2013-01-08 08:04:04

Mshikamano wa upendo na waathirika wa Ugonjwa wa Ukimwi na Matumaini ya Bara la Afrika kwa siku za usoni!


Jumuiya ya Mtakatifu Egidio yenye Makao yake Makuu mjini Roma, inaliangalia Bara la Afrika kwa matumaini makubwa na inapenda kushirikiana na wananchi Barani Afrika katika harakati za kujiletea maendeleo yao wenyewe kwa kupambana kufa na kupona na ugonjwa wa Ukimwi, ambao kwa kiasi kikubwa umekuwa ni kikwazo cha maendeleo kwa familia nyingi.

Mradi wa "The Dream" unaosimamiwa na Jumuiya ya Mtakatifu Egidio Barani Afrika kwa ajili ya kusaidia mapambano dhidi ya maambukizi ya ugonjwa wa Ukimwi na utapiamlo miongoni mwa watoto, ulioanzishwa kunako mwaka 2002 unaendelea kuonesha mafanikio makubwa kwa kudhibiti maambukizi ya virusi vya ugonjwa wa Ukimwi kutoka kwa Mamamjamzito kwenda kwa mtoto.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, katika maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani kwa Mwaka 2012, aliiomba Jumuiya ya Kimataifa, kuonesha mshikamano wa dhati na waathirika wa Ukimwi duniani, lakini zaidi katika nchi zinazoendelea. Uwe ni mkakati unaopania kupunguza maambukizi ya ugonjwa wa Ukimwi kutoka kwa Mamamjamzito kwenda kwa mtoto, jambo ambalo linawezekana, ikiwa kama watu wataonesha mshikamano wa upendo.

Kwa mara ya kwanza mradi wa DREAM ulianza kufanyiwa majaribio nchini Msumbiji na sasa mradi huu umeenea nchini: Angola, Cameroon, Guinea Bissau, Kenya, Malawi, Nigeria, DRC na Tanzania. Ni mradi ambao umeleta mabadiliko makubwa sana miongoni mwa wagonjwa wa Ukimwi katika nchi hizi. Wanawake wamefaidika zaidi kwani wamekuwa wakihusishwa moja kwa moja katika kuhangaikia hatima ya maisha yao wenyewe pamoja na watoto wao, ili kuwajengea matumaini ya kesho iliyo bora zaidi.

Kutokana na changamoto mbali mbali zinazowakabili waathirika wa ugonjwa wa Ukimwi, kunako mwaka 2005, nchini Msumbiji, wanawake waliokuwa wameathirika kwa ugonjwa wa Ukimwi, walianzisha Chama cha Wanawake Wenye Ndoto ya Matumaini Mapya. Mama Artemisa Chiziane ni kati ya waasisi wa ndoto hii nchini Msumbiji. Ni Chama ambacho kimekuwa mstari wa mbele kutoa ushauri nasaha kwa waathirika wa ugonjwa wa Ukimwi, pamoja na kuwasaidia kukabiliana na changamoto mbali mbali za maisha ya kifamilia.

Mama Chiziane anasema kwamba, Mradi wa DREAM unajikita hasa zaidi katika kudhibiti, kuzuia na kutoa tiba kwa wagonjwa wa Ukimwi, kwa kuzingatia utu na heshima ya mwanadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Lengo ni kuunganisha harakati za kuzuia maambukizi ya ugonjwa wa Ukimwi pamoja na kutoa tiba kwa kuwapatia waathirika vidonge vya kurefusha maisha. Haitoshi tu kudhibiti, bali, kusaidia juhudi za kuokoa maisha ya watu yanayoendelea kupukutika kutokana na ugonjwa wa Ukimwi.

Kwa wanawake wajawazito, mradi unapania pamoja na mambo mengine, kuhakikisha kwamba, wanatokomeza maambukizi ya virusi vya Ukimwi kutoka kwa Mama kwenda kwa mtoto. Ni matumaini ya mradi wa DREAM kwamba, baada ya miaka michache ijayo, hata Barani Afrika, kunaweza kuwepo kizazi cha watoto wasioathirika kwa virusi vya Ukimwi.

Kutokana na ushirikiano mzuri na wadau mbali mbali katika mradi huu, watoto zaidi ya elfu kumi nchini Msumbiji wamezaliwa pasi ya kuwa na virusi vya Ukimwi. Ndoto hii inawezekana kuwahusisha wanawake wengi zaidi, kwa kuwapatia dawa za kurefusha maisha.

Hizi ni juhudi ambazo zinapaswa kuungwa mkono pia na Serikali anasema Mama Artemisa Chiziane, ili kutoa matumaini kwa wanawake wengi zaidi, hasa wale wanaoishi vijijini. Huko ni vigumu zaidi kupata dawa za kurefusha maisha na matokeo yake, watu wengi bado wanaendeleza imani za kishirikina, mila na desturi ambazo zimepitwa na wakati.







All the contents on this site are copyrighted ©.