Rais Jakaya Mrisho Kikwete wa Tanzania anaanza ziara rasmi ya Kiserikali nchini Ufaransa,
Jumamosi, Januari 19, 2013, kwa mwaliko wa Rais wa Ufaransa, Mheshimiwa Francois Hollande.
Mara baada ya kuwasili kwenye Uwanja waNdege wa Charles De Gaul mjini Paris,
Rais Kikwete ambaye anafuatana na Mama Salma Kikwete atapokelewa rasmi katika Ufaransa
kwa gwaride na kupokelewa na Waziri wa Misaada ya Maendeleo wa Ufaransa, Mheshimiwa
Paschal Canfin.
Kwa mujibu wa ratiba, Jumapili, tarehe 20 Januari, 2013 Rais
Kikwete atakutana na kufanya mazungumzo na Mama Frannie Leautiera mbaye ni Mtendaji
Mkuu wa Mfuko Private Fund na baadaye atakutana na Mama Marie Christine Saragosse,
Mtendaji Mkuu wa Redio France International (RFI). Mkutano huo utafuatiwa na kikao
kati ya Rais Kikwete na Jumuiya ya Watanzania wanaoishi nchini Ufaransa. Jumatatu,
Rais Kikwete atakutana na kufanya mazungumzo na Mheshimiwa Francois Hollande, Rais
wa Ufaransa kwenye Kasri ya nchi hiyo ya Elysee Palace.
Mazungumzo kati ya
Rais Kikwete na Rais Hollande yatafuatiwa na chakula cha mchana ambako Rais Kikwete
atakaribishwa na Waziri wa Mambo ya Nje wa Ufaransa, Mheshimiwa Laurent Fabius. Baada
ya chakula hicho cha mchana, Rais Kikwete atakutana na kuzungumza na Bwana Yves Louis
Darricarere, Rais wa Kampuni ya Mafuta ya Kimataifa ya Total.
Mazungumzo hayo
yatafuatiwa na mazungumzo mengine kati ya Rais Kikwete na Kiongozi wa Madhehebu ya
Ismailia Duniani H.H The Aga Khan na baada ya hapo, Rais Kikwete atakwenda Kasri la
Luxemburg kukutana na kuzungumza na Rais wa Bunge la Seneti la Ufaransa, Mheshimiwa
Jean Pierre Bel.
Usiku wa Jumatatu, RaisKikwete atakula chakula cha usiku na
Rais wa zamani wa Ufaransa, Mheshimiwa Valery Giscard d’Estaing ambaye ni Mwenyekiti
wa Tanzania Wildlife Conservation Foundation. Jumanne, Rais Kikwete atakuwa na siku
nyingine yenye shughuli nyingi ambako miongoni mwa mambo mengine atakutana na kufanya
mazungumzo na mabalozi wa Afrika wanaowakilisha nchi zao katikaUfaransa, na atakutana
na Mheshimiwa Abdou Diouf, Katibu Mkuu wa Umoja wa Kimataifa wa Nchi Zinazongumza
Lugha ya Kifaransa na Rais wa zamani wa Senegal.
Rais Kikwete pia atashiriki
majadiliano kuhusu masuala ya kimataifa yaliyoandaliwa na Taasisi ya Mahusiano ya
Kimataifa ya Ufaransa – Institute Francais Des Relations International (IFRI) na atakutana
na kuzungumza na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Maendeleo ya Kimataifa la Ufaransa
(AFD).
Rais Kikwete ataondoka nchini Ufaransa Jumatano, Januari 23, 2013, kwenda
Uswisi ambako atatembelea Makao Makuu ya Shirikisho la Soka Duniani (FIFA) mjini Zurich
na baadaye kwenda Davos kuhudhuria mkutano wa mwaka huu wa Shirika la Uchumi Duniani
– World Economic Forum (WEF).