2013-01-29 07:34:59

Maadhimisho ya Juma la Shule za Kanisa Katoliki Ireland


Baraza la Maaskofu Katoliki Ireland, limefungua rasmi maadhimisho ya Juma la Shule za Kanisa Katoliki nchini humo kwa kuwaalika wanafunzi, walimu, wazazi na walezi wanaounda Jumuiya ya Shule, kuendelea kuadhimisha utambulisho wao kama taasisi za Kanisa Katoliki, kwa njia ya maisha, masomo yanayotolewa pamoja na haki zote fungamanishi, tangu wakati kengele ya kwanza inapogonga hadi ile ya mwisho inapoashilia kumalizika kwa siku na hata wakati mwingine, nje ya kuta za shule.

Shule si majengo bali ni safari inayofumbata maisha ya watu mbali mbali. Hapa ni mahali ambapo wanafunzi wanajenga utamaduni wa urafiki wa kudumu, wanathamini elimu na maarifa waliyojipatia; ni kumbu kumbu endelevu ya uzoefu na mang’amuzi, fadhila na tunu mbali mbali zilizorutubishwa na kukuzwa hatua kwa hatua, ili hatimaye, ziweze kutoa mazao yanayokusudiwa.

Kanisa Katoliki linatambua dhamana ya kutoa elimu bora na makini, itakayomwandaa mwanafunzi katika maisha yake: kiroho na kimwili, ndiyo maana Kanisa linatoa kipaumbele cha pekee katika mikakati ya kichungaji kuhusiana na elimu, kwani huu ni wajibu shirikishi na utume ambao ni sehemu ya vinasaba vya Mama Kanisa, Shule zinazomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa Katoliki, ni Jumuiya za Imani na Yesu Kristo ndiye Kiongozi mkuu, anayewachangamotisha kuendeleza ujenzi wa Fumbo la Mwili wake yaani Kanisa.

Juma la shule za Kanisa Katoliki nchini Ireland kwa mwaka 2013 linaongozwa na kauli mbiu “shule ni Jumuiya za Imani; fursa ya kushirikishana Habari Njema”. Maadhimisho haya yanayokwenda sanjari na Mwaka wa Imani, iwe ni fursa kwa waamini kugundua ndani mwao ile furaha ya kuamini pamoja na kuendelea kujitahidi kuwa karibu zaidi na Kristo katika Maadhimisho ya Sakramenti za Kanisa, Tafakari ya Neno la Mungu na Matendo ya huruma, yanayoonesha ushuhuda unaong’ara ulimwenguni.








All the contents on this site are copyrighted ©.