2013-01-07 11:46:08

Mzee Mdiba anaendelea kupata nafuu!


Afya ya Mzee Nelson Mandela, Rais mstaafu wa Afrika ya Kusini, inaendelea kuimarika baada ya kulazwa kutokana na kusumbuliwa na ugonjwa wa mapafu na baadaye kupasuliwa ili kuondoa mawe yaliyokuwa kwenye figo zake, Kwa takribani majuma matatu, Mzee Mandela alilazwa Hopsitalini na kuruhusiwa kurudi nyumbani hapo tarehe 26 Desemba 2012.

Taarifa ya Rais Jacob Zuma wa Afrika ya kusini, iliyotolewa Jumapili tarehe 6 Januari 2013 inabainisha kwamba, afya ya Mzee Madiba inazidi kuimarika na anaendelea kupata matibabu akiwa nyumbani kwake nje kidogo ya Jiji la Johanesburg. Pole pole Mzee Madiba anaanza kurudia katika hali yake ya kawaida. Rais Zuma anamhakikishia Mzee Madiba kwamba wananchi wa Afrika ya Kusini na watu wenye mapenzi mema kutoka sehemu mbali mbali za dunia wanampenda na wanaendelea kumsindikiza kwa sala, dua na maombi yao.

Wananchi wengi ndani na nje ya Afrika ya Kusini, walianza kuingiwa na wasi wasi kuhusu afya ya Mzee Madiba sanjari na umri wake kuendelea kuwa mkubwa. Itakumbukwa kwamba, Mzee Nelson Mandela ana umri wa miaka 94, si haba. Mzee Mandela alikaa kizuizini kwa kipindi cha miaka 27 wakati wa utawala wa Ubaguzi wa rangi Afrika ya Kusini na huko akashambuliwa na ugonjwa wa Kifua kikuu. Akaachiwa huru mwaka 1990.

Kunako mwaka 1994 akachaguliwa kuongoza Afrika ya Kusini, huku akipeperusha bendera ya ushindi ya ANC. Kwa mara ya mwisho Mzee Madiba kuonekana hadharani ni wakati wa mashindano ya Kombe la Dunia kwa Mwaka 2010, wakati viwanja vya michezo Afrika ya Kusini, vilipowaka moto!







All the contents on this site are copyrighted ©.