St. Thomas Aquinas, Nairobi yaadhimisha Jubilee ya miaka 50 tangu ilipoanzishwa
Seminari kuu ya Mtakatifu Tomas wa Akwino, iliyoko Jimbo kuu la Nairobi, Kenya, iliyoanzishwa
na Shirika la Wadominikani, kunako tarehe 25 Januari 1963, imeadhimisha Jubilee ya
Miaka 50 tangu ilipoanzishwa. Hadi sasa wanafunzi 1069 wamehitimu masomo katika taalimungu
na kati yao zaidi ya Mapadre 1,000 wanaendelea kutoa huduma za kichungaji ndani na
nje ya Kenya.
Askofu mkuu Zacchaeus Okoth, wa Jimbo kuu la Kisumu, Askofu mkuu
Peter Kairu wa Jimbo kuu la Nyeri na Askofu mkuu Boniface Lele wa Jimbo kuu la Mombasa
ni kati ya Maaskofu 8 waliobahatika kusoma Seminarini hapo.
Ibada ya Misa Takatifu
iliyohudhuriwa na umati mkubwa, iliongozwa na Kardinali John Njue, Rais wa Baraza
la Maaskofu Katoliki Kenya, kwa kushukuru waasisi wa Seminari hii ambayo imetoa mchango
mkubwa katika maisha na utume wa Kanisa nchini Kenya katika kipindi cha miaka 50 iliyopita.
Maadhimisho ya Jubilee hii yaliongozwa na kauli mbiu "Majiundo ya Kipadre katika Karne
ya 21".
Kardinali Njue amewataka wananchi wa Kenya kuendelea kujenga na kuimarisha
umoja na mshikamano wa kitaifa: kabla, wakati na baada ya uchaguzi mkuu unaotarajiwa
kufanyika nchini humo hapo tarehe 4 Machi 2013.
Kwa upande wake, Askofu mkuu
Okoth amewataka wanasiasa pia kujenga utamaduni wa huduma; haki na amani; wajikitahidi
kuponya madonda ya utengano ambayo yamekuwa ni kiwazo kikubwa katika kujenga na kuimarisha
umoja wa kitaifa kutokana na misigano ya kikabila na kijamii. Ili kujipatanisha na
jirani, kuna haja ya kusamehe na kusahau, kwani hii ni sehemu ya kweli za Kiinjili
zinazogusa undani wa mtu!
Seminari ya Mtakatifu Tomas wa Akwino imekuwa ni
kiwanda kikubwa cha majiundo ya Mapadre kwa Kanisa Katoliki nchini Kenya pamoja na
nchi wanachama wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Afrika Mashariki na Kati, AMECEA.
Kanisa nchini Kenya katika maadhimisho haya limewakumbuka na kuwaombea Wamissionari,
Mapadre na Watawa wote waliojitoa kimaso maso kutangaza Habari Njema ya Wokovu na
matunda yake yanaonekana kwa sasa.
Maadhimisho haya yamekwenda sanjari na
Kumbu kumbu ya Mtakatifu Tomas wa Akwino, inayoadhimishwa na Mama Kanisa kila mwaka
ifikapo tarehe 28 Januari.