Mkakati wa kupambana na umaskini miongoni mwa watoto na vijana nchini Tanzania
Rais Jakaya Mrisho Kikwete wa Tanzania, Jumatano, Januari 2, 2013, amezindua ugawaji
wa mbuzi wa maziwa na kuku katika mpango wenye thamani ya karibu Sh. 96 milioni na
wenye lengo la kuwatoa maelfu ya watu, na hasa watoto na vijana, kwenye umasikini
uliokithiri.
Aidha, chini ya mpango huo unaolenga hasa kuwaongezea wananchi
kipato, Rais Kikwete pia amekabidhi vyandarua 250 katika jitihada za kuhakikisha kuwa
ongezeko la kipato linaweza tu kuongezewa thamani kama watu wanabakia na afya nzuri.
Rais
Kikwete amezindua ugawaji huo katika sherehe iliyofanyika kwenye Kijiji cha Msoga,
Wilaya ya Bagamoyo, Mkoa wa Pwani na kuhudhuriwa na viongozi wa Kanisa la Kiinjili
la Kilutheri Tanzania (KKKT), Kanisa la Anglikana Tanzania na Kanisa la Methodist
Tanzania, makanisa ambayo yanashirikiana na taasisi isiyokuwa ya kiserikali ya Compassion
International Tanzania (CIT) katika kuendesha miradi ya ufadhili wa kuondoa umasikini
kwa kufadhili familia na watoto waishio katika mazingira magumu.
Pamoja na
Rais kikwete katika sherehe hizo alikuwa ni Askofu Mkuu wa Kanisa la Anglikana Tanzania,
Dr. Valentino Mokiwa, Askofu Mkuu wa Dayosisi ya Morogoro la Kanisa la Kiinjili la
Kilutheri Tanzania (KKKT), Jacob Mameo Ole Paulo, Askofu Mkuu wa Kanisa la Kimethodisti
la Tanzania, Dkt. Mathew Peter Byamungu, Mkurugenzi wa CIT katika Tanzania, Mchungaji
Joseph Mayala, Maaskofu na Wachungaji wa makanisa mbali mbali nchini.
Wazazi
500 kutoka vituo viwili vya Huduma ya Mtoto Mkoa wa Pwani vilivyoko katika Kanisa
la KKKT, Dayosisi ya Morogoro, Jimbo la Chalinze, Usharika wa Chalinze na Mtaa wa
Msoga na katika Kanisa la Anglikana la Mtakatifu Benedicto la Mlandizi watanufaika
na mradi huo wa mbuzi wa maziwa na kuku unaofadhiliwa na CIT kwa kiasi cha Sh. 95,
497,000.
Chini ya mradi huo, kiasi cha mbuzi wa maziwa 300 na kuku kiasi cha
1,000 watagawiwa bure kwa wananchi na hasa kwa familia zilizoko kwenye umasikini na
mpaka sasa wazazi 250 wamepewa mafunzo ya kuweza kuendeleza miradi ya mbuzi wa maziwa
na kuku.
Mbali na kutoa mbuzi watatu na kuku watatu kwa wawakilishi wa wananchi
hao, Rais Kikwete pia ametoa vyandarau 250 kwa watoto kutoka familia za vituo hivyo
viwili, ni sehemu ya vituo vyenye watoto 67, 280 ambao CIT inawafadhili kupitia Programu
ya Maendeleo ya Mtoto, moja ya program tatu zinazoendeshwa na CIT katika Tanzania
ambako taasisi hiyo iliingia rasmi Oktoba 30, mwaka 1999.
CIT pia inafadhili
watoto wengine 1,164 kwenye Programu ya Kunusuru Maisha ya Mama na Mtoto katika mikoa
13 ya Tanzania ambako taasisi hiyo inashirikiana na makanisa ya Kiinjili yapatayo
262 kutoka Madhehebu 22 ya Kikristo. Mikoa ambako CIT ina shughuli zake ni Pwani,
Arusha, Manyara, Dodoma, Kilimanjaro, Singida, Morogoro, Mwanza, Tabora, Shinyanga,
Mara, Iringa na Dar es Salaam. CIT ambayo ilianzishwa miaka 61 iliyopita nchini Korea
Kusini ina makao yake Colorado Springs, Marekani.
Akizungumza mara baada ya
kukabidhi mbuzi na kuku hao, Rais Kikwete amelishukuru CIT kwa misaada yake ya kupambana
na umasikini na kuboresha afya ya Watanzania. Amesema kuwa masikini hawako Tanzania
peke yake na ndiyo maana makao makuu ya taasisi hiyo yako Marekani. “Wakati mwingine
ukisikiliza watu utadhani umasikini uko Tanzania peke yake. Siyo kweli na ndiyo maana
CIT ina ofisi zake Marekani inafanya kazi huko.
Hivi tunavyozungumza kiasi
cha watoto milioni 67 wenye umri wa kwenda shule duniani ambao hawaendi shule, sisi
katika Tanzania kiwango cha watoto wenye umri wa kwenda shule wanaokwenda shule ni
asilimia 97. Bado asilimia tatu tu,” amesema Rais Kikwete na kuongeza: “Watu milioni
300 duniani kwa sasa hawana uhakika na mlo wao unaofuata utatoka wapi. Watu milioni
650 duniani hawana makazi salama duniani. Hivyo, ndugu zangu siyo Tanzania tu.”