2013-01-28 08:08:41

Juma la kuhamasisha miito ya kitawa ndani ya Kanisa nchini Ureno


Mahujaji wa Imani, mitume wa Uinjilishaji Mpya ndiyo kauli mbiu inayoongoza maadhimisho ya Juma la Kuombea Miito Mitakatifu nchini Ureno, linaloanza hapo tarehe 27 Januari hadi tarehe 3 Februari 2013. RealAudioMP3

Maaskofu Katoliki nchini Ureno wanabainisha kwamba, kwa namna ya pekee, watawa ni mahujaji wa imani, mitume wenye nguvu na uzuri wa imani ni watu wanaosukumwa na upendo wa Kristo ili kujitoa kimaso maso kwa ajili ya mchakato wa Uinjilishaji, sehemu mbali mbali za dunia.

Hii ni dhamana kwa Wakristo wote waliobatizwa ndani ya Kanisa, lakini, ni changamoto ya pekee inayofanyiwa kazi na watawa katika maisha yao ya kila siku, kwa kumfuasa Kristo katika maisha ya utii, ufukara na usafi kamili. Hiki ni kielelezo cha neema na ushuhuda unaoonesha muungano wao wa karibu na Mwenyezi Mungu. Itakumbukwa kwamba, imani ya kweli ni jibu endelevu linaloonesha katika uhalisia wa maisha, ile nguvu inayotenda kazi ndani mwao; nguvu ambayo Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita anasema, inapaswa kukua na kukomaa, ili kutoa matunda yanayokusudiwa, yaani wongofu na utakatifu wa maisha.

Imani tendaji anasema Baba Mtakatifu inajionesha hata katika vipaumbele vya maisha ya waamini, lakini kwa watawa, imani hii ni kielelezo cha mikakati ya huduma inayotolewa na Mama Kanisa kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, kutokana na hali yao ya maisha. Ni imani inayobubujika katika maisha ya watawa kwa kukutana na Yesu Kristo aliyeuabadili maisha na vipaumbele vyao.

Ni Makatekista wa kwanza wa Imani, wanaojitoa kila siku, kurithisha imani hii kwa watoto na vijana wanaofanya hija ya kumtafuta, kumfahamu ili hatimye, kumpenda na kumtumikia Mungu kwa njia ya Yesu Kristo.

Watawa ni kielelezo cha imani inayoungamwa na Mama Kanisa, Imani ambayo inaadhimishwa katika Mafumbo ya Kanisa, kwa namna ya pekee katika maadhimisho ya Sakramenti mbali mbali za Kanisa zinazomkirimia mwamini baraka na neema anazohitaji katika hija yake ya Imani. Kwa namna ya pekee, hii ni Imani inayojidhihirisha katika maisha ambayo yanaoongozwa na Amri za Mungu, ili kumwezesha mwamini kuwa adili katika maneno na matendo yake. Mwishoni, hii ni Imani inayomwilishwa katika Sala.

Watawa ni mashahidi hai wa Injili ambayo inamwilishwa katika uhalisia wa maisha, kwa kuonesha uzuri na nguvu ya imani tendaji katika maisha ya mwamini. Ndiyo maana Baraza la Maaskofu Katoliki Ureno, linawaalika Watawa kwa namna ya pekee, kukumbatia Fumbo la Imani, sababu maalum ya wito na maisha yao, changamoto ya kuendeleza utume wa Kanisa unaojikita katika Uinjilishaji Mpya, kwa kusoma alama za nyakati, kwa kutambua kwamba, hata Wakristo wengine wanashiriki dhamana hii, lakini kwa kiwango tofauti.

Maaskofu wanasema, Waamini wanaweza kuendelea kutangaza Habari Njema ya Wokovu kwa njia ya Sala endelevu; Katekesi ya kina; elimu ya dini shuleni, kwa kumwilisha Injili katika matendo ya huruma pamoja na kujitoa kimaso maso kuwatangazia Injili wale ambao bado hawajabahatika kusikia Injili ya Kristo ikitangazwa katika viunga vyao.

Kiungo makini katika kutangaza Imani ni ushuhuda unaotolewa na waamini wote kila mtu kadiri ya maisha na wito wake ndani ya Kanisa. Ni mwaliko wa kuendelea kuyatakatifuza malimwengu kwa njia ya tunu msingi za Kiinjili, Maadili na Utu wema, kwani kuna hatari kubwa kwamba, watu wengi wakaendelea kumezwa na malimwengu.

Baraza la Maaskofu Katoliki Ureno, linawashukuru na kuwapongeza Watawa wa Mashirika ya kitawa na kazi za kitume wanaofanya kazi zao ndani na nje ya Ureno kwa ushuhuda makini na endelevu wanaoutoa kwa maisha na utume wa Kanisa.








All the contents on this site are copyrighted ©.