Wakristo wajitambue vema na kuonesha ushujaa katika kuihubiri Injili ya Kristo
Kila mmoja katika kuongoka kwake, kujifahamu na kuishi kadiri ya alivyoumbwa na kuitwa
ni zoezi la kiroho na hatua kubwa katika kumfuasa Kristo. Hayo yamesemwa na Askofu
Mkuu Yuda Thaddei Ruwa’ichi wa Jimbo Kuu la Mwanza, Tanzania, katika Adhimisho la
Misa Takatifu ya Sikukuu ya kuongoka kwa Paulo Mtume. Katika adhimisho hilo lililofanyika
katika Seminari Ndogo ya Mt. Maria, Nyegezi, aliwapatia pia Majandokasisi wawili daraja
ya Ushemasi ambao ni: Theophilus Kumalija wa Parokia ya Mwabagole na Bernadin Mtula
wa Parokia ya Sumve. Askofu Mkuu Ruwai’cihi alioanisha maisha ya Mtume Paulo na
Wakristo katika zama hizi ili waweze kuiga mfano wa mtume huyo. Mtume Paulo kadiri
ya mapokeo, alikuwa mfupi wa kimo na mwenye umbo dogo. Hakuwa mnyonge kwa sababu hizo,
bali alijikubali na kujisimamia kwa ujasiri bila kumangamanga. Naye alifundwa na kubobea
katika sheria, chini ya Mwalimu maarufu, Gamalieli. Paulo akawa mkereketwa wa imani
yake ya Kiyahudi na hivyo akawatesa hata kufa, Wakristo waliodhaniwa kupotosha imani
ya Kiyahudi. Ukereketwa na ujasiri huo ndio, Kristo anautumia na kumuongoa Paulo,
anamfanya mfuasi wake na mhubiri hodari wa Habari Njema. Pauolo alikuwa tayari kusimulia
habari za maisha yake ya awali ambayo kwa mwingine angeweza kujionea aibu na kuficha:
ya kwamba: alikuwa mtesi na muuaji wa Wakristo. Maneno magumu na mazito namna hii
yasiposimuliwa huelemea moyo na kumfanya mhusika kuwa na huzuni. Kumbe, ni vizuri
kushirikisha juu ya maisha binafsi na kuwa tayari kubadilika. Maisha ya awali hayapaswi
kuwa ni nukta katika maisha, hayapaswi kuwa mwisho bali ni hatua nyingine ya kubadilika
na kusonga mbele. Kauli kuu ni kujikubali, kupokea wongofu, kuitikia wito, kuwa kiumbe
kipya na kuishughulikia Habari Njema ya Wokovu. Mtume Paulo katika kukutana na
Kristo alidhihirisha sifa fulani nzuri za kujifunza toka kwake. Akitoa mifano ya baadhi
ya sifa hizo, Askofu Mkuu alifafanua: kutokuwa na kigugumizi, kutokusita katika suala
zima la imani na utendaji wa kila siku; kuwa na ari ya kumwamini na kumfuasa Kristo
kwa ujasiri hata ikibidi kutoa sadaka kubwa, Paulo alipata shida nyingi katika safari
zake kama mawimbi ya bahari, alipigwa mawe na kadhalika, lakini aliona fahari katika
Msalaba wa Kristo, na hivyo kushiriki mateso kwa imani. Askofu Mkuu alifafanua
kuwa ukristo unaoogopa mateso, ukristu unaopenda mambo rahisi rahisi ni upagani mamboleo;
Jambo muhimu ni kuhuburi Injili kwa uaminifu. Paulo aliliona jukumu la kuhubiri kuwa
ni Jukumu Takatifu, kwani alikuwa amekabadhiwa uwakili huo na kuwa mwaminifu, na kudiriki
kusema “Ole wangu nisipoihubiri Injili”; alikuwa thabiti katika ukweli, akitafuta
haki kwa nidhamu na heshima. Aliwaalika waamini wote wajisomee maisha ya mtume Paulo
katika kitabu cha Matendo ya Mitume na katika Nyaraka zake. Agizo la Kristo “Enendeni
ulimwenguni kote mkaihubiri Injili” bado ni agizo hai mpaka leo, alisema Askofu Mkuu
Ruwa’ichi. Ni wito ulio hai na makali yake mpaka leo na unahitaji uwajibikaji na utekelezaji
kutoka kwa kila mkristu. Kwa namna ya pekee, aliwaalika Mashemasi Theophilus Kumalija
na Bernardin Mtula kuizingatia sauti hiyo ya Kristo katika wito wao, waisikie kuwa
ni hai na inawadai. Askofu Mkuu Ruwa’ichi alielezea pia kuwa Jimbo kuu la Mwanza
limekuwa na utamaduni wa kutoa daraja ya Ushemasi katika Seminari hiyo Ndogo ya Nyegezi
ili kuhamasisha, kuwatia moyo na kukuza ari ya miito kwa wasemniari wadogo. Amewapongeza
wazazi wa mashemasi hao na kuwaalika waamini wote waendelee kuombea miito mitakatifu
ili Kristu azidi kuita vijana wengi anaopenda wamtukie kwa namna ya pekee. Shemasi
Theophilus Kumalija alizaliwa tarehe 07 Oktoba 1978 katika Kijiji cha Mwabagole Wilayani
Kwimba, Mwanza. Malezi na mafunzo ya wito Mtakatifu alipata katika Seminari kuu za
Kibosho, Moshi, kwa masomo ya Falsafa na Segerea, Dar es Salaam, kwa masomo ya Taalimungu
(2005-2012). Shemasi Bernardin Mtula alizaliwa 20 Mei 1981 katika kijiji cha Sumve
wilayani Kwimba, Mwanza. Mafunzo na malezi alipatia katika Seminari Kuu za Kibosho,
Moshi, kwa masomo ya Falsafa na Kipalapala, Tabora, kwa Taalimungu (2005-2012). Itakumbukwa
kuwa tarehe 08 Januari 2013 Jimbo kuu la Mwanza lilipata tunda la kwanza la Ushemasi
kwa mwaka huu, Peter Madata kutoka Parokia ya Kabila, Mwanza. Kwa mapenzi ya Mungu,
mashemasi hawa watapadirishwa mwaka huu kama ifuatavyo: Peter Madata 08 Agosti, Bernadini
Mtula 22 Agosti na Theophilus Kumalija 05 Septemba.