagonjwa wengi waliokuwa wanatumia dawa za kurefusha maisha, wanaweza kufariki dunia,
kwani wengi wao wanakabiliwa na ukata ambao kwa sasa unachangiwa pia na athari za
mafuriko yaliyoikumba Malawi kwa siku za hivi karibuni. Kama hali hii haitapatiwa
ufumbuzi wa kudumu, wastani wa umri wa wananchi wa Malawi kuishi utaweza kushuka chini
ya miaka arobaini. Kwa sasa watu wengi hawana makazi maalum baada ya makazi yao kusombwa
na mafuriko.
Ukata pia unalikumba Kanisa ambalo linawezeshwa na waamini ambao
kwa sasa wanakabiliwa na hali ngumu ya uchumi, kiasi kwamba, huduma katika shughuli
za kichungaji, elimu na afya zimeanza kuathirika kwa sasa. Umaskini ni kati ya changamoto
zinazofanyiwa kazi na Baraza la Maaskofu Katoliki Malawi, lililoanza mkutano wake
hapo tarehe 28 Januari na unatarajiwa kuhitimishwa hapo tarehe Mosi Februari 2013.
Maaskofu pia wanajadili namna ya kutekeleza Maazimio ya Maadhimisho ya Awamu
ya Pili ya Sinodi ya Maaskofu wa Afrika, Mwaka wa Imani pamoja na maandalizi ya Mkutano
mkuu wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika Mashariki na Kati, AMECEA,
unaotarajiwa kufanyika nchini Malawi, hapo mwaka 2014.