Onesheni mshikamano wa dhati na watu wenye ulemavu kwa kuwawezesha kiuchumi ili wajitegemee!
Waziri Mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda amesema, suala la uchangiaji wa VICOBA kwa ajili
ya watu wenye ulemavu linahitaji kupangiwa mkakati maalum ili zipatikane fedha za
kutosha kuwapa mitaji nao pia wajitegemee. Amesema yuko tayari kukaa na Mkurugenzi
Mtendaji wa IPP, Bw. Reginald Mengi ili wabungue bongo ya jinsi ya kutunisha mfuko
wa VICOBA kwa ajili ya watu wenye ulemavu.
Ametoa ahadi hiyo Jumapili, Januari
20, 2013 wakati akizungumza na watu wenye ulemavu wa mkoa wa Dar es Salaam katika
hafla yao ya chakula cha mchana ya kuukaribisha mwaka mpya 2013 iliyofanyika kwenye
ukumbi wa Diamond Jubilee jijini Dar es Salaam. Hafla hiyo iliandaliwa na Bw. Mengi.
“Bwana
Mengi amewasha moto mzuri kwa kuwachangia hawa watu sh. milioni 100. Nimeambiwa kuwa
walianza kwa kujichangisha sh. milioni 17. Najua nami nawajibika kuwachangia lakini
itabidi nikae naye tuone jinsi huduma hii inavyoweza kusambaa na kuwafikia Watanzania
wengi zaidi,” alisema Waziri Mkuu.
Alisema ili uwe mpango endelevu, wabuni
mpango utakaowajumuisha Watanzania wengi zaidi, wakiwemo wanasiasa, viongozi wa dini
na wengine wengi. “Nia yetu ni kila mwenye nacho achangie ili kuwasadia wenzetu wawe
na miradi ya kujikimu kimaisha kupitia mikopo ya VICOBA,” alisema.
Akijibu
risala ya watu wenye ulemavu iliyosomwa na Mwenyekiti wa Shirikisho la Vyama vya Watu
wenye Ulemavu Tanzania (SHIVYAWATA), Bi. Lupi Maswanya ambayo ilikumbushia ombi la
kupatiwa Ofisi ya kudumu, Waziri Mkuu alisema ahadi yao bado anaikumbuka, hajaisahai
ila bado naifanyia kazi.
Katika risala yao, watu wenye ulemavu pia waliiomba
Serikali iharakishe kutoa kanuni za Sheria Na. 9 ya mwaka 2010 ya Haki za Watu wenye
Ulemavu ili kuharakisha muundo wa Baraza la walemavu na kamati zake.
“Pia tunaiomba
Serikali itohoe kwa lugha nyepesi na kuitangaza sheria hiyo katika vyombo mbalimbali
ikiwemo kuiweka kwenye maandishi ya nukta nundu kwa ajili ya watu wenye uoni hafifu,”
ilisema sehemu ya risala yao.
Pia walimuomba Rais Jakaya Kikwete amteue Mwenyekiti
wa Baraza la Ushauri la Taifa la Watu wenye Ulemavu ili kuharakisha uundwaji wa Baraza
na Kamati zake kwa mujibu wa sheria hiyo.
Mapema akimkaribisha Waziri Mkuu
kuongea na hadhara hiyo, Bw. Mengi aliiomba Serikali iangalie uwezekano wa kukabili
tatizo la dawa za kulevya kwa namna ya pekee kwani linachangia kwa kiasi kikubwa tatizo
la watu wenye matatizo ya akili nchini. “Hawa nao wanageuka kuwa watu wenye ulemavu
wa akili,” alisema.
Naye muasisi wa VICOBA nchini, Bi. Devotha Likokola alisema
kikundi cha watu wenye ulemavu kimefikisha wanachama 150 lakini kinakabiliwa na changamoto
ya waombaji wengi wenye ulemavu hasa kutoka mikoani.
“Mfuko huu waliuanzisha
wao wenyewe, na kuamua kukopeshana ili wafanye biashara. Bw. Mengi akawaongezea sh.
milioni 100. Wamesema wakiwezeshwa wanahitaji miaka mitano tu nao wataanza kufadhili
watu wengine,” alisema Bi. Likokola.