2013-01-21 10:34:52

Rais Obama aapa kuongoza Marekani kwa kipindi kingine cha miaka 4


Rais Barack Obama wa Marekani, Jumapili, tarehe 20 Januari 2013 aliapishwa rasmi kuanza awamu ya pili ya uongozi wake kwa miaka mingine minne. Ameapa kulinda na kutetea katiba ya nchi. Hafla hii imehudhuriwa na watu wachache kwani ilikuwa ni utekelezaji wa Katiba inayosema kwamba, Rais baada ya kuchaguliwa atapaswa kuapishwa tarehe 20 Januari.

Wakati huo huo, Makamu wa Rais Joe Biden aliapishwa mapema asubuhi na baadaye kwa pamoja walikwenda kutoa heshima na kuweka shada la maua kwa Askari wa Marekani waliopoteza maisha vitani. Awamu ya Pili ya uongozi wa Rais Obama unakabiliwa na changamoto ya kuendelea kufufua na kurekebisha uchumi; kuweka bayana sera kuhusu wahamiaji pamoja na mkakati wa kudhibiti silaha za moto nchini Marekani.

Utamaduni wa kuachiana madaraka kwa njia ya amani ni tukio ambalo linawaunganisha Wamarekani wote kwa kuweka kando misimamo yao ya kisiasa, ili kuonesha umoja wa kitaifa na ukomavu wa kisiasa na kidemokrasia.







All the contents on this site are copyrighted ©.