Ubatizo wa Yesu ni kielelezo cha upendo wa Mungu kwa mwanadamu unaojionesha katika
Fumbo la Umwilisho na Pasaka
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita wakati wa Sala ya Malaika wa Bwana, Kwenye
Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, hapo tarehe 13 Januari 2013,
amesema kwamba, Shereha za Ubatizo wa Bwana, zinafunga rasmi shamra shamra za maadhimisho
ya Kipindi cha Noeli, kilichotoa mwanga unaofukuza giza la dhambi na ujinga. Kanisa
katika Sherehe za Ubatizo wa Bwana linamtafakari Yesu wana wa Bikira Maria, ambaye
Kanisa lilifanya tafakari ya kina kuhusu Fumbo la Umwilisho wakati wa Siku kuu ya
Noeli.
Katika Siku hii, Kanisa linakutana na Yesu akiwa mtu zima, akipokea
Ubatizo wa Toba Mtoni Yordani na kwa njia ya Ubatizo wake, akayatakatifuza maji yote
duniani, kama Liturujia ya Mashariki inavyokazia.
Baba Mtakatifu anabainisha
kwamba, Yesu Kristo alikwenda kupata Ubatizo wa Toba, ni kielelezo cha mwanzo wa utume
wa maisha yake ya hadhara, yanayojionesha kwa namna ya pekee kabisa katika Fumbo la
Umwilisho, pale Mwenyezi Mungu alipoamua kujinyenyekesha na kushuka kutoka mbinguni,
katika mambo yote akawa sawa na binadamu isipokuwa hakutenda dhambi. Kwa ufupi kabisa,
hiki ni kielelezo cha upendo wa Mungu kwa mwanadamu unaojionesha kwa namna ya ajabu
kwa njia ya uwepo wa Yesu Kristo miongoni mwa watu. Yesu alipokea Ubatizo wa Toba
kama kielelezo cha mshikamano na binadamu, ndiyo maana Yohane alipomwona anakuja,
akawaambia wanafunzi wake, tazameni Mwanakondoo wa Mungu anayeondoa dhambi za dunia.
Yesu alipobatizwa, mbingu na nchi zilifunguka na Roho Mtakatifu akamshukia
kwa mfano wa Njiwa na sauti kutoka mbinguni ikasikika ikisema, “Huyu ndiye mwanangu
mpendwa wangu ninayependwa naye, msikieni Yeye”. Yesu ni kielelezo cha hali ya juu
kabisa cha utekelezaji wa utashi na mapenzi ya Mungu katika maisha yake, yanayoonesha
upendo unaofikia hitimisho lake katika mateso, kifo na ufufuko wa Kristo. Yesu ni
kielelezo cha maisha ya mtu mpya, ambaye katika sura ya ulimwengu huu anaamua kuchagua
njia ya unyenyekevu na uwajibikaji makini, kiasi hata cha kuyamimina maisha yake,
ili kusimama kidete kutangaza Ukweli na Haki.
Baba Mtakatifu anasema, kuwa
Mkristo ni changamoto ya kujitahidi kuishi katika mtazamo huu, kwa kutambua kwamba,
kwa njia ya Ubatizo, mwamini amezaliwa upya kwa Maji na Roho Mtakatifu na kwamba,
Kanisa limepewa dhamana ya kuwakirimia watu upya wa maisha, changamoto ya kukataa
dhambi na nafasi zake, ili kushikamana na Kristo; ni mwaliko wa kumkataa Shetani kwa
kumtambua Kristo kuwa ni Nafsi ya Pili katika Fumbo la Utatu Mtakatifu.
Baba
Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, anasema, katika Maadhimisho ya Sherehe ya Ubatizo
wa Bwana, amebahatika kuwabatiza watoto ishirini waliokuwa na umri kati ya miezi mitatu
hadi minne. Kwa namna ya pekee, ametuma salam na matashi mema kwa watoto wote waliozaliwa
katika kipindi hiki na anawaalika wakristo kutambua dhamana waliyojitwalia wakati
walipopokea sakramenti ya Ubatizo, inayowawezesha kuanza hija ya maisha ya uzima wa
milele. Katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, kila mwamini anachangamotishwa kutambua
ile zawadi ya Ubatizo, inayoonesha upendo wa Mungu na kwamba, kwa njia hii waamini
wanakuwa kweli ni watoto wa Mungu
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita,
alikumbusha kwamba, Jumapili, tarehe 13 Januari, 2013, Mama Kanisa ameadhimisha Siku
ya 99 ya wakimbizi na wahamiaji duniani, iliyoongozwa na kauli mbiu “Mahujaji wa Imani
na Matumaini”. Kwani wale wanaohama katika nchi zao wanakuwa na imani na matumaini
kwa ajili ya kesho iliyo bora zaidi; wanafanya hivyo kwa vile wana mtumainia Mwenyezi
Mungu anayeongoza mapito ya maisha yao, kama alivyofanya kwa Mzee Ibrahim, Baba wa
Imani. Wahamiaji na wakimbizi ni watu wenye imani na matumaini thabiti.
Baba
Mtakatifu amezikumbuka Jumuiya za Wahamiaji wa Kikatoliki walioko mjini Roma na kuwaweka
wote chini ya ulinzi na usimamizi wa Watakatifu Frances Cabrini na Mwenyeheri Giovanni
Battista Scalabrini.