2013-01-04 07:34:29

Baba Mtakatifu Benedikto XVI wakati wa Siku kuu ya Epifania atawaweka wakfu Maaskofu wakuu wateule!


Monsinyo Guido Marini, Mshereheshaji mkuu wa Ibada za Kipapa mjini Vatican anabainisha kwamba, Mama Kanisa katika maadhimisho ya Siku kuu ya Tokeo la Bwana, maarufu kama Epifania anatumia fursa hii pia kutangaza “Mbiu ya Pasaka” inayoonesha jinsi ambavyo Kanisa litaendelea kumtangaza na kumwonesha Kristo miongoni mwa Mataifa katika maadhimisho mbali mbali yatakayofanywa na Mama Kanisa katika kipindi cha Mwaka 2013. RealAudioMP3
Ikumbukwe kwamba, kazi ya ukombozi inafikia kilele chake katika Fumbo la Pasaka, yaani, mateso, kifo na ufufuko wa Kristo, unaopania kumkomboa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti.
Tukio la Mamajusi kutoka Mashariki waliongozwa na nyota kwenda Bethlehemu kumwona Mfalme wa Wayahudi aliyezaliwa ni tukio la kwanza kabisa linaloonesha Ufunuo wa Bwana kwa watu wa Mataifa katika ulimwengu. Yesu Kristo ni mwanga wa mataifa na kilele cha historia ya maisha ya mwanadamu; Yeye ni mwanzo na mwisho, Alfa na Omega; Nyakati zote ni zake. Yesu Kristo ndiye anayeongoza hija ya maisha ya mwanadamu inayohitimishwa kwa njia ya mateso, kifo, ufufuko na kupaa kwake mbinguni.
Monsinyo Marini anasema, ndiyo maana katika maadhimisho ya Siku kuu ya Tokeo la Bwana, Kanisa linatangaza “Mbiu ya Pasaka” inayopembua matukio makuu ya Maadhimisho ya Mwaka wa Kanisa mintarafu Historia ya Ukombozi inayojikita katika Siku kuu tatu muhimu katika maisha na utume wa Kristo: Mateso, kifo na ufufuko wake: Jumaa kuu.
Katika maadhimisho ya Siku kuu ya Tokeo la Bwana, hapo tarehe 6 Januari 2013, Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, anatarajiwa kuwaweka wakfu Maaskofu wakuu wapya wanne nao ni: Monsinyo Vincenzo Zani, Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la Elimu Katoliki; Monsinyo Fortunatus Nwachukwu aliyeteuliwa kuwa Balozi wa Vatican nchini Nicaragua; Monsinyo Nicolas Thevenin aliyeteuliwa kuwa Balozi wa Vatican pamoja na Monsinyo Georg Ganswein, katibu muhtasi wa Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, aliyeteuliwa pia kuwa ni Mkuu wa Nyumba ya Kipapa.
Katika Ibada hii, Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, anatarajiwa kusaidiwa na Kardinali Tarcisio Bertone, Katibu mkuu wa Vatican pamoja na Kardinali Zenon Grocholewski. Maaskofu wakuu wateule watatambulishwa kwa Baba Mtakatifu na Kardinali Marc Ouellet, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya Maaskofu.








All the contents on this site are copyrighted ©.