Maaskofu jishikamanisheni na Yesu, ili muwe ni nyota angavu inayowaonesha watu ukweli
katika hija ya maisha yao hapa duniani!
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, katika Maadhimisho ya Sherehe ya Tokeo la
Bwana, Kwenye Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Jumapili, tarehe 6 Januari
2013 amewaweka wakfu Maaskofu wakuu wanne watakaoshiriki katika maisha na utume wa
Khalifa wa Mtakatifu Petro kwa ajili ya Kanisa moja linalojionesha pia katika Makanisa
mahalia.
Siku kuu ya Tokeo la Bwana ni kielelezo cha hija ya wachamungu waliojitaabisha
kwenda kumtafuta, kumwona, kumwabudu na hatimaye kumpatia zawadi zao. Ni kielelezo
cha watu wa nyakati, tamaduni na mitindo mbali mbali ya maisha, wanaofanya hija ya
kutaka kukutana na Mwenyezi Mungu katika maisha na kwa njia ya Siku kuu ya Epifania,
Mwenyezi Mungu anaonesha ukarimu wake kwa binadamu wote.
Baba Mtakatifu Benedikto
wa kumi na sita anasema, anaendelea kufuata Mapokeo yaliyoachwa na Mtangulizi wake,
Yohane Paulo wa Pili, kwa kuwaweka wakfu Maaskofu wapya wakati wa Maadhimisho ya Siku
kuu ya Tokeo la Bwana, kwani kuna uhusiano mkubwa kati ya hija ya watu wanaomwendea
Yesu na utume wa Askofu, anayepaswa kuwaonesha watu njia. Mamajusi ni kielelezo na
mfano bora wa kuigwa na Maaskofu katika kuwafundisha, kuwaongoza na kuwatakatifuza
watu waliodhaminishwa kwao na Mama Kanisa.
Mamajusi walikuwa ni wasomi, wadadisi
na wanafalsafa mahiri, daima walitamani kufahamu mambo msingi katika maisha na hasa
zaidi, kuhusu uwepo wa Mungu na kutaka kukutana naye ana kwa ana. Ni watu waliotafuta
ukweli kuhusu: Mungu, mwanadamu na ulimwengu. Katika hija ya maisha yao ya ndani inayojionesha
kwa namna ya pekee katika safari waliyoifanya kwamba, ni watu waliokuwa wanamtafuta
Mungu.
Baba Mtakatifu anasema kwamba, Askofu anapaswa kuwa ni mtu wa Mungu
anayeshughulikia mafao ya watu wake na kwa ajili ya wengine; akitoa kipaumbele cha
pekee cha uwepo wa Mungu katika huduma zake; kiasi hata cha kujitoa sadaka, kama inavyojionesha
kwa njia ya Fumbo la Msalaba. Askofu anapaswa kuwa ni mtu wa imani inayoongoza mapito
ya maisha yake hapa duniani, daima akijitahidi kujenga na kutekeleza ahadi za Ufalme
wa Mungu, zinazojionesha katika haki, ukweli na upendo. Katika mantiki hii, Askofu
anapaswa kuwa ni kiongozi wa: imani, matumaini na mapendo.
Imani ni hija ya
maisha ya ndani kumwendea Mwenyezi Mungu, inayojionesha katika kiu na hamu ya kukutana
na Mungu; ili kupata utulivu na usalama, si katika mambo ya dunia hii, bali kwa kujitoa
bila ya kujibakiza kwa ajili ya wengine. Askofu kama hujaji wa Mungu anapaswa kuwa
kweli ni mtu wa sala, daima akijiweka wazi mbele ya Mungu, akibainisha mahitaji na
furaha yake na ile ya jirani zake. Awe ni daraja la mawasiliano kati ya Mungu na binadamu
kwa njia ya Yesu Kristo, ili Mwanga wa Kristo uweze kung'aa duniani.
Baba Mtakatifu
anabainisha kwamba, Mamajusi kutoka Mashariki ya mbali walikuwa ni watu wenye ujasiri
na unyenyekevu uliokuwa unapata chimbuko lake katika imani, kiasi hata cha kujitosa
kuongozwa na nyota bila kuogopa magumu na hatari ambazo zingeweza kuwakabili katika
safari yao. Bali walionesha moyo wa ujasiri wakasonga mbele, jambo ambalo si rahisi!
Mamajusi waliongozwa na Mungu kutafuta mambo ya msingi katika maisha, bila kushinikizwa
wala kukatishwa tamaa na maneno ya watu wengine. Walijitosa kutafuta ukweli uliokuwa
na maana kubwa zaidi kuliko jambo jingine lolote lile.
Askofu anapaswa kuwa
ni mtu wa imani na mnyenyekevu, ambaye yuko tayari kushirikishana na wengine, Imani
ya Kanisa katika nyakati zote hata kama atakabiliwa na majaribu pamoja na magumu ya
maisha yanayotawala kwa nyakati hizi kwa kukumbatia yale wanayodhani kwamba ni muhimu
zaidi. Dhana ya ukanimungu inaendelea kusambaa kwa kasi ya ajabu, hii ndiyo changamoto
kubwa kwa Askofu wa leo, anayepaswa kuwa jasiri akionesha kanuni msingi za kufikiri
na kutenda na kutafuta ukweli, akitambua kwamba, ametumwa na Kristo kama Kondoo kati
ya Mbwamwitu.
Uchaji wa Mungu unamwondolea na kumkomboa mwamini kutoka katika
hofu inayoletwa na binadamu. Licha ya madhulumu kama inavyojionesha kwenye Matendo
ya Mitume, lakini bado mitume wa Yesu, waliendelea kumtangaza Yesu kuwa ni Masiha
kwa ari na moyo mkuu zaidi. Waandamizi wa Mitume wa Yesu wataendelea kukabiliana na
mateso pamoja na madhulumu wanapotekeleza dhamana na jukumu la kutangaza Injili ya
Kristo; licha ya yote haya, lazima watekeleze utume wao kwa watu wa ulimwengu mamboleo.
Dhamana
yao haiitaji kibali kutoka kwa Wakuu wa Mataifa na wala si chanzo cha vurugu, bali
wanatoa mwaliko kwa kila mtu kushiriki katika ile furaha ya ukweli unaoonesha njia.
Kristo anapaswa kuwa ni kigezo kinachowasukuma kusimama kidete kulinda na kuwashirikisha
wengine Injili, bila kusahau kwamba, watapata "mkong'oto wa nguvu" kutoka kwa wale
wanaopinga Injili ya Kristo, lakini wanapaswa kufurahi kwani wanashiriki katika mateso
ya Kristo.
Mamajusi waliongozwa na nyota hadi wakamwona Mtoto Yesu, mwanga
unaowaangazia wote wanaofika hapa duniani. Mamajusi kama mahujaji wa imani ni mwanga
angavu katika historia na wanaonesha njia ya kufuata, kama ilivyojionesha kwa Watakatifu
wa Mungu walioangaza katika usiku wa giza la dunia; wanawatumikia na kuwaongoza waamini
katika hija ya maisha yao hapa duniani, changamoto kwa waamini kung'ara kama nyota
angavu hapa duniani.
Huu ni ukweli kwa Maaskofu waliowekwa wakfu kwa ajili
ya Kanisa la Yesu, changamoto ya kujishikamanisha naye katika maisha ya Kisakramenti,
ili kuwa ni watu wenye hekima na nyota inayotangulia ili kuwaongoza na kuwaonesha
watu ukweli katika hija ya maisha yao hapa duniani.
Baba Mtakatifu Benedikto
wa kumi na sita, anahitimisha mahubiri yake kwa kuwakumbusha Maaskofu wakuu wapya
kwamba, Kanisa linawaombea ili Kristo awajaze mwanga wa imani na mapendo thabiti,
daima wakijiaabisha kumtafuta Mungu, ili kuonja mang'amuzi na uwepo wake wa karibu.
Kanisa linawaombea ili waweze kupata ujasiri na unyenyekevu wa kiimani. Bikira Maria
aliyewaonesha Mamajusi Mfalme wa Wayahudi; kama Mama mwema, awaoneshe wao pia Yesu
ili kuwasaidia na kuwaongoza watu kuona ile njia inayokwenda kwa Yesu.