Tume ya kukusanya maoni ya Katiba Mpya Tanzania kuanza kukusanya maoni ya katiba kutoka
katika Makundi, Changieni vyema kwa mafao ya Taifa la Tanzania
Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Jaji Joseph Warioba ametoa ufafanuzi kuhusu
hotuba ya Rais Jakaya Kikwete aliyoitoa usiku wa mwaka mpya 2013 na kuzungumzia mchakato
wa Katiba unaoendelea na kusema Rais hapaswi kulalamikiwa kwani yote aliyosema yamo
ndani ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba. Jaji Warioba alitoa ufafanuzi huo l Jumamosi,
Januari 5, 2013 katika mkutano wake na Waandishi wa Habari wakati akizungumzia tathmini
ya kazi ya kukusanya maoni binafsi ya wananchi kupitia mikutano iliyomalizika tarehe
19 Desemba mwaka 2012.
“Kuna kitu gani kipya alichosema Rais? Yote aliyosema
yapo kwenye Sheria ya Mabadiliko ya Katiba na mimi katika mikutano yangu yote nanyi
nimeyaeleza na hakuna asiyejua,” alisema Jaji Warioba ambaye ameshawahi kuwa Mwanasheria
Mkuu wa Serikali, Waziri Mkuu na Makamu wa Rais. “Rais alielezea mchakato wote kuanzia
kukusanya maoni, kuandaa rasimu, kufanyika kwa Mabaraza ya Katiba, Bunge Maalum la
Katiba na kura ya maoni…haya yote yapo kwenye sheria ambayo Wabunge waliipitisha,”
alisema Jaji Warioba wakati akijibu swali la Mwandishi wa Habari mmoja aliyetaka kujua
kauli ya Tume kuhusu maoni ya baadhi ya wanasiasa kuwa Rais aliingilia kazi za Tume.
“Hivi
ingekuwaje kama Rais angetoa salam za Mwaka Mpya bila kuzungumzia mchakato muhimu
kwa nchi kama huu wa Katiba,” alihoji Jaji Warioba. Akizungumzia mikutano ya kukusanya
maoni iliyomalizika mwezi uliopita, Jaji Warioba alisema kazi ya kukusanya maoni ilianza
tarehe 2 Julai mwaka jana na Tume yake imetembelea na kufanya mikutano 1,776 katika
mikoa yote 30 ya Tanzania Bara na Zanzibar. Kwa mujibu wa Jaji Warioba, jumla ya wananchi
1,365,337 walihudhuria mikutano hiyo na kati yao, wananchi 64,737 walitoa maoni kwa
kuzungumza katika mikutano na wengine 253,486 walitoa maoni yao kwa maandishi katika
mikutano hiyo.
Kwa mujibu wa maelezo ya Jaji Warioba, takwimu hizi hazijumuishi
maoni yanayoendelea kukusanywa na Tume yake kupitia posta, totuvi ya Tume, mitandao
ya kijamii na ujumbe mfupi wa simu za mkononi ambao hadi kufikia Ijumaa, Januari
4, 2013 jumla ya ‘sms’ 16,261. Kuhusu idadi ya wananchi waliojitokeza mikutanoni na
kutoa maoni yao, Mwenyekiti huyo alisema Tume imeridhika na idadi hiyo na kufafanua
kuwa kilichokuwa kinatafutwa na Tume ni hoja na kwamba haukuwa wakati wa kupiga kura.
“Ilikuwa
ni muhimu kufikia watu wengi iwezekanavyo na ndiyo maana tumefika kila sehemu. Lakini
tangu awali, tulishasema hatutaweza kumfikia kila mtu,” alisema na kuongeza kuwa Tume
yake imeridhika na idadi na maoni yaliyotolewa na wananchi na kutoa mfano wa Tume
ya Nyalali ambayo alisema ilipokea maoni ya wananchi 21,000 lakini Ripoti ya Tume
hiyo ilisheheni mambo muhimu kwa taifa.
Jaji Warioba alifafanua kuwa katika
awamu zote nne za mikutano ya kukusanya maoni, wananchi wametoa maoni kuhusu maeneo
yote muhimu kama utawala, haki, maadili na mamlaka yao na mengineyo. Aliongeza kuwa
mikutano ya Tume ya kukusanya maoni ililelenga kupata hoja za msingi ili Tume iweze
kuandaa Rasimu ya Katiba ambayo itawasilishwa katika mikutano ya Mabaraza ya katiba
itakayofanyika kila wilaya.
Akizungumzia hatua inayofuata, Jaji Warioba alisema
kuwa kuanzia Jumatatu, tarehe 7 Januari, 2013, Tume hiyo itaanza kukutana na makundi
mbalimbali kwa lengo la kukusanya maoni yao kuhusu Katiba Mpya. Makundi hayo ni Vyama
vya Siasa; Vyama vya Kitaaluma; Asasi za Kiraia; Taasisi za Kidini, Vyama vya Wafanyakazi,
Wakulima na Wafanyabiashara na makundi mengine mbalimbali.
Kwa mujibu wa Mwenyekiti
huyo, Tume yake imeshawasiliana na makundi hayo na imeandaa utaratibu wa kukutana
na wawakilishi wao katika ofisi za Tume na baadhi ya kumbi jijini Dar es Salaam na
Zanzibar.
Tume ya Mabadiliko ya Katiba ilianza kazi rasmi Mei 2 mwaka jana
(2012) na kazi ya kukusanya maoni kupitia mikutano imefanyakika kwa awamu nne. Awamu
ya kwanza ilifanyika kati ya Julai 2 – 30, 2012 wakati awamu ya pili ilifanyika kuanzia
tarehe 27 Agosti – 28 Septemba, 2012. Awamu ya tatu iliyofanyika kati ya terehe 8
Oktoba, 2012 na tarehe 6 Novemba, 2012 na awamu ya nne na ya mwisho ilifanyika kati
ya tarehe 19 Novemba – 19 Desemba mwaka jana (2012).