2013-01-14 10:08:11

Kanisa Katoliki linapania kuendeleza majadiliano ya kidini kwa njia ya ushuhuda wa maisha!


Kardinali Jean Louis Tauran, Rais wa Baraza la Kipapa la Majadiliano ya Kidini anasema kuna haja ya kuendelea kujenga na kuimaraisha utamaduni wa majadiliano ya kidini kuhusu masuala ya uwepo na umuhimu wa Mwenyezi Mungu katika maisha ya watu, kutokana na ukweli kwamba, watu wengi wanamezwa na malimwengu, kiasi cha kushindwa kutambua uwepo wa Mungu kati yao. RealAudioMP3
Mwaka 2012 umekuwa na matukio muhimu sana katika mchakato wa kudumisha majadiliano ya kidini kati ya Wakristo na Waamini wa Dini ya Kiislam, mintarafu Mwongozo wa Baraza hili kama unavyobainishwa na Waraka wa Kristo Mchungaji Mwema. Lengo ni kuendeleza majadiliano ya kidini kwa njia mbali mbali, lakini zaidi katika ushuhuda wa maisha, daima wakitafuta kutambua na kuimarisha tunu msingi za maisha ya kiroho, hasa wakati huu watu wanapoonesha kiu ya kutaka kumfahamu Mungu kwa undani zaidi.
Majadiliano ya kidini na Waamini wa Dini ya Kiislam yanaendelea kupewa kipaumbele cha pekee kama njia ya kutaka kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani, usalama na utulivu, daima wakiwa wanatafuta mafao ya wengi ndani ya Jamii. Sharia ya dini ya Kiislam anasema Kardinali Tauran imekuwa ni chanzo cha migogoro ya kidini sehemu mbali mbali za dunia na kikwazo cha majadiliano ya kidini katika nchi kama Pakistan na Nigeria ambako watu wasiokuwa na hatia wanaendelea kupoteza maisha yao kutokana na chuki na uhasama wa kidini. Kwa bahati mbaya misimamo mikali ya kiimani inaweza kupelekea watu wengi wakakosa uelewa na maana sahihi na tunu bora za maisha ya kiroho zinazofumbatwa katika dini ya Kiislam.
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, wakati wa hija yake ya kichungaji nchini Lebanon kama sehemu ya kuzindua matunda ya Sinodi ya Maaskofu Katoliki Mashariki ya kati, alibainisha kwa kina na mapana utashi wa Kanisa Katoliki kuendeleza mchakato wa majadiliano ya kidini na waamini wa dini ya Kiislam; majadiliano yanayojikita katika heshima na ukweli; toba, wongofu wa ndani pamoja na dhamana ya Mama Kanisa kutangaza Injili ya Kristo hadi miisho ya dunia, kama alivyobainisha wakati wa hotuba yake ya matashi na kheri ya Siku kuu ya Noeli kwa Mwaka 2012.
Kanisa Katoliki linaendelea kushirikiana na waamini wenye mapenzi mema katika kukuza na kudumisha majadiliano ya kidini sehemu mbali mbali za dunia, kama inavyojionesha kwa kuwa ni mwanachama mwanzilishi wa Kituo cha KImataifa cha Majadiliano ya Kidini na Kitamaduni, kilichofunguliwa mjini Vienna, hapo tarehe 26 Novemba 2012. Ni kituo muafaka cha majadiliano katika ukweli, uwazi, heshima na kuthaminiana kama binadamu walioumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.
Kardinali Tauran anasema mwaka 2012 umekuwa ni mwaka wenye matukio mbali mbali yanayoonesha umuhimu wa kuendeleza majadiliano ya kidini, ili kujenga misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa dhati; waamini wa dini zote wanapaswa kushirikiana kwa dhati kwa ajili ya mafao ya wengi, hakuna maendeleo ya kweli pasi na amani. Dini zichangie katika ujenzi wa haki, amani, upendo na maelewano.
Maadhimisho ya Mwaka wa Imani ni fursa kwa Wakristo kufahamu kwa kina imani yao kuhusu Yesu Kristo Mkombozi wa dunia, kwa kuwashirikisha wengine ile furaha ya kukutana na Kristo katika maisha na kweli za Kiinjili. Hata katika umaskini wake, Kanisa linapenda kutoa mwaliko wa pekee kwa Watoto wake, kutolea ushuhuda makini wa Imani yao kwa Kristo na Kanisa lake; kwa kuwahakikishia wote wanaowashangaa kwamba, kwa hakika wamekutana na Yesu Kristo Mwana wa Mungu aliye hai.








All the contents on this site are copyrighted ©.