2013-01-10 09:19:49

Utapimlo mkali unatishia maisha ya watoto zaidi ya 200,000 nchini Sudan ya Kusini


Licha ya maboresho ya huduma ya afya ya Mama na Mtoto sehemu mbali mbali za dunia, lakini bado kuna idadi kubwa ya watoto wanaopoteza maisha yao Barani Afrika kutokana na utapiamlo wa kutisha. Hii inatokana na kuendelea kuwepo kwa ukame wa mda mrefu uliopelekea baa la njaa linalochochea pia umaskini.

Taarifa zinabainisha kwamba, kuna watoto laki mbili nchini Sudan ya Kusini wanaokabiliwa na utapimlo wa kutisha na kwamba, kila siku watoto wenye uzito mdogo wanaendelea kupata tiba kwenye Hospitali kuu ya Juba, inayotoa huduma pekee kwa watoto. Kila mwaka Jumuiya ya Kimataifa inajitahidi kuwahudumia watoto wapatao sabini elfu, lakini hali ni mbaya zaidi Sudan ya Kusini kwa idadi ya watoto wenye utapiamlo wa kutisha imefikia laki mbili. Hali ni mbaya zaidi vijijini ambako watoto wanaendelea kupoteza maisha kutokana na ugonjwa wa homa kali na Malaria.

Takwinu za Idadi ya Watu nchini Sudan ya Kusini zinaonesha kwamba, kuna jumla ya watu millioni tisa na nusu ya idadi ya wananchi wa Sudani ya Kusini ni vijana na watoto. Itakumbukwa kwamba, Sudan ya Kusini ilijipatia uhuru wake kunako Mwaka 2011 baada ya kupiga kura ya maoni, iliyoonesha kwamba, wananchi wa Sudan ya Kusini walikuwa wanataka kujitenga na Sudan Kongwe. Kwa bahati mbaya, Serikali ya Sudan ya Kusini bado iko katika mchakato wa maboresho ya miundo mbinu iliyokuwa imeharibiwa vibaya kutokana na vita ya wenyewe kwa wenyewe nchini humo.

Serikali kwa kushirikiana na wadau mbali mbali inaendelea kupambana na baa la umaskini, linaloendelea kupungua siku hadi siku, lakini tatizo la utapimlo bado ni kubwa miongoni mwa watoto kutoka Sudan ya Kusini.







All the contents on this site are copyrighted ©.