2013-01-25 07:57:47

Sikuu ya kuongoka kwa Mtakatifu Paulo, mtume na Mwalimu wa Mataifa: kutembea katika furaha na sherehe


Katika siku hii ya nane na ya mwisho ya kuombea Umoja wa Wakristo, wazo letu kuu ni kutembea katika furaha na sherehe. RealAudioMP3
Kwenda kwa unyenyekevu na Mungu maana yake kutembea katika furaha na sherehe. Mtu anayewatembelea wenye shida na dhiki anakutana nao katika furaha na dhiki zao. Mfano mzuri ni wa wale walio na matatizo mazito ya umilikaji wa ardhi, wasiokuwa na makazi na kazi.
Hata katika masomo ya leo tunaona ujumbe wa matumaini na sherehe Nabii Habakuki anafurahi katika Bwana wakati wa ukame na njaa. Ushuhuda ya kwamba Mungu atakuwa pamoja na watu wake katika matatizo yao ni sherehe ya matumaini. Bikira Maria anamtembelea binamu yake Elizabet kufurahi naye katika ujauzito wake. Anaimba ”Magnificat”, utenzi wake wa kumtukuza Mungu, utenzi wenye matumaini hata kabla mtoto wake hajazaliwa.
Kutoka gerezani, Mtakatifu Paulo Mtume kwa Mataifa anazihimiza Jumuia za Kikristo zilizoko Filipi kufurahi na kusherehekea akisema: Furahini katika Bwana siku zote. Katika Biblia, sherehe na furaha inahusishwa na matumaini katika uaminifu wa Mungu.
Tunaposali kuomba umoja wa Wakristo wiki hii, tukiwa katika siku ya mwisho, tukiiombea kwa namna ya pekee wakati huu Jumuia ya Wadalit kule India, tujiangalie, tujichunguze pia sisi wenyewe juu ya utambuliko wa hali yetu ya kikikristu katika njia ya imani.
Sherehe na furaha yetu ya kuwa na umoja miongoni mwetu sisi wakristo bado lazima ipokelewe katika matumaini na mapambano. Imejikita katika matumaini kwamba Sala ya Kristo ili tuwe wamoja itatekelewa katika muda wa kimungu na kupitia njia za kimungu. Ina msingi katika shukrani kwamba umoja ni zawadi ya Mungu na katika kutambua kwamba umoja tulio nao kama marafiki wa Yesu ni ule unaoonekana katika ubatizo.
Imejisimika katika imani kwamba, Mungu anamwita kila mmoja wetu kufanya kazi kuleta umoja na kwamba juhudi zetu zitatumiwa na Mungu, tukimuamini Mtakatifu Paulo anayetuambia, katika kila katika Sala na shukrani maombi yenu yajulikane kwa Mungu. Kutembea na Mungu kuelekea umoja wa kanisa kunatuhitaji tutembee kinyenyekevu na Mungu katika sherehe na furaha, katika sala na matumaini.

SALA
Ee mungu wa rehema, tunaomba roho wako mtakatifu azijaze jumuia zetu furaha na sherehe ili tuweze kuufikia umoja tunaoushiriki tayari na kuendelea kwa bidii moja kuutafuta umoja unaoonekana. Tunafurahi katika imani na matumaini kwa jina la wale wote wanaokataa heshima yao kupungua, tukiona ndani yao neema na ahadi ya uhuru.
Tunaomba utufundishe kushiriki furaha na kujifunza kutokana na uvumilivu wao. Washa tena ndani yetu matumaini na tegemeza maazimio yetu, ili kwa jina la yesu Kristu tuweze kutembea pamoja katika upendo, tukiinua sauti ya pamoja kwa upendo, tukiimba kwa pamoja kukuabudu. Mungu wa uzima tuongoze katika njia ya haki na amani. Amina.
MASWALI
Ni mapambano gani kuelekea kwenye haki yapo katika jumuia yako? Ni nini chanzo cha kusherehekea?
Ni mapambano gani kuelekea Umoja wa Wakristo yapo katika jamii yako? Je, chanzo cha kusherehekea ni kipi ?
Tafakari hii imeandaliwa na Padre Emmanuel Nyaumba.









All the contents on this site are copyrighted ©.