2013-01-14 09:28:13

Katiba Mpya ya Tanzania izingatie: haki msingi za binadamu, uhuru wa kuabudu na uhai wa binadamu dhidi ya utamaduni wa kifo!


Askofu Michael Msonganzila wa Jimbo Katoliki Musoma, Tanzania anasema kwamba, kwa miaka kadhaa, watanzania wameonesha hitaji la kuwa na Katiba Mpya, itakayokidhi mahitaji ya watanzania kwa sasa. Hitaji hili linadai mabadiliko ya kina miongoni mwa viongozi wa Serikali, viongozi wa vyama vya kisiasa, viongozi wa kidini na wananchi kwa ujumla wao. Kanisa Katoliki limeendelea kuwa mstari wa mbele kuwahamasisha Wakatoliki kushiriki kikamilifu katika mchakato wa kutoa maoni yao kuhusu Katiba Mpya ya Tanzania. RealAudioMP3
Mambo ya kuzingatia kwanza kabisa ni kuhakikisha kwamba, haki msingi za binadamu na uhuru wa watu unaheshimiwa, sanjari na uhuru wa kidini, ambao ni mhimili wa haki msingi za binadamu. Kwa vile Katiba ya nchi ni Sheria Mama, kamwe isibebe wala kukumbatia udini unaoweza kuwa ni shinikizo kutoka kwa makundi ya kidini nchini Tanzania.
Sharia, Mahakama ya Kadhi na Mahakimu wa Makahaka ya Kadhi ni mambo ambayo hayapaswi kuingizwa kwenye Katiba ya Tanzania, kwani Tanzania kimsingi ni nchi ambayo haina dini na wala Serikali yake haina dini, lakini watu wake wa dini na imani zao zinazopaswa kuheshimiwa na kulindwa Kikatiba. Shinikizo kutoka katika makundi ya kidini linaweza kuvuruga misingi ya haki, amani, utulivu na mshikamano wa kitaifa. Imani zisipingane na haki msingi za binadamu. Kama kuna kundi linalotaka uwapo wa Mahakama ya Kadhi, basi ijitegemee na wala isiwe ni sehemu ya shughuli za Serikali.
Kanisa Katoliki lina Mahakama yake, lakini hiki ni chombo huru kinachojitegemea na hakihitaji ridhaa ya ya Serikali ili kutekeleza majukumu yake. Katiba Mpya itetee na kulinda maisha ya mtu tangu pale anapotungwa mimba hadi mauti ya kawaida inapomfika, kamwe Katiba isikumbatie utamaduni wa kifo. Kuna haja pia ya kufuta adhabu ya kifo!







All the contents on this site are copyrighted ©.