Tanzania imepania kupunguza uhaba wa walimu wa shule za Serikali kwa mwaka 2013
Serikali ya Tanzania itaajiri na kusambaza walimu 28,746 katika shule za msingi
na sekondari kuanzia mwezi huu wa Januari 2013, hatua ambayo itapunguza kwa zaidi
ya nusu ukosefu wa walimu katika shule za Serikali nchini. Mpaka sasa Tanzania ina
upungufu wa walimu 57,177 katika shule za Serikali, tatizo ambalo Serikali inasema
kuwa italimaliza katika miaka michache ijayo kutokana na idadi kubwa ya walimu wanaofundishwa
katika vyuo mbali mbali nchini. Rais Jakaya Mrisho Kikwete ametangaza mjini Igunga
siku ya Jumatatu, Januari 7, 2013 kuwa kati ya walimu hao watakaoajiriwa na kusambazwa
14,600 watakuwa wa shule za msingi, walimu 14,060 watakuwa wa shule za sekondari na
80 watakuwa walimu wa vyuo vya ualimu. Akihutubia maelfu ya wananchi wa mjini Igunga
kwenye Uwanja wa Barafu kwenye siku ya pili ya ziara yake ya kikazi katika Mkoa wa
Tabora, Rais Kikwete amesema kuwa mikoa yenye uhaba mkubwa zaidi wa walimu ndiyo itapewa
kipaumbele katika mgawo huo wa walimu. Mkoa wa Tabora ni moja ya mikoa yenye uhaba
mkubwa wa walimu, ikiwa na ukosefu wa walimu 2, 055 na Wilaya ya Igunga pekee ikiwa
inahitaji kiasi cha walimu 285. Hii itakuwa mara ya pili mfululizo kwa Serikali kuajiri
na kusambaza idadi kubwa ya walimu wa shule za msingi na sekondari katika jitihada
za kumaliza tatizo la ukosefu wa walimu nchini ambalo kwa namna moja linachangia matatizo
ya elimu nchini. Mwaka juzi, Serikali iliajiri na kusambaza walimu 24,621 ambao
kati yao 11,379 walikuwa wa shule za msingi, walimu 13,246 walikuwa wa shule za sekondari
na walimu 42 walikuwa ni wa vyuo vya elimu. Wakati shule za Serikali nchini zinaendelea
kukabiliwa na upungufu wa walimu, shule binafsi nchini zina ziada ya walimu, shule
za msingi zikiwa na ziada ya walimu 2, 857 na zile za sekondari zikiwa na ziada ya
walimu 459 hali inajionyesha katika matokeo mazuri ya mitihani kwa wanafunzi wa shule
hizo. Rais Kikwete amewaambia wananchi kuwa Serikali pia inakabiliana ipasavyo
na matatizo mengine yanayoikabili sekta ya elimu ikiwa ni pamoja na ukosefu wa maabara,
ukosefu wa nyumba za kutosha za walimu na ukosefu wa vitabu vya wanafunzi. Rais Kikwete
pia amezungumzia suala la huduma ya maji nchini akisema kuwa Serikali yake imeonyesha
jitihada za kukabiliana na ukosefu wa maji katika maeneo mbali mbali ya Tanzania. Kwa
upande wa Igunga, Rais Kikwete amesema kuwa kufuatia kuzinduliwa kwa Mradi wa Maji
wa Bulenya mji wa Igunga na vijiji vitatu vinavyozunguka mji huo sasa vinapata maji
kwa asilimia 70. Ameahidi kuwa asilimia 30 iliyobakia itapatiwa majawabu na mradi
wa maji kutoka Ziwa Victoria ambayo yatavutwa kwa ajili ya matumizi ya wakazi wa miji
ya Nzega, Igunga na Tabora na vijiji ambako mabomba ya mradi huo yatapitia. Wakati
huo huo, Rais Jakaya Mrisho Kikwete, Jumatatu, Januari 7, 2013, ameweka jiwe na msingi
kwenye ujenzi wa daraja kubwa na kuzindua mradi mkubwa wa maji katika Mkoa wa Tabora
ambako anafanya ziara ya kikazi ya siku nne kukagua, kuweka jiwe la msingi na kuzindua
miradi ya maendeleo. Katika tukio ambalo ni la kihistoria tokea Tanzania kupata
uhuru, Rais Kikwete ameanzisha rasmi ujenzi wa daraja kwenye Mto Mbutu, nje kidogo
tu ya mji wa Igunga, kwa kuweka jiwe la msingi la daraja ambalo litatoa huduma kwa
wakazi wa mikoa ya Tabora, Singida, Shinyanga na Simiyu. Wakati Rais akiweka jiwe
la msingi kwenye ujenzi wa Daraja hilo katika sherehe ya kufana iliyohudhuriwa na
maelfu ya wananchi wa mji wa Igunga na vijiji vya jirani, wananchi waliendelea kuvuka
Mto huo uliojaa maji kutokana na mvua zinazoendelea sasa Mkoani Tabora kwa kutumia
miguu wengi wakiwa wamebeba baiskeli, pikipiki, mifugo na mali zao nyingine vichwani
mwao kuelekea mjini Igunga kwenye masoko. Ujenzi wa Daraja la Mbutu ni utekelezaji
wa Ilani ya CCM kwa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010 na ahadi ya Mheshimiwa Rais Kikwete
wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu wa mwaka huo ambako aliahidi kuwa Serikali yake
ingejenga daraja kwenye Mto huo ambao huhamahama kutegemea wingi wa maji. Daraja
hilo litawanufaisha moja kwa moja wakazi 84,000 wa kata saba za Mkoa wa Tabora na
wakazi wa wilaya jirani za Iramba (Mkoa wa Singida), Meatu (Mkoa wa Simiyu) na Kishapu
(Mkoa wa Shinyanga) na mzungumzaji mmoja baada ya mwingine katika sherehe hizo ameelezea
ujenzi wa daraja hilo kuwa ni ukombozi mkubwa wa wananchi wa eneo hilo. Inakadiriwa
kuwa ujenzi wa daraja hilo utakamilika Novemba mwaka huu na utagharimu kiasi cha Sh.
bilioni 11.286 zilizotolewa na Serikali ya Tanzania. Rais Kikwete pia amezindua
Mradi wa Maji na Chujio la Maji la Mji wa Igunga katika kijiji cha Bulenya, nje kidogo
ya Mji huo wa Igunga. Mradi huo uliogharimu kiasi cha Sh. Bilioni 6.7 zilizotolewa
na Serikali ya Tanzania utawanufaisha wakazi wa Mji wa Igunga na vijiji vitatu vinavyozunguka
mji huo ambao wakazi wake sasa wataweza kupata maji kwa asilimia 70. Kiasi cha watu
32,600 watanufaika na maji ya mradi huo ambao sasa watakuwa wanapata lita 2,600 za
maji kwa siku badala ya lita 710 za sasa.