2013-01-28 08:18:16

Mwaka wa Imani iwe ni fursa ya toba na wongofu wa ndani


Baraza la Maaskofu Katoliki Korea katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani uliotangazwa na kuzinduliwa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, linabainisha kwamba, Mwaka 2013 umetengwa maalum kwa ajili ya kuhamasisha shughuli za Uinjilishaji Mpya kwa ari na kasi kubwa zaidi, kwa kujitahidi kusoma alama za nyakati na kutumia njia mbali mbali za mawasiliano ili kuweza kufikisha ujumbe wa Injili kwa hadhira inayokusudiwa. RealAudioMP3
Waamini walei wanaalikwa kwa namna ya pekee, kushiriki katika maisha na utume wa Kanisa, wakitambua kwamba, wanayo dhamana ya kuyatakatifuza malimwengu, changamoto iliyotolewa na Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, yapata miaka hamsini iliyopita. Familia ya Mungu nchini Korea, itambue wajibu wake wa kumtangaza Kristo kwa njia ya ushuhuda wa maisha adili na matakatifu. Lengo ni kuhakikisha kwamba, kabla ya kujimwaga katika utume wa Uinjilishaji Mpya, Kanisa lenyewe linapaswa kujiinjilisha kwanza.
Familia ya Mungu nchini Korea katika maadhimisho ya Mwaka wa Imani, inapaswa kujikita katika toba na wongofu wa ndani; kuimaraisha imani, matumaini na mapeno kwa njia ya maisha ya Kisakramenti, Tafakari ya kina ya Neno la Mungu, Tafakari ya Mafundisho ya Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, bila kusahau kujichotea utajiri unaofumbatwa katika Mafundisho Jamii ya Kanisa, ambayo kimsingi ni Biblia ya Waamini walei katika mchakato wa kuyatakatifuza malimwengu. Waamini wanapaswa kuhakikisha kuwa, imani yao inajionesha katika matendo.
Maadhimisho ya kumbu kumbu ya Miaka ishirini ya Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki, iwe ni fursa kwa waamini kufanya tafakari ya kina kwa kushirikishana kuanzia ndani ya Familia, Jumuiya Ndogo ndogo za Kikristo, Parokia na Jimbo katika ujumla wake. Familia ya Mungu ijifunze kushirikishana utajiri wa Nyaraka mbali mbali za Kanisa kwa kutumia njia za mawasiliano zilizopo, ili kweli za Kiinjili ziweze kuwafikia na kuwagusa wengi katika maisha na vipaumbele vyao.
Maaskofu wanakazia kwa namna ya pekee mikakati inayolenga kuimarisha Jumuiya ndogo ndogo za Kikristo, mahali ambapo imani katika matendo inajionesha kwa kiasi kikubwa. Hapa ni mahali waamini wanaposhirikishana utajiri wa Neno la Mungu;Maandalizi kwa ajili ya kupokea Sakramenti mbali mbali za Kanisa pamoja na utekelezaji wa mipango ya shughuli za kichungaji.
Waamini walei, watambue dhamana na wajibu wa kujikita katika Uinjilishaji wa Jamii, kwa njia ya utakatifu wa maisha; Utume wa Familia pamoja na kuwahusisha vijana katika maisha na utume wa Kanisa, kwani hawa ni tegemeo la Kanisa kwa sasa na kwa siku za usoni. Vijana wakiwa imara na thabiti, Kanisa linauhakika wa kuendelea kutekeleza utume wake hata kwa siku za usoni.
Maaskofu wanasema kwamba, kuna mambo kadhaa ambayo Waamini katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani wanapaswa kuyatekeleza kwa umakini, uchaji na moyo wa ibada. Wanapaswa kuimarisha Imani, inayokuzwa na kukomaa katika maisha ya Sala; Mafundisho Tanzu ya Kanisa; Katika Maadhimisho ya Liturujia ya Kanisa, hususan Sakramenti ya Ekaristi Takatifu na ile ya Upatanisho na kwamba, matendo ya huruma yawe ni matunda ya Imani tendaji.
Waamini waongozwe na kauli mbiu inayowataka kuhakikisha kuwa Familia ya Mungu inajikita katika kutangaza Injili. Itakumbukwa kwamba, Mwaka 2012, Baraza la Maaskofu Katoliki Korea lilikazia umuhmu wa Sala katika Familia. Kipaumbele bado kinaendelea kutolewa kwa utume wa Familia kwani Familia katika ulimwengu mamboleo wanasema Maaskofu inakabiliwa na changamoto hasi zinazotaka kufifisha maana, utume na dhamana ya Familia katika Kanisa na Jamii kwa ujumla. Vijana wahusishwe kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa.
Maaskofu wa Kanisa Katoliki Korea wanasema kwamba, kwa njia hii, kutakuwepo na uwezekano mkubwa wa kuona matunda ya Mwaka wa Imani katika uhalisia wa maisha ya waamini wenyewe. Mwaka wa Imani, usipite na kuwaacha waamini wakiwa wakavu kama kigae, bali iwe ni fursa ya kuifahamu, kuishuhudia na kuitangaza Imani ya Kanisa Katoliki inayojikita katika Fumbo la Mateso, Kifo na Ufufuko wa Yesu Kristo, Mkombozi wa Dunia.







All the contents on this site are copyrighted ©.