Zingatieni sheria za maabara na jikiteni katika maboresho ya huduma za afya!
Waziri wa afya na Ustawi wa Jamii Dr. Hussein Mwinyi ameitaka bodi ya maabara binafsi
za afya kuchukua hatua kwa wale wanaokwenda kinyume na sheria ikiwepo kusimamisha
huduma na kuwapeleka mahakamani wale watakaokaidi sheria ya kuratibu huduma za maabara
binafsi za afya. Dkt. Mwinyi ameyasema hayo Alhamisi tarehe 17 Januari 2013 alipokuwa
akizindua bodi mpya ya maabara binafsi za afya .Alisema sheria hiyo iliyopitishwa
na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kuanza kutumika mwaka 1998 ilikuwa
na lengo la kuboresha huduma za maabara pamoja na kufanikisha utoaji wa huduma bora
za afya nchini. “Uboreshaji wa mabadiliko ya sekta ya afya ni vema ufanyike sambamba
na uboreshaji wa huduma za maabara ikiwemo uzingatiwaji wa maadili ya utoaji wa huduma
za maabara ili kuepuka athari zinazoweza kutokea kwa mtoa huduma au anayehudumiwa
yaani mgonjwa”alisema Aidha, aliitaka bodi hiyo kuratibu na kukagua majengo,vifaa,vitendanishi
na kuhakikisha usahihi wa majibu ya vipimo ili kuleta ubora wa matokeo ya uchunguzi
wa magonjwa pamoja na kutoa nafasi kwa wataalamu wa maabara kuanzisha huduma hiyo
hapa nchini. “Kazi ya bodi hii ni ya muhimu sana kwani utoaji wa huduma ya tiba
haukamiliki iwapo hakuna huduma ya uchunguzi wa magonjwa,ikiwemo maabara,hivyo maabara
inapofanya kazi zake kwa usahii,inampa nafasi nzuri mganga kuwa na usahii wa tatizo
la mgonjwa na kutoa dawa inayostahili na kutuonesha umuhimu wa kuwa na wataalamu wazuri
wa maabara”. Hata hivyo Waziri huyo ameitaka bodi hiyo kupitia na kufanya maboresho
mapya ya sheria, kanuni na miongozo iliyopo ili iandane na mabadiliko yanayojitokeza
na kuweza kusimamia na kusajili maabara zote nchini. Awali akisoma hotuba yake
Mwenyekiti wa bodi hiyo Dr. Magraret Mhando alisema bodi yake inatarajia kuhakikisha
kuwa vifaa na vitendanishi vyote vinavyotumika nchini vina ubora unaokubalika na vimeorodheshwa
katika orodha ya vifaa na vitendanishi vya maabara ya afya pamoja na kusajili na kuandikishwa
maabara na maduka yote kwa mujibu wa sheria. Bodi mpya ya maabara binafsi za afya
inaundwa na wajumbe wapatao kumi inatarajia kumaliza muda wa utendaji wake kwa miaka
mitatu mwaka 2015.