2013-01-09 08:31:21

Matumizi bora ya mitandao ya kijamii yalenge maboresho ya maisha ya watu katika medani mbali mbali za maisha


Imeelezwa kuwa matumizi mabaya ya teknolojia ya habari na mawasiliano inayokwenda sambamba na matumizi ya kompyuta na mitandao yake imekuwa kichocheo kikubwa cha kumong’onyoka kwa maadili na utu wema katika jamii ya watanzania hasa vijana. Vilevile matumizi hayo mabaya ya kompyuta na mitandao yake yamechangia kwa kiasi kikubwa kuongezeka kwa matukio ya wizi wa mitandao hapa nchini.
Hayo yamesemwa hivi karibuni na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Dr. Rehema Nchimbi wakati akifungua rasmi kituo cha kutolea mafunzo ya kompyuta kinachomilikiwa na Kanisa Anglikani Parishi ya Magugu iliyopo Mkoani Manyara.
Dr. Nchimbi alibainisha kwamba, dunia sasa hivi ni kama kijiji na imeunganishwa na mitandao ya kompyuta, vilevile sekta ya teknolojia ya habari na mawasiliano imepiga hatua kubwa kimaendeleo. Lakini watu wamekuwa na matumizi mabaya na matokeo yake yanaishia kuharibu misingi bora ya kijamii, kumong’onyoa maadili na hata kufanyia wizi wa taarifa, fedha na wizi mwingine kupitia mitandao ya kompyuta.
Akiongea na viongozi wa Kanisa hilo na waumini waliojitokeza kwenye hafla hiyo ya ufunguzi, Dr. Nchimbi alitahadharisha kwamba, kituo hiko ni cha Kanisa hivyo uendeshaji wake na falsafa ya kituo hiki uzingatie maadili mema na uwajibikaji ili kituo kikawajenge wote watakaopita hapo kujifunza kwa nidhamu na uwajibikaji mkubwa zaidi.
Mafunzo ya kituo hiko yazingatie falsafa ya kuwaandaa wanafunzi wake katika hali ya usalama kimaadili ili wawe watendaji wenye maadili ambao kupitia wao na elimu watakayoipata basi Taifa liweze kupiga hatua kwenye sekta nyingine kama uchumi, kilimo mifugo na maendeleo endelevu ya watu.
Mapema akitoa taarifa ya mradi huo, Katibu wa Kanisa hilo Bwana Dismas Charles alisema kuwa jengo wanalotumia kwa mafuzo ni mali ya Kanisa lakini ukarabati wake na samani zilizonunuliwa pamoja na kompyuta za kufundishia na vifaa vyake vimegharimu zaidi ya shilingi Millioni kumi. Changamoto zinazoendelea kuwakabili ni pamoja na vifaa zaidi vya kisasa vya kufundishia na vitabu vya kujisomea wanafunzi.
Akiwakilisha waumini waliofika kwenye hafla hiyo ya ufunguzi, Mkazi wa muda mrefu wa eneo hilo Bibi Selina (92) aliwausia wanajamii juu ya umuhimu wa kuwapatia elimu watoto na vijana ili hatimaye Taifa la Tanzania liweze kuwa na watumishi hodari, wachapakazi, waadilifu na wachamungu.








All the contents on this site are copyrighted ©.