2013-01-05 14:27:41

Wamissionari wa Damu Azizi ya Yesu, Vikarieti ya Tanzania wapata Wamissionari wapya wanne, tayari kutangaza matendo makuu ya Mungu!


Mheshimiwa Padre Reginald Mrosso, C.PP.S, Mkuu wa Shirika la Wamissionari wa Damu Azizi ya Yesu, Vikarieti ya Tanzania, tarehe 5 Januari 2013 amewapokea rasmi Majandokasisi wanne katika Shirika la Wamissionari wa Damu Azizi ya Yesu, katika Ibada ya Misa Takatifu iliyofanyika Miyuji, Jimbo Katoliki la Dodoma. Ifuatayo ni sehemu ya mahubiri yake pamoja na historia fupi ya maisha ya Wamissionari wapya wa Shirika la Damu Azizi ya Yesu, Tanzania.

Mambo matatu yanatuongoza katika furaha yetu ya leo. Mbele yetu wapo ndugu zetu wanne (4) ambao wanatoa maisha yao yote katika kumtumikia mungu na watu wake. kuchagua kumtumikia mungu ni kuchagua uhuru kamili. Katika somo la kwanza – Mungu anawaongoza watu wake toka utumwani babeli. Watu wanapiga kelele za furaha. ni tangazo la furaha kwa Sion. Kwamba, adui ameshindwa na Mungu wa Israeli anatawala kama Mfalme.

Somo hili linatuongoza vizuri sana siku ya leo katika kufurahi pamoja na ndugu zetu hawa pamoja na Taifa lote la Mungu. Tunaamini kabisa kuwa hawa ndugu zetu kwa hiari yao wenyewe na wakisikia mapenzi yake Mwenyezi Mungu wameamua kuchagua fungu hili lililo bora.

Hatusikii pengine kelele zao za furaha, lakini tunawaona kwa macho yetu, wakifurahi pamoja na mwokozi wao wakifurahi ukombozi kama walivyofurahi wana wa israeli. Hongereni sana wapendwa.

Mt. Gaspar katika barua yake no. 948 – anasema: pray over this and you will hear more clearly the voice of god. Anaendelea kusisitiza – no. 1294 – love your vocation and never cease yearning to perfect it. we are to give thanks to god for choosing us to serve him in some way; at the same time we say: if god were not to help me, what could i do? no. 1940.

Sisi Wanashirika wa Damu Takatifu ya Yesu – tupo katika maadhimisho ya miaka 200 ya uwepo wa Shirika letu hapa duniani. Tunaadhimisha pamoja ule ushindi mkuu ulioletwa na Mwana wa Mungu kwetu sisi wanadamu.

Somo la pili – lazungumzia tofauti ya sadaka iliyoitwa sadaka ya siku ya upatanisho na sadaka ya Kristo katika Mlima Kalvari. Sasa mji wetu wa kudumu uko mbinguni hata ikiwa tukingali bado hapa duniani, hivyo, tuwekeze katika mambo ya mbinguni.

Alipoanzisha Shirika la Wamisionari wa Damu Takatifu ya Yesu, Gaspari alichagua ibada kwa Damu Takatifu ya Yesu iwe njia pekee kwa mapadre wake ya kujitakatifuza na kushinda ubaya na utovu wa maisha ya kidini na kimaadili, hiki kilichokuwa kilele cha jitihada zake za kiroho, kitakuwa siri na alama pekee ya utakatifu wake, pamoja na ibada ya Shirika lake.

Kiini chake ni: a) kushiriki kikamilifu katika fumbo la paska lililo Fumbo la Damu ya Yesu, linaloendelea katika maisha ya kanisa na ambalo kilele chake ni sadaka ya misa; b) kuabudu damu ya Kimungu katika matoleo yake saba, damu iliyo msingi wa undugu wetu na Kristo na vilevile chemchemi ya neema zote za wokovu wetu; c) kutoa damu hiyo takatifu kwa Mungu Baba wa mbinguni ili pamoja na Yesu tuzidi kumtukuza.

“Na kwa namna hii tunatimiza kile tulichosikia katika somo hili la leo - Mungu wa amani aliyemleta tena kutoka kwa wafu mchungaji mkuu wa kondoo, kwa Damu ya Agano la milele, awafanye kuwa wakamilifu katika kila tendo jema. Ukamilifu huu utakapatikana katika kushiriki kikamilifu katika ujenzi wa taifa la mungu na katika shirika letu kwa kuishi kikamilifu kadiri ya mtindo wetu wa maisha ya Jumuiya. Barua no. 2877 inasisitiza – community life demands a certain degree of virtue and mutual compassion. Ujio wenu ni changamoto kubwa katika kuiishi hii sadaka ya Yesu Kristo aliyoitoa pale Kalvari. iliyo sadaka ya uzima na kamilifu. Maisha ya ushuhuda katika kuishi sadaka hii kama alivyofanya Mt. Gaspari uwe pia changamoto kwenu.

Mt. Ireneo – anaandika hivi; utukufu wa Mungu ni mtu aliye hai na anaongeza na uzima wa mtu ni katika kumwona Mungu. Maisha yenu yaakisi uzima wa Kimungu ili wale mtakaowahudumia waweze kuushiriki huo utukufu wa Mungu na kwa namna hiyo waupate uzima wa milele ninyi na wao.

Kanisa linaadhimisha Mwaka wa Imani. Katika Injili, leo tangazo la muda wa kutimizwa ahadi za mungu zilizoaguliwa na manabii. sasa muda huo ni kristo. Na ninyi ni washiriki wa muda huo, yaani pamoja na Kristo mnataka kujitoa kwa ajili ya kushiriki kutangaza huo Mwaka wa Bwana. Karibuni uwanjani.

Limetimia – kadiri ya Mwinjili Luka, Yesu ni Masiha na Nabii aliyejazwa na Roho Mtakatifu. Kutimilizwa kunadokeza kutekelezwa kwa unabii na kazi ya Roho Mtakatifu. Wakristo wanaendelea kuishi katika enzi hii ya kutimilizwa. Hivi tangazo hili la Bwana ni mwaliko wa kushiriki kikamilifu katika kutangaza imani thabiti na ya kweli kwa njia ya ushuhuda wa maisha adili na matakatifu. Ndicho imani inatudai leo – ninyi, sisi tulioko hapa na Taifa zima la Mungu.

Mwaka huu wa imani unamwalika kila mbatizwa:
i) Kukiri imani ya kweli na kuishi imani hiyo kila siku ya maisha.
ii) Kumtangaza Yesu au kuinjilisha kwa maneno na vitendo, kwa hali na mali.
iii) Kuimarisha maisha mema ya Kikristo katika familia, jnnk, parokia na pote.
iv) Kumtafuta Yesu kwa dhati na kujenga uhusiano wa karibu na wa kudumu naye
v) Kuimarisha moyo wa sala, maisha ya sakramenti na tafakari ya Neno la Mungu.
vi) Kuwa mwanga na chumvi katika kupambana na maovu aina na hasa mmong’onyoko wa maadili. Huu ndio wakati wa kuweka na kuingiza roho ya injili katika malimwengu.
vii) Kuishi maisha yanayoongozwa na tunu msingi za Injili.

Ndugu zangu wapendwa, tunaalikwa kuwa wasimamizi na wadau thabiti wa utangazaji wa habari njema. Tujisikie wadau wa utimilifu wa andiko lenyewe. kuwa tayari kusimama mbele ya ulimwengu na kusimamia mapenzi hayo ya Mungu kama alivyofanya Bwana wetu Yesu Kristo ndani ya Sinagogi.

Ulimwengu unatudai leo kusimama na kutamka wazi utayari wa kutangaza habari njema kwa mataifa. Pamoja na changamoto nyingi zilizo mbele yenu msikate tamaa na wala msiogope kwani Yesu ameshinda na tunaamini kuwa hata ninyi mtashinda.

Anatukumbusha Mt. Gaspar katika barua yake no.97 – I yearn for one thing only and that is to be entirely god’s, to wish for nothing but god, and to live only for god. Anaendelea kusema katika no. 2593 – So let us be united always in prayer; let us surrender ourselves to the ever lovable will of god, the only center of peace. Seek perfection in community life, interior life and a burning love for Jesus – no. 1819.

HISTORIA FUPI YA WAMISSIONARI WAPYA WA C.PP.S VIKARIETI YA TANZANIA
Historia ya Frt. Alex Alphonce Isengwa alizaliwa tarehe 2/6/1975 huko Pansiasi Mwanza. Alibatizwa tarehe 14/12/1975 na alipata Kipaimara tarehe 20/8/1989. Yeye ni mtoto wa sita (6) kati ya watoto saba katika familia yake. Baba yake ni Alphonce Kamila na Mama anaitwa Codra Issengwa. Alipata elimu ya msingi kati ya mwaka 1984 – 1991 katika shule za msingi Luhama na Itulabusiga huko Sengerema. Alijiunga na Seminari Ndogo ya St. Pius X makoko iliyoko Musoma kati ya mwaka 1992 – 1997.

Mwaka 1998 alirudi katika Seminari hiyohiyo kwa masomo ya kidato cha tano na sita. Alilifahamu shirika hili kwa kupitia kitabu chenye mashirika mbalimbali cha wito, akaandika maombi katika mashirika matano lakini baadaye alilichagua Shirika hili la Damu Takatifu ya Yesu.

Malezi ya kishirika: Mnamo Oktoba 2003 alianza malezi ya kwanza kwenye nyumba ya malezi ya Wamisionari wa Damu Takatifu ya Yesu iliyopo Miyuji – Dodoma. Kuanzia mwaka 2004 – 2007 ndipo safari ya miaka mitatu ya masomo ya falsafa kule Morogoro ilipoanza katika taasisi ya Wasalvatorian. Septemba 2007 hadi Julai 2008 alirudi katika nyumba ya malezi Miyuji – Dodoma kwa ajili ya malezi ya pili.

Mwaka 2008 hadi 2012 alikuwa Morogoro kwa miaka minne ya masomo ya tauhidi katika taasisi ya Wasalvatorian, ambapo tarehe 01/05/2009 alipewa huduma ya usomaji (lectorship) na mnamo tarehe 01/05/2010 alipewa huduma ya utumishi wa Altare (acolyte) yote hayo yamefanyika huko Morogoro mikononi mwa Askofu Telesphory Mkude. Alipokelewa Shirikani, rasmi na daima tarehe 05/01/2013 hapa Dodoma na Pd. Reginald Mrosso, C.PP.S Mkuu wa Shirika vikarieti ya Tanzania.

Tangu mwezi agosti 2012 amekuwa akifanya mazoezi ya uchungaji katika Parokia ya Tegeta Jimbo kuu la Dar es Salaam mpaka sasa. Anamshukuru Mungu kwa kumlinda hadi leo, vile vile anawashukuru wote kwa mang’amuzi yao na ushauri wao walimsaidia kutambua mpango wa Mungu kwenye maisha yake, kwa namna ya pekee Shirika la Damu Takatifu ya Yesu lililomlea hadi leo anazidi kuwaomba wote wazidi kumuombea ili adumu katika kutimiza mapenzi ya Mungu. Kwa maombezi ya Bikira Maria Mama wa Damu Azizi na ya Mtakatifu Gaspar del Bufalo, mwanzilishi wa Shirika wote wadumu katika kutenda mema amina.

Historia fupi ya Frt. Danford Mahumi: Alizaliwa mnamo tarehe 01/09/1979 katika Kigango cha Kinyambuli Parokia ya Chemchem ambapo kwa sasa kigango hiki kipo katika Parokia ya Mwanga, Jimbo Katoliki la Singida. Frt. Danford alibatizwa tarehe 11/04/1993 na kupata Kipaimara tarehe 24/09/1995 Katika Parokia ya Chemchem. Frt. Danford, ni mtoto wa tano kuzaliwa kati ya watoto tisa, katika familia ya Mzee Barnabas Mahumi ambaye kwa sasa ni marehemu na mama yake ni Celina Ally Mpinga.

Frt. Danford alianza masomo yake ya awali katika shule ya msingi Kinyambuli Wilaya ya Mkalama, mkoa wa Singida, mwaka 1990 na kuhitimu elimu ya msingi 1996. Baada ya kumaliza darasa la saba alichaguliwa kuendelea na masomo ya Sekondari mwaka 1997 hadi mwaka 2000 katika shule ya Dr. Salmini mjini Singida. Mwaka 2001 alijiunga na Seminari ya Mt. Yoseph iliyoko Jimbo Katoliki la Mbulu na kuhitimu masomo mwaka 2003. Alilifahamu shirika hili kupitia mapadre wa Shirika waliofika Kanisa kuu Jimbo la Singida yeye akiwa mtumishi Altareni.

Malezi ya kishirika: Mnamo mwaka 2003 alijiunga na nyumba ya Malezi Miyuji – Dodoma kwa malezi ya kwanza. Mwaka 2004 hadi mwaka 2007, alisoma shahada ya falsafa katika taasisi ya Falsafa na Taalimungu ya Wasalvatorian huko Kola – Morogoro. Mwaka 2007 hadi mwaka 2008 alirudi hapa nyumba ya Malezi Miyuji Dodoma kwa mwaka wa pili wa Malezi.

Mnamo mwaka 2008 hadi 2012 alirudi tena Morogoro kwa ajili ya masomo ya shahada ya kwanza ya taalimungu. Katika kipindi hicho, mnamo tarehe 01/05/2009 alipewa huduma ya usomaji (lectorship) huko Morogoro, na mnamo tarehe 01/05/2010 alipewa huduma ya utumishi wa Altare (acolyte) huko Morogoro na Askofu Telesphory Mkude. Alipokelewa Shirikani, rasmi na daima tarehe 05/01/2013 hapa dodoma na Pd. Reginald Mrosso, C.PP.S Vika wa vikarieti ya Tanzania.

Kuanzia Agosti 2012 hadi Januari 2013 alitumwa kufanya mwaka wa kichungaji katika parokia za Itigi na Chibumagwa katika Jimbo la Singida. Anawashukuru wote waliomwombea na wanaendelea kumwombea katika makuzi ya kiroho na kimwili. Mungu awabariki.

Historia Frt. John Greyson Msengi: Alizaliwa tarehe 22/07/1981 katika hospitali ya mkoa wa Singida. Baba yake ni Greyson Philemoni Zephania Msengi na Mama yake ni Maria Joseph Ilanda Ntandu. Yeye ni mwana mzaliwa wa pili kati ya watoto watatu, na ni mwana pekee wa kiume. Alibatizwa katika Kanisa la Kiluteri mnamo April 1993 katika mkesha wa Pasaka akiwa darasa la nne, alipokelewa rasmi katika Kanisa Katoliki, alipata sakramenti ya Ekaristi Takatifu na kupata Sakramenti ya Kipaimara katika Kanisa Katoliki.

Frt. John Greyson alipata elimu yake ya msingi katika shule ya msingi Mughanga iliyopo mjini Singida kuanzia mwaka 1990 hadi 1996. Alichaguliwa kujiunga na Don Bosco Seminari, Mafinga huko Iringa na alisoma huko kwa mwaka mmoja tu (pre-form one) akafukuzwa. Mwaka 1998 hadi mwaka 2000 alipata elimu ya sekondari, kidato cha pili hadi cha nne katika shule ya Sekondari Dr. Salmin Amour iliyopo Singida mjini. Kwa msaada wa Mungu alifaulu kwenda kidato cha tano. Mnamo mwaka 2001 hadi 2003 alijiunga na Seminari ya Mtakatifu Yosefu, Sanu Seminari iliyopo katika Jimbo Katoliki la Mbulu. Alilifahamu Shirika hili kupitia kwa Danford Mahumi na Paphael Limu, sasa ni Padre, waliokuwa wakisoma shule moja huko katika Seminari ya Sanu.

Malezi ya kishirika: mnamo Oktoba Mwaka 2003 alijiunga na nyumba ya Malezi Miyuji, Dodoma kwa malezi ya kwanza. Mwaka 2004 hadi mwaka 2007, alisoma shahada ya falsafa katika taasisi ya falsafa na taalimungu ya Wasalvatorian huko Kola, Morogoro. Mwaka 2007 hadi mwaka 2008 alirudi hapa nyumba ya malezi Miyuji Dodoma kwa mwaka wa pili wa malezi.

Mnamo mwaka 2008 hadi 2012 alirudi tena Morogoro kwa ajili ya masomo ya shahada ya kwanza ya taalimungu. Katika kipindi hicho, mnamo tarehe 01/05/2009 alipewa huduma ya usomaji (lectorship) huko Morogoro, na mnamo tarehe 01/05/2010 alipewa huduma ya utumishi wa Altare (acolyte) huko Morogoro mikononi mwa Askofu Telesphor Mkude. Alipokelewa Shirikani, rasmi na daima tarehe 05/01/2013 hapa dodoma na Pd. Reginald Mrosso, C.PP.S Vika wa vikarieti ya Tanzania.

Kuanzia Agosti 2012 hadi sasa alitumwa kufanya mwaka wa kichungaji katika Parokia ya Mtakatifu Nikolaus huko Kunduchi Mtongani katika Jimbo kuu la Dar es Salaam. Anaungana na mzaburi kwa maneno yake mazuri ya shukrani kusema: “nimrudishie Bwana nini kwa ukarimu wake wote alionitendea? Nitakipokea kikombe cha wokovu na kutangaza jina la Bwana.” (Zab 116:12-13) Anawashukuru na ninyi nyote mliopo hapa na hata wale wote wasiokuwepo hapa, waliowazima na wafu. Anawashukuru kwa kujinyima na kwa majitoleo yenu, kwa sadaka zenu na kwa misaada yenu ya hali na mali hadi yeye kufikia hatua hii kubwa na muhimu sana katika maisha yake.

Historia Frt. Raymond Deodatus Kaele alizaliwa tarehe. 27/02/1980 katika kijiji cha Kasahunga Parokiani Kibara. Baba yake anaitwa Deodatus Biseko Makongo na Mama yake anaitwa Christina Namboga Sylivester. Raymond ni mtoto wa nne katika familia yenye watoto kumi. Alibatizwa tarehe 17/08/1983 na kupata Sakramenti ya Ekaristi Takatifu tarehe 27/07/1992 na Sakramenti ya Kipaimara tarehe 9/06/1996 katika Parokia ya Kibara.

Raymond alianza darasa la kwanza mwaka 1989 na kuhitimu darasa la saba mwaka 2005. Mpaka anahitimu elimu yake ya msingi alipitia shule nne tofauti na hii ilitokana na maisha ya kikazi ya baba yake ambaye alikuwa mwalimu. mwaka 1989 alisoma Bitaraguru shule ya msingi,; 1990-1993 alikuwa Mahyoro shule ya msingi; 1993-1994 alikuwa anasoma Sikiro shule ya msingi na 1994-1995 alihitimu darasa la saba katika shule ya msingi Nakatuba, shule zote zinapatikana katika wilaya ya Bunda.

Alipitia katika Seminari ya Mt. Pius wa kumi, Makoko Seminari, iliyoko katika Jimbo la Musoma kati ya mwaka 1996 na 1999 ambapo alihitimu kidato cha nne. mwaka 2000 Julai alijiunga na shule ya sekondari ya Malangali iliyoko Mkoani iringa kwa masomo ya kidato cha tano na cha sita na hivyo akahitimu mwaka 2002.

Raymond alipata kulijua shirika kupitia vipeperushi mbalimbali, lakini kwa namna ya pekee, anamshukuru pd. mkuchu wa jimbo la morogoro kwa kumpa moyo na kumpatia anuani ya mkurugenzi wa miito hali iliyopelekea leo awepo hapa namna hii mnavyomwona.

Malezi ya kishirika: Mnamo Oktoba Mwaka 2003 alijiunga na nyumba ya malezi Miyuji Dodoma kwa malezi ya kwanza. mwaka 2004 hadi mwaka 2007, alisoma shahada ya falsafa katika taasisi ya falsafa na taalimungu ya Wasalvatorian huko kola – morogoro.mwaka 2007 hadi mwaka 2008 alirudi hapa nyumba ya malezi miyuji dodoma kwa mwaka wa pili wa malezi. mnamo mwaka 2008 hadi 2012 alirudi tena Morogoro kwa ajili ya masomo ya shahada ya kwanza ya teolojia.

Katika kipindi hicho, mnamo tarehe 01/05/2009 alipewa huduma ya usomaji (lectorship) huko Morogoro, na mnamo tarehe 01/05/2010 alipewa huduma ya utumishi wa Altare (acolyte) huko Morogoro mikononi mwa Askofu Teleesphor Mkude. Alipokelewa Shirikani, rasmi na daima tarehe 05/01/2013 hapa Dodoma na Pd. Reginald Mrosso, C.PP.S Vika wa vikarieti ya Tanzania.

Mwaka 2012 Mwezi Agosti, alianza mazoezi ya kichungaji katika Jumuiya ya Procura iliyoko Parokia ya Tegeta Jimbo kuu la Dar es Salaam. Anawashukuru wote kwa sala zenu na msaada wenu wa hali na mali katika njia hii aliyoitiwa na Mungu. anaomba sala zenu daima.








All the contents on this site are copyrighted ©.