Askofu Msaidizi Eusebius Nzigilwa wa Jimbo kuu la Dar es Salaam, Alhamisi, tarehe
24 Januari 2013 ameongoza Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa la Mtakatifu Gaspar
del Bufalo, Jimbo kuu la Dar es Salaam kwa ajili ya kumwombea Marehemu Padre Joachim
Minja Ndelianarua aliyefariki dunia hapo tarehe 22 Januari 2013.
Yafuatayo
ni mahubiri yaliyotolewa na Mheshimiwa Padre Reginald Mrosso, C.PP.S, Mkuu wa Shirika
la Wamissionari wa Damu Azizi ya Yesu, Vikarieti ya Tanzania, kama sehemu ya Katekesi
ya kina, wakati huu Mama Kanisa anapoadhimisha Mwaka wa Imani. Matukio kama haya yawe
ni nafasi ya kutafakari kuhusu Imani ya Kikristo katika Fumbo la Kifo.
MWANADAMU;
KKK 1008 na 413 tunasoma hivi; kifo ni tokeo la dhambi. Na kwamba mwanadamu ndiye
asili ya mauti – kinyume cha muumba wake – Mwa. 3. Kifo cha kweli ni kifo cha mwenye
dhambi. Mamlaka ya ufundishaji wa kanisa, mfafanuzi halisi wa matamshi ya Maandiko
Matakatifu na mapokeo hufundisha kwamba kifo kimeingia ulimwenguni kwa sababu ya dhambi
ya mwanadamu – Hek. 1,13 – yaani, Mungu hakuifanyiza mauti, wala haimpendezi walio
hai wakipotea; Rom. 5,12. Ingawa mwanadamu ana hali ya kufa, Mungu alimweka asife.
Kifo kilikuwa ni kinyume cha mipango ya Mungu Muumbaji, nacho kiliingia ulimwenguni
kama tokeo la dhambi – Hek. 2,23-24. Kifo cha kimwili, ambacho mwanadamu angekuwa
huru nacho, ndiye adui wa mwisho wa mwanadamu ambaye lazima kumshinda – 1Kor. 15,26
– adui wa mwisho atakayebatilishwa ni mauti.
MWILI – KKK 990 – neno mwili laeleza
mtu katika hali yake ya udhaifu na ya kufa – Mwa. 6,3; Zab. 56,5; Isa. 40,6. Ufufuko
wa mwili huonyesha kwamba baada ya kifo hakutakuwa na uzima wa roho peke yake bali
kwamba hata miili yetu yenye hali ya kufa itapata tena uzima – Rom. 8,11 – lakini,
ikiwa Roho wake yeye aliyemfufua Yesu katika wafu anakaa ndani yenu, yeye aliyemfufua
Kristo Yesu katika wafu ataihuisha na miili yenu iliyo katika hali ya kufa, kwa Roho
wake anayekaa ndani yenu.
KIFO - KKK 1006 – mbele ya kifo fumbo la hali ya
kibinadamu linakuwa kubwa sana. Kwa namna moja kifo cha mwili ni kawaida, lakini kwa
imani kwa kweli kifo ni mshahara wa dhambi – Rom. 6,23; - kwa maana mshahara wa dhambi
ni mauti, bali karama ya Mungu ni uzima wa milele katika Kristo Yesu Bwana wetu, Mwa.
2,17 – walakini matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula
matunda ya mti huo utakufa hakika. Kwa wale wanaokufa katika neema ya Kristo, kifo
ni ushirika katika kifo cha Bwana, ili kuwezza kushiriki pia ufufuko wake.
Lakini
kwa njia ya Kristo – tunapata uzima mpya – Rum. 8,29, - maana wale aliowajia tangu
asili, aliwachagua tangu asili wafananishwe na mfano wa Mwana wake, ili yeye awe mzaliwa
wa kwanza miongoni mwa ndugu. 2Kor. 5,17, - hata imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo
amekuwa kiumbe kipya, ya kale yamepita, tazama, yamekuwa mapya. Yoh. 14, 5-6 – Tomaso
akamwambia, Bwana, sisi hatujui uendako, nasi twaijuaje njia? Yesu akamwambia, Mimi
ndimi njia na kweli na uzima, mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi. Yoh. 3,5 –
Yesu akajibu, amini, amini, nakuambia, mtu asipozaliwa kwa maji na Roho, hawezi kuuingia
ufalme wa Mungu. Mk. 16,16 – Aaminiye na kubatizwa ataokoka, asiyeamini atahukumiwa.
MAUTI
NA UKOMBOZI.
Mtume Paulo anaelezea mauti na aina fulani ya ukombozi
– Rum. 7,1…. Kwa kifo cha huyo mtu – tunakombolewa na maisha ya zamani – Rum. 7,1-5.
– kwa maana tulipokuwa katika hali ya mwili, tamaa za dhambi, zilizokuwako kwa sababu
ya torati, zilitenda kazi katika viungo vyetu hata tukaizalia mauti mazao. Bali sasa
tumefunguliwa katika torati, tumeifia hali ile iliyotupinga, ili sisi tupate kutumika
katika hali mpya ya roho, si katika hali ya zamani, ya andiko
MAISHA YA
MKRISTO – AINA MBILI ZA KIFO CHA MKRISTO.
1. Kwa njia ya Ubatizo na imani
– Rum. 1,6 – ambao katika hao ninyi mmekuwa wateule wa Yesu Kristo - tumejiunga na
Kristo aliyekufa na kufufuka – Rum. 8,11 – lakini, ikiwa Roho wake yeye aliyemfufua
Yesu katika wafu anakaa ndani yenu, yeye aliyemfufua Kristo Yesu katika wafu ataihuisha
na miili yenu iliyo katika hali ya kufa, kwa Roho wake anayekaa ndani yenu.
KKK
628 – Ubatizo ambao alama yake ya asili na timilifu ni kuzamishwa, waashiria bayana
kushuka kaburini kwa mkristo anayeifia dhambi pamoja na Kristo ili aishi maisha mapya.
Tulizikwa pamoja naye kwa njia ya ubatizo katika mauti yake, kusudi kama Kristo alivyofufuka
katika wafu kwa njia ya utukufu wa Baba, vivyo hivyo na sisi tuenende katika upya
wa uzima – Rom. 6,4; Kol. 2,12 – mkazikwa pamoja naye katika ubatizo, na katika huo
mkafufuliwa pamoja naye, kwa kuziamini nguvu za Mungu aliyemfufua katika wafu; Efe.
5,26.
2. Mauti ya pili – utengano wa mwili na roho hapa duniani.
Wafu
wanafufuka namna gani? KKK 997 – kufufuka maana yake nini? Kwa kifo, mtengano wa roho
na mwili, mwili wa mtu huoza, pindi roho yake huenda kukutana na Mungu ikingojea kuunganika
na mwili uliotukuka. Mungu, kwa uwezo wake mkuu, atairudishia kwa hakika miili yetu,
uzima usioharibika kwa kuiunganisha na roho zetu, kwa nguvu ya ufufuko wa Yesu.
KKK
– 1005 – Ili kufufuka pamoja na Kristo, ni lazima kufa pamoja na Kristo; ni lazima
kutokuwamo katika mwili na kukaa pamoja na Bwana – 2Kor. 5,8 – lakini tunao moyo mkuu,
nasi tunaona ni afadhali kutokuwamo katika mwili na kukaa pamoja na Bwana. Katika
kwenda huko, yaani kifo, roho hutengana na mwili – Fil. 1,23. Nayo itaungana na mwili
wake siku ya ufufuko wa wafu.
UFUFUKO
KKK 999
– Namna gani? Kristo amefufuka pamoja na mwili wake hasa – tazameni mikono yangu na
miguu yangu ya kuwa ni Mimi mwenyewe. – Lk. 24,39, lakini hakuurudia uzima wa kidunia.
Wakati huo huo, ndani yake wote watafufuka pamoja na miili yao wenyewe waliyo nayo
sasa, lakini mwili huo utageuzwa katika mwili mtukufu, katika mwili wa kiroho – Fil.
3,21; 1Kor. 15,44. labda mtu atasema: Wafufuliwaje wafu? Nao huja kwa mwili
gani? Ewe mpumbavu, uipandayo haihuiki isipokufa, nayo uipandayo hupandi mwili ule
utakaokua ila chembe tupu … hupandwa katika uharibifu, hufufuliwa katika kutoharibika;
wafu watafufuliwa wasiwe na uharibifu…maana sharti huu uharibikao, uvae kutoharibika,
nao huu wa kufa uvae kutokufa – 1Kor. 15,35-53.
KKK – 998 – Nani
atafufuka? Watu wote waliokufa. Wale waliofanya mema kwa ufufuo wa uzima, na wale
waliotenda mabaya kwa ufufuo wa hukumu - Yoh. 5,29; Dan. 12,2 –tena, wengi wa hao
walalao katika mavumbi ya nchi wataamka, wengine wapate uzima wa milele, wengine aibu
na kudharauliwa milele .
Mwadilifu, maana yake asiye na dhambi, afungamanaye
na Mungu, hafi kabisa – Hek, 11,26 – lakini wewe unaviachilia vyote, kwa kuwa ni vyako,
Ee Mfalme Mkuu mpenda roho za watu, maana roho yako isiyoharibika imo katika vyote.
TAFAKARI
KWA NINI KANISA HUADHIMISHA IBADA YA
MISA YA MAZIKO YA MKRISTO? HUSALI MAKABURINI?
IBADA YA MAZIKO Ni
adhimisho la fumbo la pasaka kwa matumaini. Ni sala ya kanisa – ili kuwaombea wale
wote waliokwisha kuungana na mwili wa Kristo kwa njia ya ubatizo waingie katika uzima.
Ila kabla ya hapo – wapitie katika mauti kama Kristo Bwana wao alivyofanya,
kwa sababu katika ubatizo walikufa pamoja na Kristo na kufufuka pamoja naye.
KUWAOMBEA
MAREHEMU Kanisa linawaombea marehemu ili watakaswe, ikiwa wanahitaji kutakaswa
kabla ya kupokelewa mbinguni wakati miili yao inapobaki ardhini ikingoja kurudi kwa
Kristo na ufufuko wa wafu.
Hii ndiyo sababu kanisa linatolea sadaka ya misa
kwa ajili ya marehemu. Pia kanisa linasali na kuwaombea marehemu kusudi wapate msaada
wa kiroho na waamini walio bado hai wapate matumaini ya uzima ujao mbinguni.
UFUFUKO
WA KRISTO – NI TOFAUTI NA UFUFUKO WETU.
Ufufuko wa Kristo ni tofauti na
ufufuko mwingine – KKK 646 – ufufuko wa Kristo haukuwa kurudi katika maisha ya kidunia,
kama ilivyokuwa ufufuko mwingine alioufanya kabla ya Pasaka; kama ule wa binti Yairo,
wa kijana wa Naim, wa Lazaro. Kwa kweli hayo yalikuwa ni matokeo ya miujiza, lakini
wale waiotendewa miujiza waliyarudia maisha ya kidunia ya kawaida. Wakati fulani watakufa
tena. Ufufuko wa Kristo, kimsingi ni tofauti. Katika mwili wake uliofufuka, anapita
kutoka hali ya kifo kufikia maisha mengine yaliyo juu ya wakati na mahali. Mwili wa
Yesu katika ufufuko umejazwa nguvu ya Roho Mtakatifu; unashiriki maisha ya uzima wa
kimungu katika hali ya utukufu wake, hivi kwamba Mt. Paulo anaweza kusema kuwa Kristo
ni Mtu Mbinguni – 1Kor. 15,35-50.
- Tunasoma katika 1Thes. 4,14 – maana, ikiwa
twaamini ya kwamba Yesu alikufa, akafufuka, vivyo na hao waliolala katika Yesu, Mungu
atawaleta pamoja naye na 1Kor. 15,20 – lakini sasa Kristo amefufuka toka wafu, limbuko
lao waliolala. Kwa kifupi ufufuko wa wakristo wategemea ufufuko wa Kristo.
Mungu Baba anawafufua wakristo kwa nguvu ile ile na karama ile ile aliyomfufua
Yesu Kristo.
Tunaamini kwamba mkristo amepewa
uzima mpya unaomfanya kuwa mtoto wa Mungu – Rum. 8,14 – kwa kuwa wote wanaoongozwa
na Mungu, hao ndio wana wa Mungu.
Mungu
Baba huunganisha Kristo Mfufuka na mkristo kwa imani na ubatizo – Rum. 1,16; 6,4 –
basi tulizikwa pamoja naye kwa njia ya ubatizo katika mauti yake kusudi kama Kristo
alivyofufuka katika wafu kwa njia ya utukufu wa baba, vivyo hivyo na sisi tuenende
katika upya wa uzima.
HITIMISHO
1Kor. 2,6-10
– habari juu ya hekima ya Mungu – walakini iko hekima tusemayo kati ya wakamilifu,
ila si hekima ya dunia hii, wala ya hao wanaoitawala dunia hii, wanaobatilika, bali
twanena hekima ya Mungu katika siri, ile hekima iliyofichwa, ambayo Mungu aliazimu
tangu milele, kwa utukufu wetu, ambayo wenye kuitawala dunia hii hawaijui hata mmoja,
maana kama wangaliijua, wasingalimsulibisha Bwana wa utukufu, lakini kama ilivyoandikwa;
mambo ambayo jicho halikuyaona wala sikio halikuyasikia, wala hayakuingia katika moyo
wa mwanadamu, mambo ambayo Mungu aliwaandalia wampendao. Lakini Mungu ametufunulia
sisi kwa Roho. Maana Roho huchunguza yote, hata mafumbo ya Mungu.