2013-01-22 10:19:39

Ukeketaji ni mila na desturi zilizopitwa na wakati


DR. Olav Fykse Tveit, Katibu mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni, hivi karibuni alisema kwamba, anaunga mkono jitihada za Jumuiya ya Kimataifa kupiga rufuku mila na desturi zilizopitwa na wakati, zinazoendelea kuleta madhara na usumbufu mkubwa miongoni mwa wanawake, kiasi cha kuwanyima haki zao msingi. Mila za ukeketaji bado ziko katika Jamii nyingi za Kiafrika na sehemu nyingine za dunia.

Dr. Tveit anasema, kama kiongozi wa Kanisa anaunga mkono juhudi zinazofanywa na Serikali pamoja na wanaharakati mbali mbali, ambao wameendelea kusimama kidete kulinda na kutetea haki msingi za wanawake, dhidi ya mila na tamaduni zilizopitwa na wakati, zinazoendeleza nyanyaso kwa wanawake na wasichana sehemu mbali mbali za dunia.

Ukeketaji una madhara makubwa kwa maisha ya wasichana na wanawake, wakati mwingine, mila hizi zimepelekea vifo vya wanawake na wasichana kutokana na kutokwa na damu kwa wingi. Ni mila ambayo imewasababishia wanawake kupata maumivu makali wakati wa kujifungua na hivyo kuhatarisha maisha yao wenyewe na watoto wanaowabeba tumbaoni mwao.

Anaunga mkono juhudi za kutokomeza mila na desturi zilizopitwa na wakati, kwani wanawake wanapaswa pia kuheshimiwa na kuthaminiwa utu na heshima yao! Dr. Tveit ameyasema hayo hivi karibuni alipokuwa anashirikisha mawazo yake na Wanaharakati wa kimataifa wanaopinga mila na desturi zilizopitwa na wakati dhidi ya utu na heshima ya wanawake, alipokutana nao kwenye Makao Makuu ya Baraza la Makanisa Ulimwenguni.

Anasema, Baraza la Makanisa Ulimwenguni, Mwezi Oktoba 2013, litafanya Mkutano Mkuu, huko Busan nchini Korea. Mada itakayoongoza Mkutano huu ni "Mungu wa uhai, tuongoze katika haki na amani".Anasema, imani yao kwa Mungu wa uhai ndiyo inayowawajibisha kusimama kidete kupinga mila na desturi zinazomdhalilisha mwanamke. Kuna idadi kubwa ya wasichana ambao maisha yao yako hatarini kutokana na baadhi ya Jamii kuendekeza mila na desturi za ukeketaji, ambazo kwa sasa zimepitwa na wakati.

Dr. Tveit anaungana na viongozi mbali mbali wa kidini kupinga vitendo vya unyanyasi wa kijinsia wanavyofanyiwa wanawake kwa kisingizio cha kuendeleza mila na desturi, hata kama zimepitwa na wakati. Haki msingi za wanawake zinapaswa kulindwa na kuheshimiwa.







All the contents on this site are copyrighted ©.