Rasilimali ya nchi ni kwa mafao ya watanzania wote na wala si kwa baadhi ya watu!
Wazee wa Tabora wameunga mkono msimamo wa miaka yote wa Serikali kwamba rasilimali
za Tanzania, ikiwamo gesiasilia iliyogunduliwa katika mikoa mitatu ya Tanzania ukiwamo
Mkoa wa Mtwara, itumike kwa manufaa ya nchi nzima na wala si kunufaisha mikoa ambako
gesiasilia hiyo inapatikana ama imegunduliwa. Aidha, wazee hao wameitaka Serikali
kuanzisha sera na utaratibu ya kutenga sehemu maalum katika hospitali zote nchini
kwa ajili ya kuhudumia wazee ambao wanapata shida kupanga foleni kwa ajili ya kupatiwa
huduma za afya.
Wazee hao pia wamepongeza msimamo wa Serikali ya Rais Kikwete
kuhakikisha kuwa hakuna ardhi ya Mtanzania yoyote inachukuliwa kwa matumizi ya umma
bila kufidiwa na Serikali. Wazee hao walieleza msimamo wao kuhusu masuala hayo wakati
walipokutana na Rais Kikwete kwa mkutano maalum uliofanyika usiku wa kuamkia leo,
Jumatano, Januari 9, 2013, katika Ikulu Ndogo ya Tabora ambako Rais Kikwete anafanya
ziara ya siku tano kukagua na kufungua miradi ya maendeleo.
Wazee hao wa CCM
wa Tabora Mjini wametoa msimamo wao kuhusu gesiasilia na rasilimali nyingine nchini
na kuhusu msimamo wa baadhi ya wakazi wa Mtwara ambao wamekuwa wanaendesha kampeni,
isiyokuwa na tija na isiyoungwa mkono na watu, kupinga gesiasilia kusafirishwa kwenda
Dar Es Salaam. Wamefanya hata maandamano kuishinikiza Serikali kubadili sera hiyo
ya kihistoria ya Tanzania.
Serikali inatumia mabilioni ya fedha kujenga bomba
la kusafirisha gesi kutoka Mtwara kwenda Dar es Salaam ambako itatumika kuzalisha
umeme kwa wingi na kumaliza tatizo la umeme sugu la sasa nchini na pia kwa matumizi
ya viwanda. Umeme utakaozalishwa kutokana na gesiasilia hiyo utaunganishwa kwenye
gridi ya taifa kwa manufaa ya mikoa yote nchini. Mbali na Mtwara, gesiasilia pia imegundulika
mikoa ya Pwani na Lindi ambako tayari gesiasilia yake inatumika kuzalisha umeme kwa
ajili ya mikoa ya Lindi na Mtwara.
Wazee hao wamemwambia Rais Kikwete kuwa
msimamo wa baadhi ya wananchi wa Mtwara, wakiongozwa na baadhi ya wanasiasa na hasa
wale wa vyama vya upinzani, unashangaza kwa sababu miaka yote tokea uhuru msimamo
wa Tanzania ni kwamba raslimali inayopatikana katika sehemu yoyote ya Tanzania itumike
kwa ajili ya nchi nzima na watu wake na siyo kwenye mikoa inakopatikana raslimali
hiyo.
“Kuhusu hili suala la msimamo wa baadhi ya wananchi wa Mtwara kuhusu
gesi, tunaamini kuwa wenzatu wa Mtwara wamepotoka na kughafilika kwa sababu msimamo
wetu wa kihistoria katika nchi hii ni kwamba raslimali za nchi yetu zitumike kwa ajili
ya nchi nzima na wananchi wote wa Tanzania,” wamesema wazee hao katika risala yao
kwa Rais Kikwete na kuongeza: “Wenzetu hawa wa Mtwara nadhani wamedandia ajenda ambayo
hawaijui na hawakuianzisha wao kwa sababu kazi ya gesiasilia imefanywa na Chama cha
Mapinduzi (CCM) lakini wanaojaribu kuvuruga kazi hiyo ni wapinzani wa CCM.”
Rais
Kikwete aliwashukuru wazee hao wa Tabora na kuwaambia kuwa kila mtu, kila mkoa ukitaka
kubakia na rasilmali yake ni dhahiri kuwa haitakuwepo Tanzania. “tutaigawa nchi yetu
na kuibakiza vipande vipande.” Aliongeza Mheshimiwa Rais: “Baadhi yetu sisi wanasiasa
tayari tumeharibikiwa na sasa wanatafuta namna ya kujijenga upya kwa kutumia suala
la gesiasilia.” Rais Kikwete pia alikubaliana na wazo la kuanzisha sehemu maalum ya
matibabu ya wazee katika hospitali nchini. “Hili ni wazo zuri na tutaangalia jinsi
gani linavyoweza kutekelezeka.”
Wakati huo huo, Rais Jakaya Mrisho Kikwete amewaagiza viongozi nchini kuwaondoa
mara moja watu wote waliovamia misitu na vyanzo vya maji, wakiwamo waliovamia Bonde
la Mto Kilombero, Mkoani Morogoro. Kuanzia sasa viogozi wasiwaonee aibu watu wote
wanaovamia misitu ya Serikali na kuharibu vyanzo vya maji na uoto wa asili. “Viongozi
tulisimamie hili bila woga wala aibu na wala wanasiasa wenzangu msiliingilie ili kupotosha
watu. Kwenye hili, tusione haya wala aibu hata kidogo. Tuwaondoe wote na bila kuchelewa
kwa sababu kwa kufanya hivyo tunanusuru taifa letu,” ameagiza Rais Kikwete.
Rais
Kikwete alitoa maagizo hayo Alhamisi, Januari 10, 2013, wakati alipoweka jiwe la
msingi kwenye Mradi wa Uboreshaji wa Upatikanaji Maji katika Mji wa Tabora kwenye
siku ya tano na ya mwisho ya ziara yake Mkoani humo. Tokea Jumamosi iliyopita, Rais
Kikwete amekuwa katika Mkoa wa Tabora akikagua, kuweka jiwe la msingi na kuzindua
miradi mbali mbali ya maendeleo zikiwamo barabara, miradi ya maji, shule na daraja.
Akizungumza
na wananchi kwenye eneo la Bwawa la Igombe, nje ya Mji wa Tabora, Rais Kikwete amesema
kuwa viongozi wakiendelea kuruhusu uvamizi wa maeneo ya misitu na vyanzo vya maji
watakuwa wanaruhusu uangamizaji wa taifa. “Hatuwezi kukubali jambo hilo, kila mtu
ana kwao alikotokea, arudi kwao na siyo kuvamia misitu na mabonde katika maeneo mengine.
Nawataka viongozi wahakikishe hili linafanyika bila woga wala haya. Waondoeni wavamizi
wote katika mabonde, katika vyanzo vya maji na kwenye misitu.”
Rais amesema
kuwa uamuzi wake aliochukua miezi mitatu tu baada ya kuingia madarakani wa kuwahamisha
wafugaji waliokuwa wamevamia Bonde la Ihefu sasa umeanza kurudisha uhai kwenye Mto
Ruaha. “ Watu waliingiza ng’ombe 460,000 katika eneo lile na kuharibu kabisa mfumo
mzima wa Bonde lile. Tuliwaondoa na sasa angalau tunaanza kuona uhai kwenye Mto Ruaha
ambao ulikuwa umekauka kwa sababu ya chanzo chake kuvurugwa na kuharibiwa.”
Rais
amesema kuwa ni jambo la hatari kabisa kwa uhai wa binadamu kuharibu vyanzo vya maji
kwa sbabau hakuna mbadala wa maji. “Tukikosa maji tutakunywa na kutumia nini? Soda?
Unaweza kupika ugali kwa kutumia soda? Kinamama mnaweza kupika ugali kwa kutumia soda?”
Rais Kikwete amewauliza wananchi kwenye sherehe hiyo.