Boresheni imani yenu kwa Kristo na Kanisa lake kwa njia ya Sala ya Kanisa yenye utajiri
mkubwa kutoka katika Zaburi
Mama Kanisa anawaalika watoto wake katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, kuendelea
kuboresha imani yao kwa Kristo na Kanisa lake kwa njia ya Sala na Tafakari ya Neno
la Mungu; Maisha ya Kisakramenti na Matendo ya huruma, kama kikolezo cha imani tendaji.
Leo katika makala hii, tunaye Mheshimiwa Padre Stephano Kaombe, Gombera wa
Seminari Ndogo ya Visiga, Jimbo kuu la Dar es Salaam, anayetushirikisha tafakari ya
Zaburi ya 96. Ikumbukwe kwamba, Sala za Kanisa ni kwa ajili ya Wakristo wote, kumbe
kuna haja ya kujenga utamaduni wa kusali Sala za Kanisa. Basi huu uwe ni mkakati maalum
katika maadhimisho ya Mwaka wa Kanisa.
Dominika 2 Mwaka C. ZABURI
96
Mwimbieni Bwana wimbo mpya, mwimbieni Bwana, nchi yote. Mwimbieni
Bwana, libarikini jina lake, tangazeni wokovu wake siku kwa siku. Wahubirini
mataifa habari za utukufu wake, na watu wote habari ya maajabu yake.
Kwa
kuwa Bwana ni mkuu mwenye kusifiwa sana, na wa kuhofiwa kuliko miungu yote. Maana
miungu yote ya watu si kitu, lakini Bwana ndiye aliyezifanya mbingu. Heshima
na adhama ziko mbele zake, nguvu na uzuri zimo katika patakatifu pake.
Mpeni
Bwana, enyi jamaa za watu, mpeni Bwana utukufu na nguvu, mpeni Bwana utukufu
wa jina lake. Leteni sadaka mkaziingie nyua zake, mwabuduni Bwana kwa uzuri
wa utakatifu wake; tetemekeni mbele zake, nchi yote.
Semeni katika mataifa,
“Bwana ametamalaki!” Naama, ulimwengu umethibitika usitikisike, atawahukumu
watu kwa adili.
Mbingu na zifurahi, nchi na ishangilie, bahari na ivume
na vyote viijazavyo, Mashamba na yashangilie, na vyote vilivyomo, ndipo miti
yote ya mwituni iimbe kwa furaha; mbele za Bwana, kwa maana anakuja, kwa maana
anakuja aihukumu nchi. Atahukumu ulimwengu kwa haki, na mataifa kwa uaminifu
wake.
Zaburi hii inasadikiwa ilitungwa wakati Waisraeli walipokuwa wanajiandaa
kurudi tena katika nchi yao ya ahadi, toka Uhamishoni Babeli, ndiyo mazingira yake.
Walikuwa wamejaa matumaini na furaha kuu, kutokana na wema Mungu aliowatendea wa kuwapa
nafasi nyingie tena kurejea kwao. Hakuna jambo lililokuwa la thamani kama kwao kumtolea
Mungu sadaka ya wimbo wa sifa.
Iwe ni mwanzo wa mwaka, mwezi, siku mpya tunapoifungua
mioyo yetu au tunapoanza Uinjilishaji mpya; tujiunge na mzaburi kumwimbia Mungu wimbo
mpya wa sifa. Upya si katika kuanza mwaka au katika maneno ya wimbo wetu, la hasha,
upya uwe katika nafasi zetu, roho yetu, akili yetu, utashi wetu. Kristo alituambia
divai mpya katika chombo kipya. Sisi leo maisha yetu, maneno na matendo yetu mbele
ya Mungu na jirani zetu, aidha katika jumuiya zetu ndo divai, ambayo Yesu Kristo ametujalia
kuifanya upya kwa mateso, kifo na ufufuko wake.
Mwimbaji wetu, hana wasiwasi,
kwani Mungu ndiye anayeshika usukani wa chombo chetu, na wala si ‘mpigadebe’ katika
kituo cha daladala au matatu!. Kutokana na ukweli huu ndio maana anaweza kuuambia
ulimwengu uwe na furaha na amani. Kwani haki inatawala kwa wote.
Mzaburi anashadidia
umuhimu wa mazingira: miti yote ya mwituni iimbe kwa furaha, twapaswa kuyapenda na
kuyatunza, kwani nayo yana nafasi katika kumsifu Mungu. Kuharibu mazingira ni sawa
na kuharibu ala ya muziki wa sifa kwa Mungu, ni ukosefu mkuu. Tunataadharishwa, kwamba
twapaswa kumsifu Mungu, kwani tusipomsifu Yeye anayetamalaki nchi, miungu ya uongo
itachukua nafasi yake kwa hila, nayo ni ubinafsi, pesa, rushwa, ugomvi, ulevi, uhasherati,
umbeya, choyo na ufisadi mwingine mwingi. Kila mmoja wetu katika juma hili kwa maneno
na matendo yake, kwa dhati na amhimidi Mungu!
Dominika 3 Mwaka C. ZABURI
19
Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu, na anga laitangaza kazi ya mikono
yake. Mchana husemezana na mchana, usiku hutolea usiku maarifa.
Hakuna
lugha wala maneno, sauti yao haisikilizani. Sauti yao imeenea duniani mwote, na
maneno yao hata miisho ya ulimwengu.
Katika hizo ameliwekea jua hema, kama
bwana arusi akitoka chumbani mwake, lafurahi kama mtu aliye hodari kwenda mbio
katika njia yake. Kutoka kwake lautoka mwisho wa mbingu, na kuzunguka kwake
hata miisho yake, wala kwa hari yake hakuna kitu kilichositirika.
Sheria
ya Bwana ni kamilifu, huiburudisha nafsi. Ushuhuda wa Bwana ni amini, humtia
mjinga hekima. Maagizo ya Bwana ni ya adili, Hufurahisha moyo. Amri ya Bwana
ni safi, huyatia macho nuru.
Kicho cha Bwana ni kitakatifu, kinadumu
milele. Hukumu za Bwana ni kweli, zina haki kabisa. Ni za kutamanika kuliko
dhahabu, kuliko wingi wa dhahabu safi. Nazo ni tamu kuliko asali, kuliko
sega la asali.
Tena mtumishi wako huonywa kwazo, katika kuzishika kuna thawabu
nyingi. Ni nani awezaye kuyatambua makosa yake? Unitakase na mambo ya siri. Umzuie
mtumishi wako asitende mambo ya kiburi, yasinitawale mimi. Ndipo nitakapokuwa
kamili, nami nitakuwa safi, sina kosa lililo kubwa.
Maneno ya kinywa changu, na
mawazo ya moyo wangu, yapate kibali mbele zako, Ee Bwana, mwamba wangu, na mwokozi
wangu.
Zaburi hii inahundwa na zaburi mbili, yaani aya 1-6 na aya 7-14. Sehemu
ya kwanza inatukuza utukufu wa Mungu katika mbingu na sehemu ya pili (ambayo ndiyo
tunayoiimba katika Dominika hii) inashangazwa na ukuu wa Sheria ya Mungu. Aliyeunganisha
sehemu hizi mbili anatuambia kwamba Sheria ya Mungu ni ajabu kuu kama vile utukufu
wa upatano tuuonao katika mbingu. Nakumbuka nilipokuwa mdogo, watoto tulipenda kuutazama
mwezi usiku, na mara zote tulimwona Mama Bikira Maria katika huo mwezi!
Mzaburi
anatupatia visawe sita vinavyoelezea Torati: ni sheria, ni ushuhuda, ni maagizo, ni
amri, ni kicho na ni hukumu. Mwamini anapaswa kutii sheria ya Mungu kwani ni kamilifu,
huburudisha, uhekimisha, inaudumufu, ni ya haki, kwa yeyote aishikayo ni tamu kama
asali. Ama kweli walicholonga wahenga: usigombane na shani ya Mungu! Sheria yake ni
ya ajabu, ni ya kushangaza machoni mwetu!
Zaburi hii tunapoipa nafasi ituongoze,
inatualika sisi sote kutafakari kwa kina jinsi gani tunavyoiishi sheria ya Mungu.
Anga linamvuto kwa watu kutokana na kufuata kwake maongozi ya Muumba. Kila siku asubuhi
tunapoamka, tunajua mawio yanatokea upande upi. Mimi na wewe leo, ilikuweza kuwa na
upatano na amani katika maisha yetu na katika mahusiano na jirani zetu, twapaswa kufuata
amri ya Mungu na hasa kama ilivyohitimishwa na Yesu Kristo (Soma Mt. 22:26 - 40).
Dominika
4 Mwaka C. ZABURI 71
Nimekukimbilia Wewe, Bwana, nisiaibike milele. Kwa
haki yako uniponye, uniopoe, umenitegea sikio lako, uniokoe. Uwe kwangu mwamba
wa makazi yangu, nitakakokwenda sikuzote. Umeamuru niokolewe, ndiwe genge
langu na ngome yangu.
Ee Mungu wangu, uniopoe mkononi mwa mkorofi, katika
mkono wake mwovu, mdhalimu. Maana ndiwe taraja langu, Ee Bwana Mungu, tumaini
langu tokea ujana wangu. Nimekutegemea Wewe tangu kuzaliwa, ndiwe uliyenitoa
tumboni mwa mama yangu, Nitakusifu Wewe daima.
Nimekuwa kitu cha ajabu kwa
watu wengi, na Wewe ndiwe kimbilio langu la nguvu. Kinywa changu kitajazwa sifa
zako, na heshima yako mchana kutwa.
Usinitupe wakati wa uzee, nguvu zangu
zipungukapo usiniache. Kwa maana adui zangu wananiamba, nao wanaoniotea roho
yangu hushauriana, wakisema, “Mungu amemwacha, mfuatieni, mkamateni, hakuna
wa kumponya.”
Ee Mungu, usiwe mbali nami; Ee Mungu wangu, fanya haraka kunisaidia. Waaibishwe,
watoweshwe, adui za nafsi yangu, wavikwe laumu na aibu, wanaonitakia mabaya.
Nami
nitatumaini daima, nitazidi kuongeza sifa zako zote. Kinywa changu kitasimulia
haki na wokou wako Mchana kutwa; maana sijui hesabu yake.
Nitakuja na mambo
ya ajabu ya Bwana Mungu, nitawakumbusha watu haki yako Wewe peke yako. Ee Mungu,
umenifundisha tokea ujana wangu, Nimekuwa nititangaza miujiza yako hata leo.
Na
hata nikiwa ni mzee mwenye mvi, Ee Mungu, usiniache. Hata niwaeleze watu wa
kizazi hiki nguvu zako, na haki yako, Ee Mungu, imefika juu sana. Wewe uliyefanya
mambo makuu; Ee Mungu, ni nani aliye kama Wewe?
Wewe, uliyetuonesha mateso
mengi, mabaya, utatuhuisha tena. Utatupandisha juu tena tokea pande za chini
ya nchi. Laiti ungeniongezea ukuu! Urejee tena na kunifariji moyo.
Nami
nitakushukuru kwa kinanda, na kweli yako, Ee Mungu wangu. Nitakuimbia Wewe kwa
kinubi, Ee Mtakatifu wa Israeli. Midomo yangu itafurahi sana nikuimbiapo, na
nafsi yangu uliyoikomboa. Ulimi wangu utasimulia haki yako mchana kutwa. Kwa
maana wameaibishwa, wametahayarika, wanaonitakia mabaya.
Hili ni ombolezo
binafsi, kilio cha aliyemzee kwa Mungu. Anaomboleza kwa kuwa amezungukwa na maadui,
anakaribia kifo, ni mzee, japo uzee wake haujakausha chemchemi ya matumaini yake,
wala kudhoofisha moyo wake wa kidini, kwani akitazama nyuma moyo wake unajaa sifu
kwa Mungu ambaye kamwe hajashindwa kumwokoa.
Zaburi hii inaandikwa na mtu ambaye
katika maisha yake amekumbana na magonjwa, majaribu makali, maadui na mabalaa kadhaa.
Sasa anapokuwa mzee, dhaifu na mpweke maadui zake wanakusanyika kupanga jinsi ya kummaliza
kabisa, kwani wanadhani Mungu ameshamtelekeza. Katika wakati huu wa matatizo makubwa,
anamwinulia Mungu macho yake, anapaza kwake kilio chake: “genge lake na ngome yake.”
Mungu ambaye alikuwa mkunga siku ya kuzaliwa kwake na kuendelea kumwongoza na kumlinda
maisha yake yote, kwake ndiye pekee tumaini lake.
Kwa aliye kijana, mzaburi
huyu anakuambia jifunze kumsifu Mungu tokea unapokuwa na umri mdogo. Kwa mzee anakuambia
kamwe usikate tamaa, Mungu yu pamoja nawe. Kwetu sote, tunaalikwa kutazama jinsi gani
tunavyohusiana na wazee, hasa leo tunaposikiwa wastaafu wakinyanyaswa kupata mafao
yao, wazee wakikosa matibabu na uwezo wa kujikimu kutokana na uzee wao tu. Wazee wanavyokuwa
wapweke kutokana na kuwatenga kwetu. Leo tunaalikwa tuwe kimbilio lao kwa wema wetu
kwao!
Papa Yohane Paulo II aliwaandikia wazee barua (1 Oktoba 1999) akionesha
mshikamano nao, kwani naye alishakwisha kula chumvi nyingi wakati anaandika barua
hii. Papa katika barua hii, anawatia moyo wazee kuishi kikamilifu maisha yao, anatuofundisha
thamani ya uzee, lakini hasa anatuasa kuwaheshimu na kuwasaidia katika uzee wao na
si kuwanyanyasa na kuwasukuma katika ‘kifo cha huruma’.
Kwa aliye kijana, mzaburi
huyu anakuambia jifunze kumsifu Mungu tokea unapokuwa na umri mdogo. Tukumbuke amri
ya Mungu: Waheshimu baba na mama, upate miaka mingi na heri duniani! Wazee tulionao
katika familia zetu, jumuiya zetu na jamii yetu, ndio wazazi wetu; tunapaswa kuwaheshimu.
Tafakari
hii imeandaliwa na Padre Stephano Kaombe.