Juma la kuombea Umoja wa Wakristo: Kile ambacho Bwana anataka kutoka kwetu!
Kipindi cha Noeli, Mama Kanisa alipata bahati ya kuadhimisha Fumbo la Umwilisho, linalotanabainisha
Ufunuo wa Mungu kwa Waisraeli, uliojionesha kwa namna ya pekee kwa Musa na Manabii
wa Mungu walioendelea kuweka hai matumaini ya Waisraeli katika utekelezaji wa maagano
ambayo Mwenyezi Mungu alifanya nao. Yesu Kristo, Neno wa Mungu aliyefanyika mwili,
ni Mungu kweli na Mtu kweli, ni daraja na utimilifu wa ufunuo wote. Kwa njia yake,
baraka na neema kutoka kwa Mwenyezi Mungu zimeweza kujionesha miongoni mwa watu na
uso wake kuwaangazia wote.
Ni sehemu ya Katekesi ya Baba Mtakatifu Benedikto
wa kumi na sita, katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, Siku ya Jumatano, tarehe 16
Januari 2013. Baba Mtakatifu anasema, Neno wa Mungu ni daraja kati ya Mungu na mwanadamu,
anayewawezesha waamini kuuona uso na hatimaye, kuzungumza na Mungu ambaye ni Baba
yao. Kwani mtu ambaye amemwona Mwana awe na uhakika kwamba, amekwisha kumwona Baba.
Baba
Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, anawaalika kwa namna ya pekee, waamini na watu
wote wenye mapenzi mema, kujibidisha kuuona uso wa Mungu kwa njia ya: Sala, Tafakari
ya Neno la Mungu na Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu. Yote haya ni kwa ajili
ya kuwaandaa waamini kutafakari mwanga wa Ufalme wake wa milele.
Baba Mtakatifu
anawatakia waamini wote heri na baraka tele, ili waweze kuangaziwa uso wa Mungu na
kuwapatia wingi wa baraka zenye furaha na amani. Anawaalika vijana kujishikamanisha
na Mungu, wakijitahidi kutolea ushuhuda wa ile furaha inayobubujika kutoka katika
Injili.
Amewakumbusha kwamba, tarehe 17 Januari, ya kila Mwaka, Mama Kanisa
anafanya kumbu kumbu ya Siku kuu ya Mtakatifu Anthonio Abate; Mmonaki, Baba wa maisha
ya kiroho na kielelezo makini cha maisha ya Kikristo. Mfano wa maisha yake, uwasaidie
vijana kumfuasa Kristo bila ya kujibakiza; awafariji wagonjwa wote na kuwawezesha
wanandoa wapya kujenga na kuimarisha moyo wa Sala na Ibada.
Kwa namna ya pekee,
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, anawaalika Wakristo wote kushiriki kikamilifu
katika Sala na Tafakari kwa ajili ya Juma la Kuombea Umoja wa Wakristo, litakalozinduliwa
hapo tarehe 18 Januari na kuhitimishwa hapo tarehe 25 Januari, Siku kuu ya Kuongoka
kwa Mtume Paulo, Mwalimu wa Mataifa. Kauli mbiu inayoongoza Sala ya kuombea Umoja
wa Wakristo kwa Mwaka 2013 ni "kile ambacho Bwana anataka kutoka kwetu": ni kutenda
haki, kupenda rehema na kwenda kwa unyenyekevu.
Baba Mtakatifu anasema, hii
ni sehemu ya Kitabu cha Nabii Mika, sura ya 6: 6-8. Anawaalika Wakristo wote kuwa
wadumifu katika kuombea umoja wa Wakristo. Nguvu ya Roho Mtakatifu iwahamasishe kujikita
katika mchakato wa kweli wa umoja wa Wakristo, ili kwa pamoja waweze kuungama kwamba,
Yesu ni Mkombozi wa Dunia.