Tafakari Zaburi 128 (127): Hii ni zaburi ya hekima, watunzi wa kundi hili kwa njia
ya kurudiarudia ujumbe na maonyo wanataka kugongomelea katika akili za wasilizaji
wao hofu ya Mungu kwani yenyewe inamzawadia mtu ustawi na furaha. Zaburi hii inazungumza
na mmoja ambaye ni mwanafamilia na mkulima. Anaambiwa juu ya baraka tatu ambazo Mungu
anamnyeshea juu yake kama ataenda kulingana na imani yake: atafurahia amani kamilifu
kwa kupata mavuno ya kutosha ya kazi yake, atapata watoto wengi na ustawi wa Jiji
la Yerusalemu akiwa na maisha marefu.
Mababa wa Sinodi ya Afrika, walipenda
kulieleza Kanisa la Bara letu, kuwa ni ‘Familia.’ Mzaburi anatusihi kuwa na familia
yenye amani, twapaswa kuwa wachamungu na kupenda kufanyakazi. Hii ni tafakari nzuri
kwa Kanisa kama familia ya Mungu inayowajibika.
Neno hofu, kwa Kiebranina Yare,
linatumika mara nyingi katika Maandiko Matakatifu. Mbele ya Mungu, wachamungu walitambua
kwamba wako mbali sana na Muumba wao. Kwao Mungu ni wa tofauti kabisa. Kwa mtazamo
huu, hofu ni jambo jema. Kutokana na Mungu kuwa kwao fumbo; ndiko kulikozaa heshima
na uchaji kwa Yeye aliyetofauti kabisa. Hofu hii haisababishi uchungu wa moyo, yanayoambatana
na hasira. Ni kinyume chake, ni chemchemi ya Baraka na heri: Heri mtu amwogopaye Bwana,
aendaye katika njia yake.
Taabu ya mikono yako hakika utaila, utakuwa na heri,
na kwako kwema. Kwa mkulima yeyote wa eneo ambalo ni jangwa na lenye mvua haba. Baraka
hii ilikuwa na maana kubwa katika maisha yake. Kwa mlengwa wa tungo hii hali ilikuwa
mbaya zaidi, licha ya ubaya wa ardhi na hali mbaya ya hewa, kulikuwapo na kunyonywa
na bughudha toka kwa wageni waliokuwa wakiwatawala. Kwa hakika kila mmoja wetu anapaswa
kuheshimu na kupenda kazi za mikono; hasa vijana. Hekima ya wahenga inatuambia ukicheza
ujanani, utalipa uzeeni. Uvivu ni kumkufuru Mungu aliyetupa ardhi na mito kwa ajili
ya ustawi wetu.
Mkeo atakuwa kama mzabibu uzaao, vyumbani mwa nyumba yako.
Hii si kauli ngeni kwa watu wa Mashariki. Ni desturi kwa wao kupanda mzabibu kando
ya nyumba, ili kutumia vizuri ardhi kwani ilikuwa haba, ni jangwa na majabari, na
pia kuufanya mti huo upate jua. Ulitumika kupendezesha mazingira ya nyumba, lakini
pia kuulinda dhidi ya wezi. Hivyo, mzabibu huu mzuri, wenye matunda mengi, ulikuwa
ni nembo ya akina mama wengi wa Mashariki. Kuwa na watoto wengi ni baraka kubwa kwa
taifa la Mungu (soma Mwa 15:5). Usasa usiwe kikwazo kwa sisi kukacha kuzaa, na kuwafanya
wanyama: mbwa, paka kuwa ndio watoto wetu!
Wanao kama miche ya mizeituni,
wakiizunguka meza yako: huu ni umithilisho mzuri sana; kuna mti wa mzabibu mkongwe
na umeanza kupukutika, umezungukwa na miche mingi mizuri na yenye nguvu, ambayo imechipuka
toka katika shina hili kongwe. Miche hii yaonekana ikilitegemeza, kulilinda na kulikumbatia
shinda kongwe. Kwa hakika hata mavuno hayajapungua licha ya ukongwe wa shina msingi,
kutokana na uzao wa miche hii mipya. Ndivyo mtunzi wetu anavyomithilisha watoto wema
na wenye upendo kwa baba yao mchamungu. Kila mche unachangia katika wema wa wote.
Hii ni baraka kubwa kwa mzazi yeyote yule.
Bwana akubariki toka Sayuni;
uone uheri wa Yerusalemu siku zote za maisha yako. Kuwa na ustawi ndani ya familia
yako, si mwisho wa kuwajibika kwako. Mkulima wetu anaambiwa afungue macho yake na
kuona patakatifu pake. Kwani hapo ndipo ilipo chemchemi ya heri zote alizonazo. Hata
sisi leo, mafanikio yetu yasitutenge na Kanisa, iwe ni kushiriki katika jumuiya au
katika ujenzi wa kanisa; toka Yerusalemu ndipo baraka za Mungu zinatushukia.
Kwa
hakika: Tazama, atabarikiwa hivyo, yule amchaye Bwana. Si kwa fedha au tanzanite,
lakini ya heri isiyochakachuliwa na tufani za maisha. Kwani Bwana atakuwa mlinzi wake
daima.