Mapinduzi ya Zanzibar 1964 yalipania kungo'a ukandamizaji, unyonyaji na ubaguzi
Rais Jakaya Mrisho Kikwete wa Tanzania amesema kuwa moja ya faida kubwa na nyingi
za Mapinduzi ya Zanzibar ni kufunguliwa kwa namna kubwa sana kwa nafasi na fursa za
elimu kwa watoto wa Wazanzibari Wazawa. Sababu kubwa ya Chama cha Afro- Shiraz Party
kufanya Mapinduzi ya mwaka 1964 ilikuwa ni kuondoa ukandamizaji, unyonyaji na ubaguzi
waliokuwa wanafanyiwa Zanzibari Wazawa katika kupata huduma ikiwepo elimu.
Akizungumza,
Jumamosi, Januari 12, 2013, wakati anazindua Shule ya Sekondari ya Mlimani-Matemwe,
Mkoa wa Kaskazini, kwenye pwani ya kaskazini ya Kisiwa cha Unguja, Rais Kikwete amesema
kuwa inashangaza sana kuwa baadhi ya watu wanaweza kuendelea kuyabeza Mapinduzi ya
Zanzibar wakati yameleta faida kubwa na nyingi kwa wananchi na wanazijua. “Sote tunatambua
sababu kubwa ya Chama cha ASP kufanya Mapinduzi ya mwaka 1964 ilikuwa ni kuondosha
ukandamizaji, unyonyaji na ubaguzi waliokuwa wanafanyiwa Wazanzibari wazawa katika
kupata huduma muhimu ikiwepo elimu. Idadi ya skuli ilikuwa ndogo sana na kwa makusudi
wazawa wenzetu chache ndio walibahati kupata elimu,” amesema Rais Kikwete na kuongeza:
“Baada
ya Mapinduzi, skuli nyingi zilijengwa na vijana wengi zaidi wanapata elimu. Kazi hiyo
inaendelea kama tunavyoshuhudia leo.” Rais Kikwete aliongeza: “Zanzibar na Pemba zilikuwa
na shule tatu tu za sekondari za Serikali kabla ya Mapinduzi ya mwaka 1964 – moja
ilikuwa Pemba ikiitwa Saidi Abdallah Secondary School na mbili zilikuwa Zanzibar,
basi. Zilizobakia zilikuwa shule za sekondari za dini. Leo tu, tunafungua kwa mpigo
shule 21 za sekondari mpya. Moja hii ambayo ni moja ya shule 13 ambazo ujenzi wake
umekamilika. Nyingine nane zikiwa zinajengwa ikiwa ni pamoja na chuo kipya cha ualimu
cha Benjamin William Mkapa.”
Uzinduzi wa shule hiyo yenye majengo na huduma
za kisasa ikiwa ni pamoja na maabara za masomo ya fikizia, kemia, biolojia na kompyuta
ni sehemu ya Sherehe za Miaka 49 ya Mapinduzi ya Zanzibar, ambayo sherehe zake zimefanyika
leo kwenye Uwanja wa Amaan, mjini Zanzibar, na kuhudhuriwa na Rais kikwete. Shule
hiyo iliyogharimu kiasi cha Sh. Bilioni 1.8 mpaka sasa ni moja ya shule 19 za sekondari
zinazojengwa Tanzania Visiwani chini ya Mradi wa Uimarishaji wa Elimu ya Lazima (ZABEIP)
miaka mitano unaogharimiwa kwa pamoja na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Benki
ya Dunia.
Serikali ya Mapinduzi (SMZ) inatoa dola za Marekani milioni sita
na Benki ya Dunia dola za Marekani milioni 42 ikiwa ni mkopo wenye masharti nafuu
na mradi wenyewe ulioanza kutekelezwa Julai 2008 unafikia mwisho wake Juni mwaka huu,
2013. Chini ya mradi huo, zinajengwa shule 10 za sekondari (kidato cha kwanza hadi
cha sita) katika kila wilaya za Tanzania Visiwani, zinajengwa shule tisa za sekondari
(kidato cha kwanza hadi cha nne) – tano Unguja na nne kisiwani Pemba, kinajengwa chuo
kipya cha ualimu cha William Benjamin Mkapa Kisiwani Pemba na shule sita zinafanyiwa
matengenezo makubwa.
Mradi huo pia ni matokeo ya mazungumzo kati ya Rais Kikwete
na uongozi wa Benki ya Dunia wakati alipofanya ziara yake ya kwanza Marekani mwaka
2006 baada ya kuwa amekuwa Rais wa Tanzania ambako aliushawishi uongozi wa Benki hiyo
kukubali kutoa fedha za kugharimia mradi huo mkubwa zaidi kuliko mwingine wowote kufanywa
na Serikali katika historia ya Zanzibar. Aidha, kutekelezwa kwa mradi huo ni utekelezaji
wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi (CCM) kwa Uchaguzi Mkuu wa 2010 ambayo
iliiagiza Serikali ya Mapinduzi kujenga shule za kisasa za sekondari 21 katika wilaya
zote za Unguja na Pemba.
Chini ya Mradi wa ZABEIP, tayari shule za sekondari
13 zimekamilika kujengwa na ujenzi wa shule sita zilizobakia pamoja na Chuo cha Ualimu
cha Benjamin William Mkapa Kisiwani Pemba unaendelea. Na ili kufikisha idadi ya shule
21 za sekondari kama inavyoelekeza Ilani ya CCM, ujenzi wa shule nyingine mbili zilizosalia
unaendelea katika eneo la Mkanyageni Kisiwani Pemba na Kiblateni Kisiwani Unguja kwa
gharama ya pamoja ya Serikali ya Mapinduzi na Benki ya Kiarabu ya Maendeleo (BADEA).
Shule
ya Mlimani-Matemwe yenye huduma kamili za elimu na ambayo ni sekondari ya kidato cha
kwanza hadi cha nne, ilianza kupokea wanafunzi Septemba mwaka jana kwa vidato vya
kwanza na tatu. Wanafunzi 231 ndiyo walianzisha shule hiyo ya kutwa na yenye hadhi
ya wilaya ikiwa na wavulana 145 na wasichana 86. Shule hiyo ina walimu tisa wakiwemo
wawili wa kujitolea kutoka Nigeria. Sherehe hizo za uzinduzi wa shule hiyo zilizohudhuriwa
na viongozi wa SMZ akiwamo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mheshimiwa Balozi Seif
Idi imehudhuriwa na mamia ya wakazi wa eneo la Mlimani-Matemwe.