2013-01-03 07:24:26

Mafundisho Jamii ya Kanisa Katoliki katika kutetea haki msingi za binadamu


Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican inakuletea kwa mapana mchango wa Kanisa Katoliki katika kulinda na kutetea haki msingi za binadamu, kama unavyopembuliwa na Kardinali Peter Turkson, Rais wa Baraza la Kipapa la Haki na Amani. RealAudioMP3

Baraza la Kipapa la Haki na Amani tangu kuanzishwa kwake mara tu baada ya maadhimisho ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, limekuwa mstari wa mbele katika kulinda, kusimamia na kutetea haki msingi za binadamu, kama ambavyo zimebainishwa katika Azimio la Haki Msingi za Binadamu, lililotolewa na Umoja wa Mataifa kunako mwaka 1948.

Baba Mtakatifu Yohane wa Ishirini na tatu ni kati ya viongozi wa Kanisa Katoliki walioweka bayana umuhimu wa kusimama kidete kulinda na kutetea haki msingi za binadamu zinazojikita katika utu wa binadamu pamoja na uhuru wa kuabudu mintarafu sheria za kimataifa na kitaifa. Hizi ni kanuni msingi zinazobainishwa katika Mafundisho Jamii ya Kanisa, yanayopania kuyatakatifuza malimwengu.

Kwa bahati mbaya anasema Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, haki msingi za binadamu na uhuru wa kuabudu ni kati ya mambo ambayo kwa sasa yako hatarini kutokana na sababu mbali mbali, ndiyo maana kuna haja kwa wadau mbali mbali kusimama kidete kuhakikisha kwamba, haki msingi za binadamu, utu na heshima yake vinalindwa na kudumishwa sehemu mbali mbali za dunia.

Tamko la Haki Msingi za Binadamu la Umoja wa Mataifa ni matokeo ya tafakari ya kina iliyofanywa na viongozi wa Jumuiya ya Kimataifa kuhusu athari zilizokuwa zimesababishwa na vita kuu ya kwanza na ile ya pili ya dunia; ambapo kuna watu wengi walipoteza maisha na mali; utu na heshima yao vikawekwa rehani. Walitaka kuweka kanuni msingi ambazo zimengefutwa na Jumuiya ya Kimataifa.

Hizi ni haki ambazo zinafumbatwa katika uhuru, haki na amani duniani. Huu ni urithi wa binadamu wa nyakati zote na mahali pote bila ubaguzi, kwani zinapata chimbuko lake kutoka kwa binadamu mwenyewe aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu na kwamba ni sehemu ya asili ya binadamu.

Ni mchango wa Kardinali Peter Turkson, Rais wa Baraza la Kipapa la Haki na Amani alioutoa hivi karibuni kwenye Kongamano la Kimataifa lililokuwa linajadili kuhusu dhamana ya Kanisa Katoliki katika kulinda na kutetea haki msingi za binadamu, kwa kutambua kuwa haki hizi zinafumbata utu wa mtu, tangu pale anapotungwa mimba tumboni mwa mama yake, hadi mauti ya kawaida yanapomsibu kadiri ya mpango wa Mungu.

Tangu mwaka 1948 haki hizi zilipotangazwa na Umoja wa Mataifa, Kanisa limeendelea kuzipigania ili ziweze kutekelezwa na Jumuiya ya Kimataifa na wala zisibaki kwenye makabati tu, kama kumbu kumbu ya nyaraka za kale.

Baba Mtakatifu Yohane wa ishirini na tatu, aliguswa kwa namna ya pekee na kinzani, wasi wasi na woga uliokuwa umetanda wakati wa Vita Baridi sanjari na ujenzi wa Ukuta wa Berlin, Ujerumani, alipoandika Waraka wa Kichungaji, Amani Duniani, Pacem In Terris, akakazia mambo makuu manne kama vigezo vya kudumisha haki msingi za binadamu: amani katika ukweli, haki, upendo na uhuru. Hizi ni tunu ambazo ni urithi mkubwa kwa binadamu wote kwani zinabubujika kutoka katika asili ya binadamu, hivyo zinapaswa kulindwa, kutetewa na kuheshimiwa na wote; kwa kuzingatia kwamba, haki inakwenda sanjari na wajibu; hakuna haki pasi na wajibu.

Hii ni haki ya kuishi, kupata huduma bora ya makazi, afya, elimu, kuabudu, uhuru wa dhamiri, uhuru wa kuchagua mfumo wa maisha; haki za kicuhumi na kisiasa pamoja na uhuru wa kwenda unakotaka kwa kuzingatia sheria na kanuni zilizopo.

SEHEMU YA PILI

Kardinali Peter Turkson, Rais wa Baraza la Kipapa la haki na amani, anaendelea kuchambua mchango wa Kanisa Katoliki katika kulinda, kutetea na kuhamasisha haki msingi za binadamu, leo anabaianisha asili ya haki msingi za binadamu zinazopaswa kuheshimiwa na kuthaminiwa na wote.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, alipolihutubia Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kunako mwaka 2008 alikazia juu ya haki msingi za binadamu ambazo ziko hatarini kutokana na baadhi ya watu kuziondoa mahali pake, kinyume kabisa cha sheria asilia ambayo imeandikwa katika dhamiri ya mtu. Matokeo yake ni baadhi ya watu kuwa na mwono tofauti unaokinzana kutokana na tofauti za kitamaduni, kisiasa, kijamii na kidini.

Kuna baadhi ya watu wanaotaka kuibua sera ambazo zitaandika upya haki msingi za binadamu, zinazotaka kutetea misimamo yao ya kisiasa na kiuchumi; kwa kutaka kukumbatia utamaduni wa kifo kwa kisingizio cha haki msingi za uzazi salama pamoja na ndoa za watu wa jinsia moja.

Kanisa Katoliki lina utajiri mkubwa wa Mafundisho Jamii ya Kanisa yanayopata chimbuko lake katika Waraka wa Kichungaji wa Baba Mtakatifu Leo wa kumi na tatu; Mambo Mapya; Rerum Novarum; Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili, katika Waraka wake kuhusu Masuala ya Kijamii Centesimus Annus, akafafanua kwa kina kuhusu asili ya haki msingi za binadamu; umuhimu wa kukuza na kudumisha upendo na mshikamano miongoni mwa Jumuiya ya Kimataifa, kama inavyojidhihirisha katika Waraka wake wa Sollicitudo Rei Socialis, cheche ya uanzishaji wa vyama vya kijamiii vilivyokuwa vinapania kulinda na kutetea uhuru na haki msingi za binadamu.

Haki msingi za binadamu zinasimikwa kwa namna ya pekee anasema Kardinali Peter Turkson katika uhai, elimu, afya, familia na uhuru wa kuabudu, kwani haya ni masuala yanayogusa undani wa utu na heshima ya kila binadamu. Baba Mtakatifu Yohane Paulo wa pili akatamka wazi kwamba, uhuru wa kidini ni muhtasari wa haki zote msingi za binadamu; kama ambavyo pia walikwishatilia mkazo Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican kuhusu utu wa mwanadamu na kweli za kidini zinazofumbatwa katika kanuni maadili.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, katika Ujumbe wake kwa Maadhimisho ya Siku ya kuombea Amani Duniani kwa mwaka 2012 alibainisha mambo yanayoendelea kuhatarisha uhuru wa mtu katika kuabudu, kiasi kwamba, hata alama za kidini nazo sasa zimekuwa ni sehemu ya kero za binadamu. Wakristo ni watu ambao wameendelea kudhulumiwa kwa kiasi kikubwa sehemu mbali mbali za dunia. Hapa Serikali zinakumbushwa wajibu wao wa kulinda maisha na mali za raia wao bila upendeleo.

Misimamo mikali ya kidini ni jambo la hatari kabisa linalotishia misingi ya haki, amani, utulivu na mshikamano wa kitaifa na kwamba, kuna wakati siasa zinatumia dini kwa ajili ya mafao yake binadamu. Tatizo la ukanimungu na mawazo mepesi mepesi yanataka kumwondoa Mwenyezi Mungu katika mipango na mikakati ya maisha ya mwanadamu, yaani kuwa na uhuru usiokuwa na mipaka wala kuwajibisha.

Dini zina wajibu wa kudumisha misingi ya haki, amani, ukweli, majadiliano na upatanisho; kwa kuheshimiana na kuthaminiana hata katika tofauti zao msingi. Serikali na Kanisa vinaweza kushirikiana zaidi kwa ajili ya kutafuta mafao ya wengi na kudumisha amani na utulivu.

SEHEMU YA TATU

Kardinali Peter Turkson anabainisha kwamba, ili Jamii iweze kusimama kidete kulinda na kutetea haki msingi za binadamu, kuna haja kwa Jamii kuwekeza katika elimu ya dini hasa miongoni mwa Vijana wa kizazi kipya kama anavyobainisha Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita. Jumuiya ya Kimataifa ijifunge kibwebwe kupambana fika na baa la umaskini wa kipato na hali bila kusahau ujinga ambao pia umeendelea kutumiwa na baadhi ya watu kuleta maafa katika Jamii.

Baa la Umaskini linaweza kutoweka kwa njia ya mshikamano wa kimataifa unaoongozwa na kanuni auni na wala si katika kuwekeza sera zinazokumbatia utamaduni wa kifo kwa kudhani kwamba, ongezeko kubwa la watu duniani ni kikwazo cha maendeleo. Jamii haiwezi kuondokana na baa la umaskini kwa kuwauwa maskini, badala yake wajengewe uwezo wa kielimu na kiuchumi ili kupambana vyema na mazingira yao, yaweze kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi.

Ni wajibu wa kila mtu kuheshimu uhuru wa kisiasa, kiuchumi na kidini kama sehemu ya mchakato wa kujenga na kudumisha amani na maridhiano katika Jamii. Familia zitekeleze wajibu wake msingi katika Jamii na wala isiwekewe kinzani na pingamizi zinazobomoa tunu msingi za maisha ya ndoa na familia kwa hoja ya kutaka kukuza na kudumisha haki msingi za binadamu. Jamii ielimishwe kuhusu haki msingi za binadamu na iwe tayari kuzitetea kwa udi na uvumba.

Kardinali Peter Turkson, Rais wa Baraza la Kipapa la haki na amani anahitimsiha mchango wake kuhusu dhamana ya Kanisa Katoliki katika kudumisha na kukuza haki msingi za binadamu kwa kusema kwamba, uhuru wa kidini hauna budi kutambuliwa kuwa ni muhtasari wa haki zote za binadamu. Dini zisaidie kujenga amani, upendo na mshikamano ndani ya Jamii na kamwe zisiwe ni chanzo cha vurugu, kinzani na vita.

Kanuni maadili na utu wema ni sehemu muhimu sana katika maisha ya mwanadamu zinazopaswa kuheshimiwa ili amani na utulivu viweze kushika kasi, bila kusahau nafasi na dhamana ya uwepo wa Mungu katika maisha ya mwanadamu. Waamini wafahamu fika kweli za imani yao ili wasiyumbishwe, bali wasimame kidete kuilinda na kuitetea kwa ajili ya mafao ya wengi na maendeleo ya Jamii.

Imeandaliwa na Padre Richard Mjigwa, C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.