Mpasuko wa kidini unaweza kuitumbukiza Tanzania katika janga la kitaifa!
Amani, utulivu na mshikamano wa kitaifa ambao watanzania wamejivunia kwa takribani
miaka 50 unaanza kuingiwa na dosari kubwa kutokana na kushamiri kwa vitendo vinavyoashiria
uvunjifu wa amani unaokumbatiwa na udini pamoja na misimamo mikali ya kiimani.
Kuna
mikakati ya makusudi kabisa inayofanywa ili kuweza kuitumbukiza Tanzania katika machafuko
ya kidini kwa kutumia mgongo wa kidini. Hayo yamesemwa hivi karibuni na Rais Jakaya
Kikwete wa Tanzania wakati akijibu hoja zilizoibuliwa katika taarifa ya tathmini ya
Mpango wa Afrika Kujitathmini kiutawala Bora, iliyowasilishwa mjini Addis Ababa, Ethiopia.
Kuna
changamoto kubwa kwamba, nchini Tanzania kumeaanza kuonekana mpasuko mkubwa wa kidini
hali inayotishia: utulivu, amani, mshikamano na maendeleo endelevu. Rais Kikwete ameonya
kwamba, Serikali yake haitakubali uchochezi wa vurugu za kidini na kwamba, Serikali
itawadhibiti.
Mambo mengine yaliyoibuliwa katika tathmini hiyo ni kuhusu uhuru
wa vyombo vya habari na haki msingi za binadamu, hasa mauaji ya watu wenye ulemavu
wa ngozi kutokana na imani za kishirikina na uroho wa utajiri wa haraka haraka.