Jiji la Roma limeamua kumuenzi Mwenyeheri Yohane Paulo II
Eneo linaloangaliana na Lango kuu la Makao Makuu ya Jimbo kuu la Roma, kwenye Kanisa
kuu la Mtakatifu Yohane wa Laterano, litapewa jina la Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili,
kama kielelezo cha heshima ya kutambua mchango wa Baba Mtakatifu Yohane Paulo wa Pili,
aliyeliongoza Kanisa Katoliki kuanzia mwaka 1978 hadi mwaka 2005.
Kanisa likatambua
utakatifu na mchango wake katika maisha na utume wa Kanisa; hapo tarehe Mosi Mei,
2011 akatangazwa kuwa Mwenyeheri na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita. Uongozi
wa Jiji la Roma unabainisha kwamba, Yohane Paulo wa Pili amekuwa ni Kiongozi mkuu
wa Kanisa, lakini zaidi ya yote, alikuwa ni mtu mwenye imani thabiti, ambaye kwa njia
ya imani hiyo ameweza kubadili uso wa dunia katika karne ya ishirini. Ndiyo maana
Jiji la Roma linapenda kumuenzi Yohane Paulo wa Pili ambaye amejidhihirisha kuwa ni
Baba wa wote.
Baada ya taratibu kukamilika, eneo hili ambalo liko mbele ya
Lango kuu la kuingilia kwenye Makao Makuu ya Jimbo kuu la Roma, sehemu ya Uwanja wa
Kanisa kuu la Mtakatifu Yohane wa Laterano utajulikana kama "Largo Giovanni Paolo
II- Karol Josef Wojtyla - Pontefice 1978 - 2005".