2013-01-17 09:11:48

Kanisa liko huru kutekeleza wajibu wake na wala halifungwi na Serikali wala Mfumo wowote wa Kisiasa


Askofu mkuu Dominique Mamberti, Katibu mkuu wa Mambo ya nchi za nje na Ushirikiano wa kimataifa mjini Vatican anasema Kanisa liko mstari wa mbele kulinda na kutetea uhuru wa kidini na dhamiri nyofu mintarafu maadili, chapa ya mtu katika masuala ya kidini, utu na heshima ya binadamu, kama alivyobainisha Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, hivi karibuni alipokuwa anazungumza na Mabalozi pamoja na wawakilishi wa nchi na mashirika ya kimataifa mjini Vatican.

Hizi ni nguzo msingi zinazopania kudumisha uhuru na demokrasia. Kuna masuala tete kama vile utoaji mimba na ndoa za watu wa jinsia moja ni mambo ambayo yanapaswa kuangaliwa kwa umakini mkubwa. Askofu mkuu Mamberti anafafanua masuala haya kutokana na uamuzi wa Mahakama ya Ulaya uliotolewa kuhusiana na mfanyakazi mmoja kutoka Uingereza aliyekatazwa kuvaa Msalaba sehemu ya kazi. Pili ni kesi ya mtumishi mmoja aliyekuwa anapingana na Mafundisho na Sheria za Kanisa, kutaka kuendelea kuajiriwa.

Katika Mafundisho Tanzu, Kanisa linafafanua kwamba, liko huru na linatekeleza dhamana na utume wake kwa kuzingatia mafao ya wengi na kuheshimu sheria ambazo zinasimamia haki na wala halifungwi na mfumo wowote ule wa kisiasa. Linaheshimu na kuthamini uhuru wa kidini pamoja na Sheria za Kimataifa.

Kanisa limejikuta kwa nyakati tofauti, likitakiwa kusimama kidete ili kutetea msimamo na uhuru wake dhidi ya Serikali na Mifumo ya Siasa, iliyotaka kuupokonya uhuru wa Kanisa. Inasikitisha kuona kwamba, utamaduni wa nchi nyingi za Ulaya, unataka kukumbatia mawazo mepesi mepesi, ulaji wa kupindukia na ubinafsi, kiasi cha kushindwa kuheshimu asili ya Kanisa ambalo ni Jumuiya ya Waamini inayoongozwa kwa misingi ya imani na akili.

Katika mazingira kama haya anasema Askofu mkuu Mamberti inakuwa ni vigumu kubainisha uhusiano kati ya viongozi wa Serikali na Jumuiya mbali mbali za kidini katika Jamii yenye mchanganyiko mkubwa wa watu mintarafu mshikamano wa kijamii na mafao ya wengi. Katika mazingira kama haya, Vatican inakazia umuhimu wa kuheshimu uhuru wa kidini katika ujumla wake pamoja na kuzingatia mwelekeo wa kijamii, unaoheshimu mtu binafsi na masuala ya kidini katika ujumla wake.

Kanisa linataka sheria, kanuni na taratibu za Jamii ziweze kuheshimiwa, lakini pia Jumuiya za kidini ziwe ni mahali ambapo uhuru wa kidini, amani na utulivu vinazingatiwa. Mafundisho haya yanapata chimbuko lake katika uhuru na yanaweza kutumika kwa dini zote bila ubaguzi.







All the contents on this site are copyrighted ©.