Mafundisho Jamii ya Kanisa yanagusa undani wa maisha na utume wa Kanisa katika huduma
Kardinali Peter Turkson, Rais wa Baraza la Kipapa la haki na amani, hivi karibuni
ameshiriki katika Kongamano la Kimataifa lililoandaliwa na Baraza la Maaskofu Katoliki
Gabon kuhusu masuala ya haki na amani, mintarafu Mafundisho Jamii ya Kanisa. Anasema,
Kanisa limeendelea kuwa mstari wa mbele katika kuhamasisha, kufundisha na kutetea
haki na amani, kama sehemu ya mchakato wa utume na maisha yake hapa duniani.
Kwa
hakika, Kanisa limekuwa ni mwanga wa mataifa kuhusiana na masuala ya haki na amani
katika masuala yanayogusa uchumi na haki jamii. Anasema, Mafundisho Jamii ya Kanisa
yanapata chimbuko lake katika Maandiko Matakatifu na kufafanuliwa kwa kina katika
maisha na utume wa Yesu; dhamana inayoendelezwa na Mama Kanisa, sehemu mbali mbali
za dunia. Ndiyo maana Kanisa limekuwa ni mdau wa pekee katika kuwahudumia na kuwatetea
wakimbizi, wahamiaji, wagonjwa, wasafiri; watoto yatima, maskini na wote wanaosukumizwa
pembezoni mwa Jamii kutokana na hali yao ya maisha.
Dhamana hii inatekelezwa
na Mama Kanisa kwa njia ya Mashirika mbali mbali ya Kitawa na Kazi za Kimissionari,
kama kielelezo cha mshikamano wa upendo unaojionesha katika Nyaraka mbali mbali za
Kanisa; na Muhtasari wake unapatikana katika Mafundisho Jamii ya Kanisa, ambayo wengine
wanayaita Biblia ya Waamini Walei, katika mchakato wa kuyatakatifuza malimwengu. Ni
nyaraka zilizotolewa kuanzia kwa Papa Leo wa Kumi na tatu hadi wakati huu, Baba Mtakatifu
Benedikto wa kumi na sita katika waraka wake wa kichungaji, Upendo katika Ukweli,
uliotolewa kunako mwaka 2007.
Kardinali Turkson anasema kwamba, chimbuko na
historia ya Mafundisho Jamii ya Kanisa ni: utu na heshima ya mwanadamu; haki, amani,
ustawi na maendeleo ya mwanadamu kiroho na kimwili. Mafundisho Jamii ya Kanisa ni
jibu makini kutokana na mahangaiko ya mwanadamu wakati wa Mapinduzi ya Viwanda Barani
Ulaya na madhara yake yakajionesha katika maisha ya watu waliojikuta wakinyanyasika
na kudhulumiwa, kiasi kwamba, haki zao msingi ziliwekwa rehani.
Mfumo wa uchumi
wa kikomunisti na Kibepari, ukaibua pia changamoto mbali mbali, kiasi hata cha kujikuta
dunia imegawanyika katika makundi: Nchi zilizozoendelea, nchi zinazoendelea na nchi
za dunia ya tatu. Huko ndiko zinakopatikana nchi zilizoko Afrika na Asia, ambazo pia
zilionja makucha ya utawala wa kikoloni. Kuanguka kwa Ukuta wa Berlini na kuhitimishwa
kwa vita baridi kati ya Marekani na Russia; na matokeo yake yakawa ni mageuzi makubwa
katika: uchumi, siasa na Jamii.
Kwa sasa Ulimwengu wa utandawazi unashuhudia
mabadiliko makubwa ya sayansi na teknolojia; kukwama kwa juhudi za maendeleo pamoja
na athari za myumbo wa uchumi kimataifa; athari za mabadiliko ya tabia nchi bila kusahau
kumong'onyoka kwa maadili na utu wema. Zote hizi ni changamoto zinazofanyiwa kazi
na Mama Kanisa katika Mafundisho Jamii, kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa binadamu
na maendeleo yake: kiroho na kimwili; utu na heshima yake, kwani ameumbwa kwa sura
na mfano wa Mungu. Lengo la Mafundisho Jamii ya Kanisa ni kujenga mji wa Mungu hapa
duniani, kwa kusimama kidete kulinda na kudumisha: upendo, haki, amani na mafao ya
wengi na wala si kwa ajili ya kikundi cha watu wachache ndani ya Jamii.