2013-01-22 07:44:15

Siku ya tano ya kuombea Umoja wa Wakristo: kutembea kama rafiki wa Yesu


Katika siku hii ya tano wazo letu kuu ni Kutembea kama rafiki wa Yesu. Kutembea kinyenyekevu na Mungu hakumaanishi kutembea pekee kama nafsi moja - ina maana kutembea na wale ambao ni ishara za uwepo wa Mungu kati yetu, marafiki zetu. “Nimewaita ninyi rafiki" anasema Yesu katika Injili ya Yohane. RealAudioMP3
Katika uhuru wa upendo tunaweza kuchagua marafiki zetu na kuchaguliwa kuwa marafiki. “Hamkunichagua mimi bali ni mimi niliyewachagua ninyi”, Yesu anatufundisha. Urafiki na Yesu unapita fikara na mahusiano yetu ya kifamilia na kijamii. Inahusiana na upendo wa kudumu wa Mungu kwa viumbe vyote.
Wimbo wa Mfalme Sulemani umetafsiriwa kwa namna mbalimbali kama wimbo wa upendo wa Mungu kwa waisraeli, au upendo wa Kristu kwa kanisa. Ile hamu waliyonayo wanaopendana ndio ushuhuda wa pekee unaopita mipaka ya kijamii. Upendo wa Mungu unawafikia kwa karibu sana wenye dhiki. Watu wenye dhiki wanajua kuwa wakati Mungu anawaangalia anafanya hivyo katika upendo wake.
Yesu anawaambia watu wenye dhiki kuwa “nimewaita ninyi rafiki”. Ni aina ya kukombolewa kutoka katika utumwa wa manyanyaso na dharau inayoletwa na matabaka ndani ya jamii. Watu wenye dhiki hivyo wana wajibu wa kuwa marafiki wa Yesu. Na Mungu anatutaka tufanye nini sisi ambao tunaitwa kutembea naye kama marafiki zake? Kanisa linaitwa kuwakumbatia wenye shida popote lilipo kama marafiki wa kawaida.
Wito huu wa kuwa marafiki na marafiki wa Yesu ni namna nyingine ya kuelewa umoja wa kanisa ambao tunaomba wiki hili. Wakristo kutoka kona zote za dunia wanaitwa kuwa marafiki na wale wote wanaopambana na ubaguzi na madhulumu. Kutembea katika umoja wa Kanisa kunatuhitaji kutembea kinyenyekevu na Mungu na kama marafiki wa Yesu.
SALA
Ee Yesu toka mwanzo wa uhai wetu umejitoa kwetu kama rafiki yetu. Upendo wako unawakumbatia wanadamu wote, hasa wale waliotengwa na kukataliwa kwa sababu ya tofauti za madaraja, utaifa, rangi, walizojitengenezea watu. Tukiwa tumejawa na uthabiti na uhakika wa heshima tuliyo nayo kwako, tunaweza kutembea pamoja kwa umoja kumwendea kila mmoja wetu na kumpokea na kumkumbatia katika roho, kama mwana wa Mungu. Mungu wa uzima tuongoze katika njia ya haki na amani. Amin.
MASWALI
Je, ni watu gani walioko katika jumuia yako ambao Yesu anakuita kujenga urafiki nao?
Ni kitu gani kinawazuia marafiki wa Yesu yaani sisi, kuwa marafiki sisi kwa sisi?
Je, ni kwa jinsi gani kuwa marafiki wa Yesu mwenyewe kunalipa changamoto Kanisa lililogawanyika?
Tafakari hii imeandaliwa na Padre Emmanuel Nyaumba.








All the contents on this site are copyrighted ©.