Kanisa nchini Pwani ya Pembe linamkumbuka Hayati Askofu mkuu Ambrose Madtha
Baraza la Maaskofu Katoliki Pwani ya Pembe, limehitimisha mkutano wake wa Mwaka, Jumapili
tarehe 20 Januari, uliokuwa umefunguliwa hapo tarehe 15 Januari 2013, kwa kumbu kumbu
ya kifo cha Askofu mkuu Ambrose Madtha, aliyekuwa Balozi wa Vatican nchini Pwani ya
Pembe.
Askofu mkuu Madtha alifariki kwa ajari ya gari hapo tarehe 8 Desemba
2012 alipokuwa anatoka katika maadhimisho ya Siku kuu ya Bikira Maria Mkingiwa Dhambi
ya Asili. Mkutano huu umekuwa ni kipindi cha neema na baraka pamoja na kudumisha umoja
na mshikamano miongoni mwa Maaskofu Katoliki wa Pwani ya Pembe.
Maaskofu hao
pamoja na mambo mengine, wamejadili hali ya maisha na utume wa Kanisa na Jamii kwa
ujumla. Kanisa nchini Pwani ya Pembe ni hai na linaendelea kusonga mbele kwa imani
na matumaini makubwa, licha ya changamoto na kinzani mbali mbali zinazoendelea kujitokeza.
Maaskofu wanaendelea kuhimiza waamini na wananchi wa Pwani ya Pembe, kusimama kidete
kulinda, kutetea na kudumisha misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kitaifa,
ili kujipatia maendeleo endelevu.