Shirika la Kikatoliki la Maisha na Familia nchini Canada, linapinga muswada uliopitishwa
hivi karibuni nchini humo wa kutaka ipitishwe sheria itakayowaruhusu madaktari kuwasaidia
watu kupata kifo laini au kwa lugha ya kitaalam, eutanasia. Shirika hili linaunga
mkono jitihada za Serikali ya Canada kuhakikisha kwamba, wagonjwa walioko kufani wanapata
tiba mahususi, kama heshima kwa utu wa mgonjwa, lakini wanapinga vikali madaktari
kutoa msaada wa kitabibu kwa wagonjwa walioko kufani ili eti waweze kufa kwa heshima!
Vitendo vya namna hii ni kuvunja sheria, maadili ya kazi pamoja na athari
nyingine zinazoweza kupatikana kutokana na utekelezaji wa muswada huu. Maisha ni zawadi
kutoka kwa Mwenyezi Mungu inapaswa kuheshimiwa, kuthaminiwa na kulindwa na wala si
jambo la kuchezea kadiri ya matakwa ya wanasiasa madarakani.
Tayari Shirika
hili limekwisha wasilisha pingamizi la kisheria dhidi ya muswada huu kwani ni mauaji
yanayotaka kuhalalishwa kwa njia ya sheria za nchi, kinyume kabisa cha Katiba inayotetea
uhai wa mtu! Ukweli ni kwamba, hata katika nchi zile ambazo Eutanasia imekubalika
kisheria kama Ubelgiji, lakini imekuwa ni vigumu sana kuweza kudhibiti vitendo vya
madaktari katika kutoa uhai wa mwanadamu.
Muswada wa sheria wa kifo laini
unatarajiwa kujadiliwa na Bunge la Canada Mwezi Juni, 2013. Lakini kwa watu wanaotaka
kusimama kidete kulinda na kutetea haki msingi za binadamu, huu ni wakati wa kuchukua
hatua ili kupinga vitendo kama hivi kwani hapa ni mauaji na wala hakuna huruma kwa
wagonjwa wanaoteseka! Kama sheria hii itapitishwa, basi itakuwa ni sheria ya mauaji
nchini Canada.
Waswahili wanasema, ukiona mwenzako ananyolewa, wewe anza kutia
maji! Sheria hizi zinaanza safari yake mbali huko Ughaibuni, baada ya miaka michache
zinaibuliwa pia katika Nchi Maskini duniani kama sehemu ya masharti ya kupata misaada!